Sanduku la Swali
● Ni nani aliye na idhini ya kufungisha ndoa au ya kuongoza mazishi?
Toleo la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1975 lilieleza kwamba katika makutaniko yetu, ni wazee na watumishi wa huduma pekee wanaostahili kuitwa “wahudumu waliowekwa rasmi” kulingana na jinsi msemo huo unavyotumika na kueleweka kisheria. Ikiwa sheria ya nchi, mji, au eneo inaruhusu ndoa zifungishwe tu na wahudumu (walio na “leseni,” “waliosajiliwa,” au “waliowekwa rasmi”) basi ni ndugu ambao kulingana na Maandiko “wamewekwa rasmi” kutumika kutanikoni, yaani wazee au watumishi wa huduma pekee, kuanzia sasa ndio wanaofaa kufungisha ndoa. (Hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi kuhusu wale waliofungisha ndoa awali.)
Mnapaswa kuchunguza na kufuata sheria za eneo lenu kuhusu suala hili. Tafadhali msiiandikie ofisi ya tawi ili kupata habari hiyo, kwa sababu ofisi ya tawi haifahamu sheria za nchi mbalimbali zinazohusu matakwa ya ndoa.
Ikiwa wenzi katika kutaniko wangependa hotuba ya ndoa itolewe na ndugu ambaye ana mwenendo mzuri lakini si mzee au mtumishi wa huduma, mipango inaweza kufanywa ili ndugu huyo atoe hotuba hiyo, halafu baada ya hotuba, mmoja kati ya wazee au watumishi wa huduma mwenye kibali cha kisheria cha kufungisha ndoa asimamie nadhiri za ndoa. Kwa kawaida, tendo la kusimamia nadhiri za ndoa ndilo linalotambulika kisheria kama kufungisha ndoa.
Maombi ya matumizi ya Jumba la Ufalme kwa ajili ya ndoa yanapaswa kuidhinishwa na halmashauri ya utumishi ya kutaniko. (Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Kiingereza ya Juni 1975 “Sanduku la Swali.”)
Suala la kutoa hotuba wakati wa mazishi ni tofauti kabisa na la kufungisha ndoa. Hakuna sheria inayoamua ni nani atoe hotuba kwenye mazishi. Kwa kawaida familia iliyofiwa huchagua ndugu mwenye kielelezo kizuri atoe hotuba ya mazishi. Huo ni uamuzi na mpango wao binafsi. Si lazima waliyemchagua awe “mhudumu aliyewekwa rasmi” au katika maana ya Kimaandiko awe “mtumishi aliyepewa mgawo au aliyewekwa rasmi” kutanikoni.