Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w08 4/1 kur. 21-23
  • Jinsi Ambavyo Ufalme wa Kale wa Lidia Unatuhusu Leo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Ambavyo Ufalme wa Kale wa Lidia Unatuhusu Leo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mawe ya Kuthibitishia ya Mfano Katika Biblia
  • Fumbo Lafumbuliwa
  • Lidia—Mwabudu wa Mungu Mkaribishaji-Wageni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Mfano wa Kuigwa—Lidia
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
  • Maisha Katika Nyakati za Biblia—Pesa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Helo—Mateso ya Milele au Kaburi la Ujumla?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
w08 4/1 kur. 21-23

Jinsi Ambavyo Ufalme wa Kale wa Lidia Unatuhusu Leo

HUENDA hujawahi kamwe kusikia kuhusu ufalme wa kale wa Lidia, hivyo, unaweza kushangaa kujua kwamba ugunduzi uliofanywa huko ulibadili jinsi ulimwengu unavyofanya biashara. Wasomaji wa Biblia wanaweza pia kushangaa kujua kwamba uvumbuzi wa Walidia unatusaidia kuelewa unabii fulani wa Biblia wenye kutatanisha. Watu wa Lidia waligundua nini? Kabla hatujajibu swali hilo, itapendeza kujua mambo fulani kuhusu milki hiyo iliyo karibu kusahauliwa.

Wafalme wa Lidia walitawala kutoka mji wao mkuu, Sardi, upande wa magharibi wa nchi ambayo wakati huo ilikuwa ikiitwa Asia Ndogo lakini sasa inaitwa Uturuki. Mfalme wa mwisho wa Lidia, Croesus, alikusanya mali nyingi sana, lakini karibu mwaka wa 546 K.W.K., milki yake ilitwaliwa na Koreshi Mkuu wa Uajemi ambaye miaka michache baadaye alishinda Milki ya Babiloni.

Inasemekana kwamba wafanyabiashara werevu wa Lidia ndio waliokuwa wa kwanza kutumia sarafu. Kwa muda mrefu, dhahabu na fedha zilitumiwa kama pesa, lakini kwa sababu ya ukubwa tofauti-tofauti wa vipande na pete za dhahabu, watu walilazimika kuzipima kila mara walipofanya biashara. Kwa mfano, huko Israeli, Yeremia nabii wa Mungu alinunua shamba na akaandika hivi: “Nikaanza kumpimia pesa, shekeli saba na vipande kumi vya fedha.”—Yeremia 32:9.

Huko Lidia, watu walioishi wakati mmoja na Yeremia waligundua kitu fulani cha kurahisisha biashara—matumizi ya sarafu zenye uzani sawa zilizotiwa muhuri rasmi. Sarafu za kwanza za Lidia zilitengenezwa kutokana na mchanganyiko wa dhahabu na fedha. Croesus alipokuwa mfalme, aliondoa sarafu hizo na badala yake akaleta sarafu za fedha na za dhahabu kamili. Walidia walitokeza mfumo wa pesa wa kutumia sarafu za madini ya aina mbili tofauti. Katika mfumo huo thamani ya sarafu 12 za fedha ilitoshana na thamani ya sarafu 1 ya dhahabu. Lakini mfumo huo ulihatarishwa na matumizi ya sarafu bandia za dhahabu iliyochanganywa na madini zenye thamani ya chini. Wafanyabiashara walihitaji njia rahisi ya kuchunguza ikiwa ilikuwa dhahabu kamili.

Walidia waligundua kwamba jiwe fulani jeusi la eneo lao ambalo liliitwa jiwe la Lidia lingetatua tatizo hilo. Sarafu inaposuguliwa kwenye jiwe hilo laini lakini lenye kukwaruza kidogo inafanyiza alama. Rangi ya alama hiyo ikilinganishwa na rangi ya sindano zilizokuwa na kiasi hususa cha dhahabu, kiasi cha dhahabu katika sarafu hiyo kilijulikana. Ugunduzi huo, yaani, kutumia jiwe la kuthibitishia, ndio uliofanya iwezekane kuwa na mfumo unaotegemeka wa kutumia sarafu. Kuyafahamu mawe ya kuthibitishia kunatusaidia jinsi gani kuielewa Biblia?

Mawe ya Kuthibitishia ya Mfano Katika Biblia

Kadiri zoea la kuchunguza dhahabu kwa kutumia jiwe la kuthibitishia lilivyoenea miongoni mwa wafanyabiashara, neno lililotumiwa kurejelea jiwe hilo lilikuja kumaanisha njia ya kujaribia. Katika Kigiriki, lugha iliyotumiwa kuandika sehemu ya Biblia, neno hilo lilitumiwa pia kurejelea mateso ya watu waliojaribiwa kwa kuteswa vikali.

Kwa sababu walinzi wa gereza ndio waliowatesa wafungwa, neno lililotokana na jiwe la kuthibitishia lilitumiwa kuwahusu walinzi wa gereza. Hivyo, Biblia inarekodi mfano wa Yesu kumhusu mtumwa asiye na shukrani ambaye alikabidhiwa kwa “walinzi wa gereza,” au katika tafsiri nyingine, “watesaji.” (Mathayo 18:34; American Standard Version, Darby, King James Version) Kuhusu andiko hilo, kitabu fulani (The International Standard Bible Encyclopaedia) kinasema hivi: “Huenda kufungwa gerezani ndiko kulikoonwa kuwa ‘kuteswa’ (na bila shaka ndivyo kulivyokuwa), nalo neno ‘watesaji’ likamaanisha tu walinzi wa gereza.” Hilo linatusaidia kufafanua andiko fulani lenye kutatanisha katika Biblia.

Fumbo Lafumbuliwa

Kwa muda mrefu, wasomaji wanyoofu wa Biblia wamejiuliza ni nini kitakachompata Shetani. Biblia inasema: “Ibilisi . . . alitupwa ndani ya lile ziwa la moto na kiberiti, ambamo wote wawili, yule mnyama-mwitu na yule nabii wa uwongo, tayari walikuwa; nao watateswa mchana na usiku milele na milele.” (Ufunuo 20:10) Bila shaka, ikiwa Yehova angechukua hatua ya kumpa mtu uzima wa milele pamoja na mateso, hatua hiyo ingepingana na upendo na haki ya Mungu. (Yeremia 7:31) Zaidi ya hilo, Biblia inaonyesha kwamba uzima wa milele ni zawadi wala si adhabu. (Waroma 6:23) Hivyo basi, andiko la Ufunuo 20:10 linatumia lugha ya mfano. Mnyama-mwitu na ziwa la moto ni mifano. (Ufunuo 13:2; 20:14) Je, mateso hayo pia ni ya mfano? Kwa kweli, neno hilo linamaanisha nini?

Kama tulivyoona, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kutesa” linatokana na neno lililotumiwa kurejelea jiwe la kuthibitishia na linaweza kurejelea mateso ya kufungwa gerezani. Hivyo, kuteswa kwa Shetani kunaweza kurejelea kufungwa milele katika gereza lenye ulinzi mkali kabisa, yaani, kifo.

Jiwe la kuthibitishia la Lidia linatusaidia kuelewa jambo lingine linalohusu ‘kuteswa’ milele kwa Shetani ambalo linapatana na upendo wa Mungu. Kama vile Walidia walivyotumia jiwe la kuthibitishia kuwa kiwango cha kujaribia pesa, ‘kuteswa’ au kifo cha milele cha Shetani kitakuwa kiwango cha milele kitakachotumiwa iwapo uasi wowote utatokea wakati ujao. Yeyote akipinga utawala wa Yehova, hakutakuwa kamwe na uhitaji wa kuchukua tena muda mrefu ili kuthibitisha kwamba mpinzani huyo amekosea.

Kuelewa kwa nini wafanyabiashara kotekote walifuata zoea la Lidia la kutumia jiwe la kuthibitishia na pia kuelewa taarifa za mfano zinazotokana na zoea hilo kunatusaidia kuelewa kile kitakachompata Shetani. Hukumu yake itakuwa kiwango cha milele cha kuhukumu ambacho kitaondolea mbali uhitaji wowote wa Mungu kuvumilia tena uasi.—Waroma 8:20.

[Blabu katika ukurasa wa 23]

Kuteswa kwa njia ya mfano kwa Shetani kunadokeza kwamba hukumu yake itakuwa kiwango cha milele

[Ramani katika ukurasa wa 21]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Bahari Nyeusi

LIDIA

SARDI

Bahari ya Mediterania

[Picha katika ukurasa wa 21]

Magofu ya Sardi la kale

[Picha katika ukurasa wa 22]

Hapo zamani, mizani ilitumiwa kupima pesa

[Hisani]

E. Strouhal/Werner Forman/Art Resource, NY

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Kiwango cha kale cha kuthibitishia mambo kinaendelea kutumika hata leo

[Hisani]

Coins: Courtesy Classical Numismatic Group, Inc.; touchstone: Science Museum/Science & Society Picture Library

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 21]

Electrum coin: Courtesy Classical Numismatic Group, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki