Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • wp18 Na. 3 kur. 8-9
  • Je, Mungu Huhisi Maumivu Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Mungu Huhisi Maumivu Yako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2018
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UUMBAJI UNATUFUNDISHA NINI?
  • BIBLIA INAONYESHAJE KWAMBA MUNGU ANA UWEZO WA KUHISI MAUMIVU YETU?
  • MUNGU HUONA, HUELEWA, NA KUHISI MAUMIVU YETU
  • Hisia-Mwenzi—Hutusaidia Kudhihirisha Fadhili na Huruma
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Onyesha Hisia-Mwenzi
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2021
  • Uwe na Huruma
    Amkeni!—2020
  • Anaelewa Maumivu Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2018
wp18 Na. 3 kur. 8-9
Msichana akimfariji mwenzake ambaye amepata jeraha kwenye goti; dada mmoja akimfariji mwenzake ambaye analia

Je, Mungu Huhisi Maumivu Yako?

UUMBAJI UNATUFUNDISHA NINI?

Mtu anaweza kuhisi maumivu ya mwingine kwa kuwazia hali au hisia za mtu huyo, na kujiona kama yeye ndiye anayepitia hali hizo. Dakt. Rick Hanson, mtaalamu wa afya ya akili, anasema kwamba “tunazaliwa tukiwa na uwezo wa kuhisi maumivu ya wengine.”

FIKIRIA HILI: Kwa nini tuna uwezo wa kuhisi maumivu ya wengine, sifa ambayo viumbe wengine duniani hawana? Biblia inasema kwamba Mungu aliwaumba wanadamu kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26) Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu katika maana ya kwamba tunaweza kusitawisha sifa zake na kuzionyesha kwa kadiri fulani. Hivyo, mtu anapohisi maumivu ya wengine na kusukumwa kuwasaidia kwa sababu anawajali, anakuwa akimwiga Muumba wetu mwenye huruma, Yehova Mungu.—Methali 14:31.

BIBLIA INAONYESHAJE KWAMBA MUNGU ANA UWEZO WA KUHISI MAUMIVU YETU?

Mungu huhisi maumivu yetu, na anachukia kuona tukiteseka. Biblia inasema hivi kuhusu taifa la kale la Israeli ambalo lilivumilia mateso makali utumwani nchini Misri, na baadaye kukabili hali ngumu jangwani kwa miaka 40: “Katika taabu zao zote, yeye alitaabika.” (Isaya 63:9) Mstari huo hausemi tu kwamba Mungu aliona taabu zao. Unaonyesha kwamba alihisi maumivu yao. Mungu alisema: “Ninajua vema maumivu yao.” (Kutoka 3:7) Mungu pia anasema: “Yeyote anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.” (Zekaria 2:8) Wengine wanapotuumiza, yeye pia huumia moyoni.

Biblia inatuhakikishia kwamba ingawa huenda tukajihukumu na kuhisi kuwa hatustahili huruma za Mungu, “[Yeye] ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.” (1 Yohana 3:19, 20) Mungu anatujua vizuri zaidi ya tunavyojijua. Anajua kikamili hali zetu, mawazo yetu, na hisia zetu. Yeye huhisi maumivu tunayokabili.

Tunaweza kutarajia kupata faraja, hekima, na msaada wa Mungu, tukiwa na uhakika kwamba yeye huwategemeza wale wanaotaabika

Maandiko yanatuhakikishia kwamba . . .

  • “Utaita, na Yehova atakujibu; utalilia msaada, naye atasema, ‘Mimi hapa!’”​—ISAYA 58:9.

  • “‘Kwa maana ninajua vizuri mawazo ninayofikiria kuwaelekea ninyi,’ asema Yehova, ‘mawazo ya amani, wala si ya msiba, ili niwape ninyi wakati ujao na tumaini. Nanyi mtaniita na kuja na kusali kwangu, nami nitawasikiliza.’”​—YEREMIA 29:11, 12.

  • “Yakusanye machozi yangu katika kiriba chako cha ngozi. Je, hayajaandikwa katika kitabu chako?”​—ZABURI 56:8.

MUNGU HUONA, HUELEWA, NA KUHISI MAUMIVU YETU

Je, kujua kwamba Mungu huhisi maumivu yetu kunaweza kutusaidia kukabiliana na hali ngumu? Fikiria kisa cha Maria:

“Baada ya mwanangu mwenye umri wa miaka 18 kupambana na saratani kwa miaka miwili na mwishowe kufa, nilihisi maumivu makali na kuona kwamba maisha ni magumu na haki haipo. Nilimkasirikia Yehova kwa kutoingilia kati na kumponya!

“Miaka sita baadaye, rafiki yangu kutanikoni, mwenye upendo na huruma, alinisikiliza nilipomweleza hisia zangu kwamba Yehova hanipendi. Baada ya kunisikiliza kwa saa nyingi bila kunikatisha, alinukuu andiko la 1 Yohana 3:19, 20, ambalo lilinigusa moyo sana. Linasema: ‘Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.’ Aliniambia kwamba Yehova anaelewa taabu zetu.

“Licha ya hilo, bado haikuwa rahisi kuondoa hasira niliyokuwa nayo! Kisha nikasoma Zaburi 94:19, inayosema: ‘Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.’ Nilihisi kana kwamba mistari hiyo iliandikwa kwa ajili yangu kabisa! Hatimaye, nilianza kuhisi utulivu ninapozungumza na Yehova kuhusu taabu zangu, nikijua kwamba ananisikiliza na kunielewa.”

Inafariji sana kujua kwamba Mungu anatuelewa na kuhisi maumivu yetu! Hata hivyo, kwa nini basi wanadamu wanateseka sana? Je, Mungu anatuadhibu kwa sababu ya makosa yetu? Je, Mungu atakomesha hali zote ngumu tunazokabili? Makala zinazofuata zitajibu maswali hayo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki