Nashukuru Licha ya Misiba—Jinsi Biblia Ilivyonisaidia Kuvumilia
Limesimuliwa na Enrique Caravaca Acosta
Ilikuwa Aprili 15, 1971 (15/4/1971), nami nilikuwa njiani kwenda kuitembelea familia yetu katika shamba letu. Kwa kuwa nilikuwa nimekaa kwa muda bila kwenda nyumbani, nilitamani sana kumwona kila mtu. Sikujua kama wote watakuwa nyumbani na ni nani ambaye ningemwona kwanza. Nilipofika, nilishtuka sana kukuta watu wanne, kutia ndani mama yangu, wakiwa wameuawa!
NILISHTUKA nikashindwa la kusema. Ni nini kilikuwa kimetukia? Ningefanya nini? Hakukuwa na mtu karibu, na nilihisi nimechanganyikiwa nisijue la kufanya. Kabla ya kuendelea na simulizi langu, ningependa kukueleza machache kuhusu maisha yangu. Na hivyo utaelewa vizuri jinsi nilivyohisi kuhusu msiba huo na misiba mingine katika maisha yangu.
Twaipata Kweli
Nilizaliwa Quirimán, karibu na mji wa Nicoya, Kosta Rika. Mwaka wa 1953, nilipokuwa na umri wa miaka 37, niliishi na wazazi wangu shambani mwetu. Ingawa tulilelewa na wazazi Wakatoliki, hatukupendezwa na mafundisho fulani ya Wakatoliki na tulikuwa na maswali mengi.
Asubuhi moja, mwanamume aliyeitwa Anatolio Alfaro alikuja nyumbani kwetu na akatutia moyo tujifunze Biblia. Alizungumza nasi kuhusu maandiko na mafundisho mengi ya Biblia. Mimi, Baba, Mama, ndugu yangu mmoja, dada yangu na rafiki yake aliyekuwa anaishi nasi, tuliketi na kumsikiliza. Tulizungumza kuanzia asubuhi hadi usiku wa manane. Tuliuliza maswali mengi.
Anatolio alilala kwetu na kukaa nasi siku iliyofuata. Tulifurahia mazungumzo hayo sana na tulisisimka hata zaidi alipojibu maswali yetu moja kwa moja kutoka katika Biblia. Mazungumzo hayo yalituchochea sana. Tulifikiria mambo tuliyokuwa tumejifunza, na tukajua kwamba tulikuwa tumeipata kweli. Anatolio alituachia magazeti na vitabu kadhaa. Jioni, tulikuwa tukivisoma na kujifunza pamoja kama familia. Hilo lilikuwa jambo gumu kwa kuwa hatukuwa na umeme. Kabla ya kuketi ili kuanza funzo, kila mmoja wetu alichukua gunia kubwa la kuwekea viazi na kujifunika miguu ili kujikinga na mbu.
Miezi sita baadaye, mimi, wazazi wangu, na watu wengine wawili wa familia yetu, tulibatizwa. Kwa furaha tulianza kwenda nyumba kwa nyumba kuwahubiria watu mambo tuliyokuwa tumejifunza. Tulisafiri muda wa saa mbili kwa miguu na nyakati nyingine kwa farasi kwenda mjini Carrillo ili kukutana na kikundi cha Mashahidi wa Yehova huko. Anatolio aliendelea kututembelea nyumbani ili kujifunza Biblia pamoja nasi. Kisha ikapangwa mikutano iwe ikifanyiwa nyumbani kwetu, na watu wanane hivi wakawa wakihudhuria. Hatimaye wote walibatizwa. Punde si punde, wahudhuriaji hao waliongezeka na kuwa kutaniko dogo la watu 20 hivi.
Naanza Utumishi wa Wakati Wote
Baada ya muda, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Kosta Rika, ilitoa mwaliko kwa wale ambao wangeweza kuanza kazi ya wakati wote ya kuhubiri. Mwaka wa 1957, nilikubali mwaliko huo na kuanza utumishi wa wakati wote. Nilifurahia sana utumishi huo. Mara nyingi nilitembea peke yangu kwa muda wa saa nyingi ili kuwafikia watu vijijini. Nyakati nyingine watu hawakunikaribisha. Ninakumbuka angalau mara tatu nilipotishwa na wanaume wenye mapanga, wakitaka kujua mimi ni nani na ninafanya nini.
Katika miaka ya 1950, barabara nyingi zilikuwa tu vijia vilivyopita nyikani, na haikuwa rahisi kwetu kuwafikia watu. Ilitubidi kutumia farasi ili kufika katika maeneo fulani. Tulivuka mito na mara kwa mara tulilala nje. Mbu walikuwa wengi mno na walitusumbua sana. Ilitubidi pia kuwa waangalifu kwa sababu ya nyoka na mamba. Licha ya hayo yote, nilifurahia sana kuwasaidia watu kumjua Yehova Mungu. Nilipofika nyumbani, nilifurahi na kuridhika sana kwa sababu niliweza kuwahubiria wengine kweli za Biblia. Nilipohubiri na kujifunza Biblia kila siku, upendo wangu kwa Yehova uliendelea kuongezeka na uhusiano wangu pamoja naye ukawa mzuri zaidi.
Baada ya muda fulani kupita, nilipewa migawo zaidi. Kwa miaka zaidi ya kumi, nilikuwa mwangalizi wa mzunguko na nilitembelea makutaniko na kuyatia nguvu. Nilikuwa nikitembelea kutaniko moja kila wiki katika maeneo mbalimbali. Ingawa matatizo ya afya yalinifanya niache pendeleo hilo la utumishi, bado ninaendelea kufurahia utumishi, kwa kumtumikia Mungu wakati wote.
Napatwa na Msiba
Mwaka wa 1971, nilipokuwa mjini Nicoya, nilirudi nyumbani kuitembelea familia yetu. Nilipoingia nyumbani, nilimkuta mama yangu mwenye umri wa miaka 80 ameanguka sakafuni. Alikuwa amepigwa risasi na kudungwa kwa kisu. Nilipoinama kumshika, alikuwa bado anapumua. Alikufa muda mfupi baadaye mikononi mwangu. Nilipotazama huku na huku, nilimwona mpishi, aliyekuwa na mimba ya miezi minane, ameanguka jikoni. Yeye pia alikuwa amekufa. Isitoshe, nilimpata dada mmoja wa kutaniko ameanguka ushorobani akiwa amekufa, na mwana wa yule mpishi akiwa amefia bafuni. Wote walikuwa wamedungwa kisu na kupigwa risasi. Ni nani aliyefanya jambo hilo lenye kuchukiza na kwa nini?
Nilipotoka nje, nilimwona baba yangu. Alikuwa amepigwa risasi kichwani lakini bado alikuwa hai! Nilikimbia nyumbani kwa ndugu yangu, umbali wa dakika 15 hivi, ambako nilipata habari kwamba mwanamke mwingine na mwana wake walikuwa pia wameuawa. Nilishtuka sana kujua kwamba muuaji ni mwana wa dada yangu. Kijana huyo mwenye umri wa miaka 17 hakuwa na akili timamu na hakuwa Shahidi. Alikuwa ametoroka eneo hilo na juhudi za kumtafuta ndizo zilizokuwa kubwa zaidi kuwahi kuonekana nchini Kosta Rika.
Kisa hicho kilikuwa habari kuu nchini. Baada ya siku saba, polisi walimpata muuaji huyo akiwa na kisu kikubwa na bastola ambayo aliuziwa na mtu fulani ijapokuwa alijua kijana huyo hana akili timamu. Polisi walimpiga risasi na kumuua walipokuwa wakimkamata.
Wakati kijana huyo alipokuwa akitafutwa, wengi walinitia moyo nikimbie kutoka eneo hilo wakiogopa kwamba anaweza kurudi na kunidhuru. Nilisali kuhusu jambo hilo kwa sababu nilihisi kwamba nilihitaji kuwa pamoja na watu wa kutaniko na pia watu wa familia waliobaki. Kwa hiyo sikuondoka.
Napatwa na Msiba Mmoja Baada ya Mwingine
Kwa kusikitisha, Baba alikufa baada ya mwaka mmoja tu. Mwaka uliofuata dada yangu, mtumishi mwaminifu wa Yehova Mungu, akauawa katika kisa tofauti. Kwa mara nyingine, watu wa jamaa yetu walishtuka kumpoteza mtu mwingine katika familia. Ni vigumu kuelezea huzuni ambayo sisi na marafiki wetu tulikuwa nayo na jinsi tulivyohisi kuwapoteza watu hao wote. Wakati wa misiba hiyo yote, nilimtegemea Yehova sana na kumwomba bila kukoma anitie nguvu.
Mwaka wa 1985, nilihudhuria darasa la siku tatu la kuwazoeza wazee Wakristo jijini San José. Baada ya masomo hayo, nilihisi nimepata nguvu kiroho. Jumatatu asubuhi na mapema niliondoka kwenda kupanda basi la kurudi nyumbani. Nilipokuwa nikitembea kuelekea kituo cha basi, nilishambuliwa na majambazi walionikaba koo na kuniibia. Walifanya hivyo haraka sana hivi kwamba sikuweza kuona nyuso zao. Baada ya kukabwa koo, nisingeweza kuzungumza jinsi watu wa Kosta Rika wanavyozungumza. Hapa katika wilaya ya Guanacaste, wanaume hupiga mayowe au kupaaza sauti wanapokutana na kusalimiana, au wanapotaka watu wajue wapo mahali fulani. Kabla ya kisa hicho, nilipaaza sauti vizuri sana, lakini sasa siwezi.
Mwaka wa 1979, nilimwoa Celia, Shahidi mwenzangu kutoka kutaniko jirani. Celia aliipenda Biblia. Tulisoma na kujifunza Biblia pamoja kila siku. Inasikitisha kwamba alikufa kwa kansa mnamo Julai (Mwezi wa 7) 2001. Nyakati nyingine ninajisikia mpweke, lakini tumaini la ufufuo hunitia nguvu.—Yohana 5:28, 29.
Nina Furaha Licha ya Majaribu
Ingawa huenda nimepatwa na misiba mingi maishani kuliko watu wengi, ninaona majaribu hayo kuwa nafasi za kuthibitisha imani na uaminifu wangu kwa Yehova. (Yakobo 1:13) Ili niweze kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu mambo ambayo yamenipata, ninajikumbusha daima kwamba sote tunapatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11) Pia, ninakumbuka kwamba hizi ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” kwa kuwa watu ni wakali, wenye jeuri, na wasiojizuia. (2 Timotheo 3:1-5) Ninakumbuka vilevile mfano wa Ayubu. Licha ya mateso yake yote—kupoteza familia, afya, na riziki—Ayubu alisema hivi kwa uthabiti: “Jina la Yehova na liendelee kubarikiwa.” Yehova alimbariki Ayubu sana kwa sababu ya utimilifu wake. (Ayubu 1:13-22; 42:12-15) Maandiko hayo ya Biblia yananisaidia kuendelea kuwa mwenye shangwe licha ya majaribu mengi.
Nyakati zote Yehova amenisaidia kuendelea kumtanguliza katika maisha yangu. Ninafarijika sana ninaposoma Biblia kila siku na imenitia nguvu za kuvumilia. Ninaposali kwa Yehova, ninafurahia “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” (Wafilipi 4:6, 7) Jambo hilo hunipa amani ya akili. Pia, kuhudhuria na kushiriki katika mikutano ya Kikristo kunaimarisha imani yangu.—Waebrania 10:24, 25.
Ingawa sasa mimi ni mzee, ninamshukuru Yehova kwa kuwa bado nina nguvu za kufanya kazi pamoja na Wakristo wenzangu, kujifunza Biblia pamoja na wengine, na kuhubiri. Kuwatumikia wengine katika njia hizo hunitia nguvu kuvumilia hali ya kuvunjika moyo. Ninamshukuru Yehova sana kutoka moyoni licha ya misiba mingi ambayo imenipata maishani.a
[Maelezo ya chini]
a Miaka miwili baada ya kuandika simulizi hili, Enrique Caravaca Acosta alikufa akiwa na umri wa miaka 90.
[Blabu katika ukurasa wa 20]
Ninafarijika sana ninaposoma Biblia kila siku na imenitia nguvu za kuvumilia
[Picha katika ukurasa wa 19]
Nikitoa mojawapo ya hotuba zangu za kwanza-kwanza
[Picha katika ukurasa wa 20]
Nikihubiri katika miaka yangu ya makamo