Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wp17 Na. 6 kur. 12-14
  • Biblia​—Kwa Nini Ziko Nyingi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Biblia​—Kwa Nini Ziko Nyingi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • BIBLIA YA AWALI KABISA
  • SEPTUAJINTI YA KIGIRIKI
  • VULGATE YA KILATINI
  • TAFSIRI MPYA ZAONGOZEKA
  • Jina la Mungu na “Agano Jipya”
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Tafsiri ya “Septuagint” Ilifaa Zamani na Inafaa Sasa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Jinsi Biblia Ilivyotufikia—Sehemu ya Kwanza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Je, Unahitaji Kujifunza Kiebrania na Kigiriki?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
wp17 Na. 6 kur. 12-14
Nakala mbalimbali za Biblia pamoja na za kielektroni

Biblia​—Kwa Nini Ziko Nyingi?

Kwa nini leo kuna matoleo au tafsiri nyingi tofauti-tofauti za Biblia? Je, unaona tafsiri hizo kuwa msaada ama kizuizi cha kuielewa Biblia? Kujifunza historia ya tafsiri za Biblia kutakusaidia uwe na maoni yanayofaa kuzihusu.

Hata hivyo, ni nani walioandika Biblia, na waliiandika lini?

BIBLIA YA AWALI KABISA

Kwa kawaida, Biblia imegawanyika katika sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ina vitabu 39 vyenye “maneno matakatifu ya Mungu.” (Waroma 3:2) Mungu aliwaongoza wanaume waaminifu kuandika vitabu hivyo kwa kipindi kirefu cha miaka 1,100 hivi, kuanzia mwaka wa 1513 K.W.K. hadi wakati fulani baada ya mwaka wa 443 K.W.K. Wengi wao waliandika kwa lugha ya Kiebrania, ndio sababu vitabu hivyo huitwa Maandiko ya Kiebrania, na pia vinajulikana kuwa Agano la Kale.

Sehemu ya pili ina vitabu 27 ambavyo pia ni “neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Mungu aliwaongoza wanafunzi waaminifu wa Yesu Kristo kuandika vitabu hivyo kwa kipindi kifupi zaidi cha karibu miaka 60, kuanzia mwaka wa 41 W.K. hivi hadi 98 W.K. Wengi wao waliandika kwa lugha ya Kigiriki, ndio sababu vitabu hivyo huitwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na pia vinajulikana kuwa Agano Jipya.

Kwa pamoja vitabu hivyo 66 vilivyoongozwa na roho ya Mungu vinafanyiza Biblia—ujumbe wa Mungu kwa wanadamu. Lakini kwa nini tafsiri nyingine za Biblia zilitokezwa? Angalau kuna sababu tatu za msingi.

  • Ili kuwawezesha watu wasome Biblia katika lugha zao.

  • Ili kuondoa makosa yaliyofanywa na wanakili na hivyo kurudisha maneno ya awali ya Biblia.

  • Ili kuboresha lugha iliyotumika.

Acheni tufikirie jinsi sababu hizo zilivyohusika katika tafsiri mbili za awali.

SEPTUAJINTI YA KIGIRIKI

Karibu miaka 300 kabla ya siku za Yesu, wasomi Wayahudi walianza kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika lugha ya Kigiriki. Tafsiri hiyo ilikuja kujulikana kama Septuajinti ya Kigiriki. Kwa nini ilitokezwa? Ili kuwasaidia Wayahudi wengi ambao wakati huo walizungumza Kigiriki badala ya Kiebrania waelewe “maandishi matakatifu.”—2 Timotheo 3:15.

Septuajinti pia iliwasaidia mamilioni ya watu ambao hawakuwa Wayahudi, lakini walizungumza Kigiriki, wajifunze mafundisho ya Biblia. Jinsi gani? Profesa W. F. Howard anasema hivi: “Katikati ya karne ya kwanza, [Septuajinti] ilikuwa Biblia kwa ajili ya Kanisa la Kikristo, ambalo wamishonari wake walitembelea sinagogi moja baada ya jingine ‘wakithibitisha kwa kutumia maandiko kwamba Yesu alikuwa ndiye Masihi.’” (Matendo 17:3, 4; 20:20) Kulingana na msomi wa Biblia F. F. Bruce, hiyo ni moja ya sababu zilizofanya Wayahudi wengi “waache kupendezwa na Septuajinti.”

Wanafunzi wa Yesu walipoendelea kupata vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, waliviunganisha pamoja na toleo la Septuajinti la Maandiko ya Kiebrania, na hivyo kufanyiza Biblia nzima tuliyo nayo leo.

VULGATE YA KILATINI

Miaka 300 hivi baada ya Biblia kukamilika, msomi wa kidini, Jerome, alitoa tafsiri ya Kilatini ya Biblia, ambayo baadaye iliitwa Vulgate ya Kilatini. Kwa kuwa tafsiri mbalimbali za Kilatini tayari zilikuwepo, kwa nini tafsiri mpya ilihitajika? Kitabu The International Standard Bible Encyclopedia kinasema kwamba Jerome alitaka kurekebisha “habari ambazo hazikutafsiriwa kwa usahihi, makosa ya waziwazi, na maneno yaliyoongezwa au kuondolewa kimakosa.”

Jerome alirekebisha makosa mengi kati ya hayo. Lakini baada ya muda, viongozi wa kanisa walifanya uamuzi ambao ungekuwa na madhara zaidi! Waliitangaza Vulgate ya Kilatini kuwa tafsiri pekee ya Biblia inayokubaliwa na wakadumisha msimamo huo kwa karne nyingi! Hatua kwa hatua lugha ya Kilatini ilififia na watu wengi hawakuielewa. Hivyo, badala ya kuwasaidia watu wa kawaida kuielewa Biblia, Vulgate iliifanya kuwa kitabu kisichoeleweka.

TAFSIRI MPYA ZAONGOZEKA

Wakati huohuo, watu waliendelea kutokeza tafsiri nyingine za Biblia, kama vile tafsiri maarufu sana inayoitwa Peshitta ya Kisiria, iliyotolewa karibu karne ya tano W.K. Lakini, tangu wakati huo, hakukuwa na jitihada zozote za kuhakikisha watu wengi wa kawaida wanapata Biblia katika lugha zao, hadi kufikia karne ya 14.

Nchini Uingereza, mwishoni mwa karne ya 14, John Wycliffe alianza kazi ya kuwatoa watu kwenye utumwa wa lugha isiyoeleweka, kwa kutokeza Biblia katika Kiingereza, lugha ambayo watu wengi katika eneo lake waliielewa. Muda mfupi baadaye, mbinu ya uchapishaji iliyovumbuliwa na Johannes Gutenberg, iliongeza kasi ya wasomi wengi wa Biblia kuchapisha na kugawanya matoleo mapya ya Biblia katika lugha mbalimbali zilizozungumzwa barani Ulaya.

Tafsiri mpya za Kiingereza zilipoongezeka, baadhi ya watu walidai hakuna haja ya kuwa na matoleo mbalimbali ya lugha ileile. Kasisi Mwingereza aliyeishi karne ya 18, John Lewis, aliandika: “Lugha huzeeka na kuacha kutumika, hivyo kuna uhitaji wa kupitia upya Tafsiri za zamani na kuziboresha ili ziwe na Lugha ambayo inatumiwa, na kufanya zieleweke kwa watu wa kizazi kilichopo.”

Leo, wasomi wa Biblia wana fursa nzuri zaidi ya kupitia upya tafsiri za zamani. Wanaelewa vizuri zaidi lugha za kale zilizotumiwa kuandika Biblia, na wana hati muhimu sana za kale ambazo zimepatikana hivi karibuni. Hati hizo huwasaidia kutambua kwa usahihi zaidi maneno ya awali ya Biblia.

Hivyo, kuna faida kubwa ya kuwa na matoleo mapya ya Biblia. Ni kweli kwamba, kuna baadhi ya tafsiri za Biblia ambazo si nzuri.a Lakini ikiwa wale wanaotoa toleo jipya la Biblia wamechochewa na upendo wa kweli kwa Mungu, toleo lao linaweza kutusaidia sana.

Ili usome Biblia kwa lugha yako katika mtandao au kupitia kifaa chako cha mkononi, tembelea www.jw.org/sw. Tafuta kwenye MACHAPISHO > BIBLIA.

a Soma makala “Jinsi ya Kuchagua Tafsiri Nzuri ya Biblia” katika toleo la Mei 1, 2008, la gazeti hili.

JINA TAKATIFU LA MUNGU KATIKA BIBLIA

Jina la Mungu kwenye kipande cha hati ya Septuajinti iliyotumika katika siku za Yesu

Jina la Mungu kwenye kipande cha hati ya Septuajinti iliyotumika katika siku za Yesu

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia jina takatifu la Mungu, Yehova, katika Maandiko ya Kiebrania na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Tafsiri nyingi za sasa za Kiswahili hazitumii jina hilo. Badala yake zinatumia jina “Bwana.” Sababu moja ya kufanya hivyo, iliyotolewa na baadhi ya watafsiri ni kuwa, jina la kibinafsi la Mungu, linalowakilishwa na Tetragramatoni (YHWH), halipatikani kwenye tafsiri ya Septuajinti ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania. Lakini je, hilo ni kweli?

Katikati ya karne ya 20, baadhi ya vipande vikuukuu vya hati ya Septuajinti iliyotumika katika siku za Yesu vilipatikana. Vilikuwa na jina takatifu la Mungu likiwa limeandikwa kwa herufi za Kiebrania. Inaonekana kwamba, baadaye wanakili waliliondoa jina la Mungu na badala yake kutumia neno la Kigiriki Kyʹri·os, linalomaanisha “Bwana.” Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imerudisha jina la Mungu mahali lilipokuwa katika Maandiko.

JE, BIBLIA IMEPOTOSHWA?

Hatikunjo ya Bahari ya Chumvi ya kitabu cha Isaya

Hatikunjo ya Bahari ya Chumvi ya kitabu cha Isaya iliyoandikwa miaka 2,000 iliyopita. Inakaribiana sana na Biblia tunayotumia leo

Ni kweli kwamba nyakati fulani wanakili wa Biblia walikosea. Lakini makosa yao hayakuupotosha ujumbe wa Biblia. “Hakuna fundisho lolote la msingi la imani ya Kikristo linalotegemea sehemu inayotiliwa shaka.”—Our Bible and the Ancient Manuscripts.

Wanakili Wayahudi walifanya makosa machache zaidi. “Waandishi Wayahudi wa karne za mwanzoni za Ukristo walinakili tena na tena maandishi ya Biblia ya Kiebrania kwa umakini wa hali ya juu.”—Second Thoughts on the Dead Sea Scrolls.

Kwa mfano, hatikunjo ya Isaya iliyopatikana katika Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi, ilitokezwa miaka 1,000 mapema ukilinganisha na hati ambazo zilikuwa zikitumika. Inatofautiana kiasi gani na hati tulizo nazo? “Ni nadra sana kukuta neno limeongezwa au kuondolewa.”—The Book. A History of the Bible.

Makosa yaliyofanywa na wanakili ambao hawakuwa makini, kama vile kuhamisha herufi, maneno, au vifungu vya maneno, sasa ni rahisi kuyatambua na kuyarekebisha. “Hakuna mkusanyo wa chapisho lingine lolote la kale duniani ambalo lina utajiri mkubwa wa ushahidi wa kimaandishi kuliko Agano Jipya.”—The Books and the Parchments.

“Wanadini wenye shaka wanaweza kuwa na uhakika kwa sababu ya ulinganifu mkubwa uliopo kati ya mafunjo ya awali kabisa ya Misri na maandishi [ya Biblia tuliyo nayo leo] licha ya kunakiliwa mara nyingi sana na kupitia kwenye viwanda vingi vya uchapishaji barani Ulaya.”—The Book. A History of the Bible.

Basi je, Biblia imepotoshwa? Jibu ni hapana!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki