Tunaweza Kufanya Nini Tunapovunjika Moyo?
MTU anaweza kupambanaje na kuvunjika moyo? Waangalizi kadhaa wasafirio, ambao huzuru makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida, waliulizwa swali hilo. Majibu yao yanaweza kutusaidia kuchanganua visababishi vya kuvunjika moyo na njia za kurekebisha hali hii ambayo yaweza kumwathiri Mkristo yeyote.
Ili kukabiliana na kuvunjika moyo, tunahitaji kufanya mengi kuliko tu kuchunguza mambo, lakini ishara zake zaweza kutia ndani kutopendezwa na sala au funzo la kibinafsi, kutohudhuria mikutano kwa ukawaida, kutokuwa na shauku, na hata kuwa na ubaridi fulani kwa Wakristo wenzetu. Hata hivyo, ishara iliyo wazi zaidi ni kupunguza bidii katika kueneza evanjeli. Ebu tuchunguze ishara hizo na kufikiria njia za kuzirekebisha.
Kuvunjika Moyo Katika Kazi Yetu ya Kueneza Evanjeli
Yesu Kristo alijua matatizo yaliyohusiana na utume wa kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Aliwatuma wafuasi wake kama “kondoo katikati ya mbwa-mwitu,” akijua kwamba kazi yao ya kuhubiri ingefanya wanyanyaswe. (Mathayo 10:16-23) Lakini hiyo haingekuwa sababu ya kuwavunja moyo. Kwa kweli, mara nyingi mnyanyaso umewaimarisha watumishi wa Yehova ambao wamemtegemea kupitia sala.—Matendo 4:29-31; 5:41, 42.
Wanafunzi wa Kristo hawakuwa wakipokewa vizuri sikuzote hata wakati ambapo hawakuwa wakinyanyaswa vikali. (Mathayo 10:11-15) Vivyo hivyo leo, kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova haifanywi sikuzote bila matatizo.a Kwa watu wengi, imani katika Mungu ni jambo la kibinafsi wasilopenda kulizungumzia. Wengine hawajihusishi kamwe na mashirika ya kidini ambayo kwa kadiri fulani hawayapendelei. Bila shaka, ubaridi, kutokuwa na matokeo, au matatizo mengine mbalimbali yanaweza kuwa visababishi vikubwa vya kuvunjika moyo. Vizuizi hivyo vyaweza kushindwaje?
Kupata Matokeo Mazuri Zaidi
Furaha tupatayo katika huduma yetu yahusiana kwa kadiri fulani na matokeo tupatayo. Hivyo basi, tunawezaje kuwa wenye matokeo zaidi katika huduma? Sisi ni “wavuvi wa watu.” (Marko 1:16-18) Wavuvi katika Israeli la kale walikuwa wakienda kuvua samaki usiku wakati ambapo wangeweza kuvua samaki wengi zaidi. Sisi pia twahitaji kuchanganua eneo letu ili twende “kuvua” wakati ambapo watu wengi wako nyumbani na wanapokuwa wenye kuitikia zaidi ujumbe wetu. Huo unaweza kuwa wakati wa jioni, mwisho-juma, au wakati mwingine. Kwa mujibu wa mwangalizi mmoja asafiriye, jambo hilo linawezekana katika maeneo ambapo watu hufanya kazi siku nzima. Yeye asema kwamba kutoa ushahidi wakati wa jioni mara nyingi huleta matokeo mazuri sana. Kutoa ushahidi kwa simu au kivivi hivi pia hutuwezesha kufikia watu wengi zaidi.
Kuvumilia katika huduma huleta matokeo mazuri. Katika Ulaya Mashariki na katika nchi fulani za Afrika, kazi ya kuhubiri Ufalme inaendelea vizuri, na jambo hilo limetokeza maongezeko mazuri. Vivyo hivyo, makutaniko mengi yamefanyizwa katika maeneo ambayo kwa muda mrefu yamefikiriwa kuwa hayana matokeo au hata katika maeneo yanayohubiriwa mara nyingi sana. Hata hivyo, vipi ikiwa hupati matokeo kama hayo katika eneo lenu?
Kudumisha Mtazamo Ufaao
Kukumbuka vizuri miradi aliyoweka Yesu kutatusaidia tusivunjike moyo tunapokabili ubaridi katika huduma yetu. Kristo alitaka wanafunzi wake watafute wale wenye kustahili, bali si kuongoa watu kwa wingi. Katika pindi kadhaa, alitaja kwamba watu wengi wangekataa habari njema, kama vile Waisraeli wengi walivyokataa kuwasikiliza manabii wa zamani.—Ezekieli 9:4; Mathayo 10:11-15; Marko 4:14-20.
‘Habari njema ya ufalme’ hupokewa kwa shukrani na watu “wenye kuona uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3; 24:14) Wanataka kumtumikia Mungu katika njia ambayo yeye ameonyesha. Hivyo, matokeo ya kazi yetu yahusiana zaidi na hali ya mioyo ya watu kuliko ustadi wetu katika kuwasilisha ujumbe. Bila shaka, twahitaji kufanya yote tuwezayo ili kufanya habari njema ivutie. Hata hivyo, matokeo yanategemea Mungu, kwa kuwa Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.”—Yohana 6:44.
Kazi yetu ya kueneza evanjeli hujulisha jina la Yehova. Watu wasikilize au wasisikilize, kazi yetu ya kuhubiri huchangia kutakaswa kwa jina takatifu la Yehova. Isitoshe, kwa kazi yetu ya kueneza evanjeli, twathibitisha kwamba sisi ni wanafunzi wa Kristo, na tuna pendeleo la kushiriki katika utume muhimu zaidi unaotekelezwa wakati wetu.—Mathayo 6:9; Yohana 15:8.
Kuvunjika Moyo na Mahusiano
Mahusiano fulani ya wanadamu, yawe katika familia au kutanikoni, yanaweza kuvunja moyo. Kwa mfano, kuna hali ya kuona kwamba watu hawakuelewi. Huenda kutokamilika kwa waamini wenzetu kukatuvunja moyo. Kwa mara nyingine, Maandiko yanaweza kutusaidia sana.
“Ushirika mzima wa ndugu” ulimwenguni pote hufanyiza familia kubwa sana ya kiroho. (1 Petro 2:17) Lakini kule kujihisi kuwa sehemu ya watu wenye muungano kunaweza kufifia wakati matatizo yanapotokezwa na mahitilafiano ya nyutu. Yaonekana kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walipata matatizo hayo pia, kwa kuwa ilimlazimu mtume Paulo awakumbushe tena na tena kuishi pamoja katika muungano. Kwa mfano, aliwahimiza wanawake wawili Wakristo—Euodia na Sintike—wamalize tofauti zao.—1 Wakorintho 1:10; Waefeso 4:1-3; Wafilipi 4:2, 3.
Ikiwa hilo ndilo tatizo, tunaweza kuchocheaje tena upendo wa kweli kwa ndugu na dada zetu? Kwa kujikumbusha kwamba Kristo alikufa kwa ajili yao na kwamba wao, kama sisi, wamedhihirisha imani katika dhabihu yake ya fidia. Twaweza pia kukumbuka kwamba wengi wa ndugu zetu wako tayari kumwiga Yesu Kristo kwa kuhatarisha uhai wao kwa ajili yetu.
Miaka kadhaa iliyopita, huko Paris, Ufaransa, bila kusita Shahidi kijana alichukua sanduku lililokuwa na bomu ambalo lilikuwa limewekwa nje ya Jumba la Ufalme. Aliteremka mbio kwenye ngazi kadhaa kabla ya kulitupa ndani ya chemchemi, ambapo lililipuka. Alipoulizwa ni nini kilichomchochea ahatarishe maisha yake kwa njia hiyo, alijibu: “Nilitambua kwamba uhai wetu ulikuwa hatarini. Hivyo nikaona ni afadhali mimi nife peke yangu kuliko sisi sote kufa.”b Ni baraka iliyoje kuwa na marafiki kama hao walio tayari kumfuata Yesu kwa makini!
Isitoshe, twaweza kutafakari juu ya roho ya ushirikiano iliyokuwako miongoni mwa Mashahidi wa Yehova waliokuwa kwenye kambi za mateso wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili.c Hivi karibuni, ndugu na dada zetu nchini Malawi walionyesha uaminifu huohuo waliposimama imara wakiwa Wakristo wa kweli. Je, wazo la kwamba ndugu zetu katika kutaniko letu wangetenda vivyo hivyo chini ya hali ngumu halituchochei kutotilia maanani au angalau kuyapunguza matatizo na magumu ya kila siku? Tukisitawisha akili ya Kristo, mahusiano yetu ya kila siku pamoja na waabudu wenzetu yatatuburudisha, wala hayatavunja moyo.
Hisia za Kibinafsi Zenye Kuvunja Moyo
“Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.” (Mithali 13:12) Kwa maoni ya baadhi ya watumishi wa Yehova, mwisho wa mfumo huu wa mambo umekawia. Wakristo huona wakati ambamo tunaishi kuwa ‘hatari na mgumu kushughulika nao,’ kama vile wengi wasioamini wauonavyo.—2 Timotheo 3:1-5.
Hata hivyo, tofauti na wasioamini, Wakristo wapaswa kufurahi kuona katika hali hizi zenye majaribu ile “ishara” ya kuwapo kwa Yesu, inayoonyesha kwamba karibuni Ufalme wa Mungu utakomesha mfumo huu mwovu wa mambo. (Mathayo 24:3-14) Hata hali zikizidi kuwa mbaya zaidi—kama vile ambavyo kwa hakika itakuwa wakati wa “dhiki kubwa”—matukio hayo hutufurahisha kwa sababu ni ishara ya kuja kwa ulimwengu mpya wa Mungu.—Mathayo 24:21; 2 Petro 3:13.
Kuahirisha katika akili uingiliaji wa Ufalme katika mambo ya siku hizi kwaweza kufanya Mkristo atumie wakati mwingi zaidi akifuatia vitu vya kimwili. Akitumia wakati wake wote katika mambo kama kazi ya kimwili na vitumbuizo, itakuwa vigumu kwake kutimiza madaraka ya Kimaandiko ifaavyo. (Mathayo 6:24, 33, 34) Mtazamo kama huo hutokeza kukata tamaa na hivyo kuvunjika moyo. Mwangalizi mmoja asafiriye alieleza hivi: “Si jambo la akili kujaribu kuishi kana kwamba uko katika ulimwengu mpya ilhali uko katika mfumo huu mwovu wa mambo.”
Njia Mbili Bora za Kurekebisha Hali
Mtu anawezaje kurekebisha hali vizuri anapotambua tatizo lake? Funzo la kibinafsi ni mojawapo ya njia bora awezazo kutumia. Kwa nini? “Hilo hutukumbusha ni kwa nini yatupasa kufanya yale tufanyayo,” akasema mwangalizi mmoja asafiriye. Mwingine pia alieleza hivi: “Kuhubiri tu kutimiza wajibu hatimaye huchosha.” Lakini funzo zuri la kibinafsi hutusaidia kubainisha kabisa daraka letu tukaribiapo mwisho. Kwa kupatana na hayo, Maandiko hutukumbusha tena na tena uhitaji wa kula vizuri kiroho ili tufurahie kikweli kufanya mapenzi ya Mungu.—Zaburi 1:1-3; 19:7-10; 119:1, 2.
Wazee wanaweza kuwasaidia wengine washinde mvunjiko wa moyo kwa kuwafanyia ziara za uchungaji zenye kutia moyo. Wakati wa ziara hizi za faragha, wazee wanaweza kuonyesha kwamba kila mmoja wetu anathaminiwa sana na kwamba ana fungu kubwa miongoni mwa watu wa Yehova. (1 Wakorintho 12:20-26) Akizungumza juu ya Wakristo wenzake, mzee mmoja alisema: “Ili kukazia thamani yao, mimi huwakumbusha yale waliyotimiza wakati uliopita. Huwaambia kwamba wao ni wenye thamani mbele ya macho ya Yehova na kwamba damu ya Mwana wake ilitolewa kwa niaba yao. Sikuzote wao huitikia vizuri kusababu huko. Kusababu huko kunapoimarishwa kwa marejezo mazuri ya Biblia, wale waliovunjika moyo huweza kuweka miradi mipya, kama vile kusali wakiwa familia, kujifunza na kusoma Biblia.”—Waebrania 6:10.
Wakati wa ziara za uchungaji, wazee wanahitaji kutahadhari wasifanye ionekane kana kwamba ni vigumu kumpendeza Mungu. Badala yake, wazee wanaweza kuwasaidia waabudu wenzao waliovunjika moyo waelewe kwamba mzigo wa wafuasi wa Yesu ni mwepesi. Hivyo, utumishi wetu wa Kikristo unatuletea furaha.—Mathayo 11:28-30.
Kushinda Mvunjiko wa Moyo
Mvunjiko wa moyo ni tatizo tupaswalo kupambana nalo hata uwe wasababishwa na nini. Kumbuka pia kwamba hatuko peke yetu katika pambano hilo. Ikiwa tumevunjika moyo, na tukubali msaada wa Wakristo wenzetu, hasa wazee. Kwa kufanya hivyo, tunaweza kupunguza hisia za kuvunjika moyo.
Zaidi ya yote, twahitaji kumgeukia Mungu ili kupata msaada wa kushinda mvunjiko wa moyo. Tukimtegemea Yehova kupitia sala, anaweza kutusaidia kushinda kabisa mvunjiko wa moyo. (Zaburi 55:22; Wafilipi 4:6, 7) Kwa vyovyote, sisi tukiwa watu wake tuna maoni kama ya mtunga-zaburi aliyeimba: “Heri watu wale waijuao sauti ya shangwe, Ee BWANA, huenenda katika nuru ya uso wako. Kwa jina lako hufurahi mchana kutwa, na kwa haki yako hutukuzwa. Maana fahari ya nguvu zao ni Wewe, na kwa radhi yako pembe yetu itatukuka.”—Zaburi 89:15-17.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Ugumu wa Kwenda Nyumba Hadi Nyumba” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1981 (la Kiingereza).
b Ona ukurasa wa 12 na 13 wa gazeti la Amkeni! la Februari 1986, lililochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
c Ona makala “Niliokoka ‘Msafara wa Kifo’” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1980 (la Kiingereza), na makala “Kushika Ukamilifu Katika Ujerumani ya Nazi” katika gazeti la Amkeni! la Juni 1986.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Ziara za uchungaji zenye kujenga zifanywazo na wazee wenye upendo zaweza kusaidia Wakristo washinde mvunjiko wa moyo