“Haki ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1988
1 Yehova Mungu anapenda haki na uadilifu. (Zab. 33:5) Mtumishi wake Elihu alitangaza hivi: “Yeye Mwenyezi hatuwezi kumwona; yeye ni mkuu mwenye uweza; tena mwenye hukumu, na mwingi wa haki, hataonea.”—Ayubu 37:23.
2 Hakika, Yehova Mungu hajapuuza ukosefu wa haki ambao umetendwa katika ulimwengu huu. Kwa kuwa yeye ni Mungu wa viwango vya adili visivyobadilika, tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba yeye hatavumilia uvunjaji wa sheria wa leo kwa wakati usio dhahiri. (Linganisha Isaya 14:3-8.) Kwa kweli, unabii wa Biblia unaelekeza kwenye wakati wetu kuwa siku za mwisho za ulimwengu usiomcha Mungu. Kwa hiyo tunahitaji kuonyesha kwa matendo yetu kwamba tunapenda uadilifu na haki ya kimungu na kwamba tunajiweka mbali na mazoea yaliyoshutumiwa ya ulimwengu huu.
3 Mashahidi wa Yehova wanatazamia “Haki ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya ambayo imeratibiwa kwa ajili ya 1988/89. Orodha ya mikusanyiko iliandaliwa katika toleo la Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1988. Kwenye mikusanyiko ya wilaya tunafunzwa na Yehova kweli kweli. Tunahudhuria tukiwa na mwelekeo wa akili unaodhihirishwa katika sala iliyovuviwa kwenye Zaburi 119:33: “Ee BWANA [Yehova, NW], unifundishe njia ya amri zako, nami nitaishika hata mwisho.” Kwa kweli, maneno haya yanaonyesha hisia ya watumishi wote wa Yehova waliojiweka wakfu leo.
4 HUDHURIA VIPINDI VYOTE: “Haki ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya itakuwa ya siku nne. Je! wewe umefanya mipango ili uhudhurie vipindi vyote? Kuanzia kipindi cha kufungua Alhamisi saa 7:30 alasiri mpaka sala ya kumalizia Jumapili karibu saa 10:00 alasiri, habari za maana ambazo ni za muhimu kwa afya yetu ya kiroho zitatolewa. Upande tofauti wa haki ya kimungu utakaziwa kila siku. Programu itatia ndani hotuba, mawonyesho, na drama. Basi, usikose hata kipindi kimoja. Inathaminiwa kwamba huenda hiyo ikahitaji wewe ujidhabihu kibinafsi na kufanya marekebisho katika ratiba yako. Huenda ukahitaji kufanya mipango fulani pamoja na mwajiri-kazi wako ili uhudhurie mkusanyiko. Ukifikiria habari hiyo kwa sala ya unyoofu na kujitahidi sana kuwa huko, hakika Yehova atakubariki.—Mt. 5:3.
5 Jitahidi kufika mapema kila siku ili uwe umeketi kabla ya vipindi kuanza. Hilo litakupa fursa ya kufurahia ushirika wa Kikristo pamoja na ndugu na dada kutoka sehemu nyingine. (Rum. 1:12) Itakuruhusu pia ujiunge katika kusifu Yehova pamoja katika wimbo, ambayo ni sehemu ya maana sana ya ibada yetu, na kushiriki katika sala ya kufungua. Fikiria pia kwamba wale wanaoketi kukuzunguka hakika watathamini kwamba hukuondosha fikira zao kwenye programu kwa kufika ukiwa umechelewa. Upendo na fikira za Kikristo, pamoja na heshima kwa Yehova na mambo ya kiroho ambayo yeye anaandaa, vyapaswa vitusukume kufanya yoteyote tuwezayo ili tufike kwa wakati.
6 Tayari umepewa habari kuhusu mkusanyiko ambao kundi lako limegawiwa kuhudhuria. Habari zinazohusu mahali pa kulala na mipango mingine ya mkusanyiko wako itaandaliwa na Halmashauri ya Mkusanyiko. Mipango na kazi nyingi imefanywa ili kuhakikisha kwamba mahali pa kuketi panapotosha, fasihi, chakula na maandalizi mengine yanapatikana kwa kila mtu.
7 ELEKEZA FIKIRA KWA YALE UNAYOSIKIA: “Maneno ya BWANA [Yehova, NW] ni maneno safi, ni fedha iliyojaribiwa kalibuni juu ya nchi; iliyosafishwa mara saba.” (Zab. 12:6) Mengi ya ‘maneno safi’ ya Mungu yatasikiwa kwenye “Haki ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya. Habari itakayotolewa haitakuwa ujumbe wa kawaida kwa msikilizaji mwenye udadisi bali itakuwa habari ya pekee kwa watu wa Yehova, kwa wale ambao wamejitoa wakfu kwake, wanaotaka kumpendeza, ‘wanaotetemeka kwa ajili ya neno lake.’ (Isa. 66:5) Kati ya watu wote duniani, sisi tumependelewa sana sana kufundishwa na Yehova.—Isa. 54:13.
8 Kusikiliza kunamaanisha kuelekeza fikira kweli kweli kwa akili na moyo wetu pia, kwa masikio yetu na nguvu zetu za kufikiri. Tunahitaji kusikiliza ‘neno la Yehova.’ (Yer. 2:4) Tunayosikia yatatia ndani maarifa sahihi ya kupanua ufahamu wetu na kuongeza kina cha uthamini wetu. Tutasikia habari ya kujenga imani yetu na kutia tumaini letu nguvu. Tutapokea shauri na nidhamu ambayo imeandaliwa kwa upendo kwa manufaa yetu. Wakati mwingi sana umetumiwa kufanya uchunguzi na kutayarisha programu. Basi, ni jambo la muhimu kwamba tusikilize na kuwa macho kwa yale ambayo Neno la Yehova linatuambia. Hivyo tunaweza kunufaika kibinafsi na kuwa na uwezo wa kutumia habari hii kuwasaidia wengine.—Mit. 18:15.
9 Kwa kuwa kusudi letu la msingi la kuhudhuria mkusanyiko ni kupokea mwongozo wa kiroho na kitia-moyo, panga ili ufike mapema vya kutosha ili ushughulikie mambo yanayohitaji kuelekezewa fikira, kama vile kupata tikiti za chakula za mkusanyiko, kisha uwe umeketi kabla ya programu kuanza. Kufanya hivyo kutakuwezesha ustarehe, akili zako zikiwa hazisumbuliwi na mahangaiko kuhusu mambo mengine yasiyohusiana moja kwa moja na programu.
10 Hakikisha kwamba unalala usingizi vizuri kila usiku ili kwamba uwe umeburudika asubuhi na uweze kukaza fikira kikamili juu ya programu wakati wa mchana. Ijapokuwa mkusanyiko unatoa fursa nzuri ya kufanya upya urafiki na kufurahia ushirika mzuri, tukiwatembelea marafiki mpaka usiku sana, huenda tusiwe macho kunufaika na programu kikamili siku inayofuata.
11 UBATIZO: Hotuba ya watakaobatizwa itatolewa Jumamosi asubuhi. Ubatizo ni wonyesho wa nje wa kwamba mmoja amejitoa mwenyewe wakfu kwa Yehova Mungu bila kuweka masharti. Sehemu hii ya programu ni mojapo mambo makuu ya mkusanyiko wa wilaya. Sisi sote tunanufaika kwa kusikiliza kwa umakini na kufikiria uhusiano wetu wenyewe pamoja na Yehova. Kwa kuongezea, tunashiriki shangwe ya wale wanaobatizwa.
12 Wale wanaopanga kubatizwa kwenye mmojapo mikusanyiko ya wilaya wanapaswa wahakikishe kwamba wanajulisha mwangalizi msimamizi mapema kabla ya mkusanyiko ili kuwa na wakati wa kutosha kufanya pitio la maswali katika kitabu Huduma Yetu. Kila mmoja anayepanga kubatizwa anapaswa kuleta vazi lenye kiasi na taulo. Tunawashauri akina dada wachunguze kimbele waone kama mavazi wanayopanga kuvaa yanaonyesha uchi yanapolowa maji, jambo ambalo halingekuwa lenye kiasi. Kanga huonekana kuwa zenye kufaa zaidi kuliko sikati au nguo pana ambazo huelekea kuinuka katika maji.—Ona Huduma ya Ufalme Yetu, Novemba 1987, ukurasa 3, fungu 6.
13 Wenye kubatizwa wapaswa kujaribu kuwa kwenye viti vyao katika sehemu iliyoonyeshwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Baada ya hotuba ya ubatizo na sala itakayotolewa na msemaji, mwenyekiti wa kipindi hicho atawatolea wanaobatizwa maagizo mafupi kisha ataomba wimbo uimbwe. Wote watasimama wakati wimbo unapoimbwa. Kabla ya kuimbwa kwa mstari wa mwisho, wakaribishaji watawaelekeza wenye kubatizwa kwenye mahali pa uzamisho au kwenye magari yatakayowapeleka hapo, huku wahudhuriaji wengine wakimaliza kuimba wimbo.
14 KUANDIKA MAMBO: Licha ya Biblia na wimbo wako, kumbuka kuleta kijitabu cha kuandika na kalamu. Huenda sisi tusiwe na zoea la kuandika mambo wakati wa mikutano ya kundi ya kila wiki kwa sababu hotuba zilizo nyingi na mawonyesho huchukuliwa kutokana na vifaa vinavyopatikana kwa wote katika kundi. Hata hivyo, kusikiliza habari katika mikusanyiko ya wilaya ni jambo tofauti kabisa. Ingawa baadhi ya hotuba zitatokea baada ya muda katika vichapo, nyingine hazitatokea. Hata kama hotuba zote zingetokea hatimaye katika vichapo, bado kuna manufaa nyingi zenye maana ikiwa wewe ungeandika mambo mafupi yenye maana.
15 Jambo moja ni kwamba, kuandika mambo makuu kunatumika kuwa msaada wa kukaza fikira. Tenga mambo makuu na maandiko makuu ya msemaji au wazo jipya ambalo huenda likatolewa. Kisha andika mambo mafupi juu ya hayo. Kwa kawaida sentensi moja au mbili zitatosha kwa jambo kuu. Kwa kufuata dokezo hili, kukaza fikira kwako bila shaka kutaendelezwa. Hutakuwa na elekeo zaidi la kuacha akili zako zitangetange au zikengeushwe. Pia wewe utatayarishwa kushiriki katika pitio la mambo makuu ya mkusanyiko pamoja na kundi lenu juma litakalofuata.
16 Je! wewe utakuwa na watoto wachanga au matineja pamoja nawe? Basi, kwa sababu gani msiwapangie pia waandike mambo makuu kulingana na uwezo na umri wao? Acha jamaa ijue kwamba wewe unapanga kufanya pitio la baadhi ya mambo makuu yaliyozungumziwa na wasemaji mrudipo mahali mnapolala au mnaposafiri kurudi nyumbani. Watoto wachanga zaidi wanaweza kutiwa moyo waandike maandiko yote yanayosomwa na kuona ni mara ngapi wao wanamsikia msemaji akitaja yale maneno makuu au kichwa cha hotuba yake. Kwa kufanya hivi, watapata mengi zaidi kutokana na hotuba zile. Ni vizuri watoto wajifunze kusikiliza kwa makini kwenye mikutano ya Kikristo. Utakuwa ukiwasaidia wao wajenge msingi imara kwa wakati ujao.—Kum. 31:12; Efe. 6:4.
17 MWENENDO MZURI: Kila mwaka kwenye umalizio wa mikusanyiko ya wilaya yetu, kwa kawaida sisi hupokea maelezo mazuri kwa habari ya utaratibu na mwenendo mzuri ulioonekana wazi. Mara nyingi watazamaji wanataja juu ya sura nadhifu ya watu wazima na watoto pia, licha ya amani na umoja wa akina ndugu wanapohudhuria mkusanyiko. Mwaka 1987 haukuwa tofauti. Lakini ni kwa sababu gani tunataja hili? Ni kwa sababu inatia moyo kujua kwamba wakati tunapoweka kielelezo kizuri, kinaonwa na kuthaminiwa na wengine. (1 Pet. 2:12) Jambo la maana zaidi, hata hivyo, kinamletea Mungu sifa. Sisi tunataka kumheshimu Yehova katika neno na tendo, na kwa kuwa watu huenda wakahukumu tengenezo na hata yule Mungu tunayemwabudu kwa mwenendo wetu, siku zote sisi tunataka kudhamiria jinsi tunavyotenda.
18 Kuna hesabu ya maeneo ambayo tutahitaji kuelekezea fikira ili ‘tuwe kama mianga’ kikamili, hasa tunapokuwa nje ya nyanja za mkusanyiko, kama vile mahali tunapolala.—Flp. 2:15.
19 Kwanza, tunatenda jinsi gani kwa habari ya kuhifadhi viti isivyohitajiwa? Maendeleo yameonekana kwa habari hii, na kwa sababu hiyo tunawapongeza. Hata hivyo, tungali tunahitaji kuelekeza fikira kwenye jambo hili, kwa kuwa wengine wanatumia vibaya mpango huu. Tafadhali kumbuka kwamba VITI VINAWEZA KUHIFADHIWA KWA WASHIRIKI WA KARIBU WA JAMAA YAKO PEKE YAO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE KATIKA GARI LAKO. Ni jambo la asili tu kutaka kuketi pamoja na wale ambao tumekuja nao, na inatazamiwa kwamba washiriki wa karibu wa jamaa wanaketi pamoja. Lakini tafadhali msiwawekee wengine viti. Mara nyingi marafiki hujitafutia viti vyao wenyewe, na vile vya ziada vilivyowekwa havitumiwi. Tunaweza kuonyesha uthamini kwa mkusanyiko kwa kufuata miongozo hiyo.—Mt. 7:12.
20 Tukiwa watumishi waliojiweka wakfu, mwenendo wetu wapaswa uwe mzuri NYAKATI ZOTE. Mwenendo ulio kielelezo kizuri unaangaliwa sana kwenye mikutaniko mikubwa na jina la Yehova linatukuzwa kwa mwenendo huo. Hata hivyo, mwenendo mbaya na ukosefu wa kuwafikiria wengine kwa upande wa wachache unaweza kuletea jina la Yehova na watu wake suto. Ripoti zimepokewa kwamba akina ndugu wachache na jamaa zao wametumia vibaya vifaa vya mahali wanapolala. Watoto wa Mashahidi fulani hawakusimamiwa vizuri na wamekuwa watundu sana. Roho ya ulimwengu inadhihirishwa miongoni mwa wachache wanaporudi mahali wanapolala. Baadhi yao hawabadili tu mavazi yao na kuvaa mavazi yasiyo na kiasi na yenye mitindo-mitindo, bali wanabadili mwenendo wao pia. Kwenye mkusanyiko, tunaona waziwazi mwenendo wa Mkristo unapaswa kuwaje, lakini wachache, baada ya kuondoka kwenye mkusanyiko, wanaonekana wanasahau yale waliyoona na kusikia katika programu. (Yak. 1:22-24) Kuwapo kwetu kwenye mkusanyiko na mahali penginepo, na pia mwenendo wetu na kujipamba, kunatoa ushuhuda juu yetu na Mungu tunayeabudu.
21 Bila shaka, programu ya mkusanyiko inapomalizika wengi wanafurahia kuwa pamoja kwa ajili ya chakula na ushirika. Hilo linaweza kupendeza na wakati unaweza kutumiwa vizuri katika mazungumzo mazuri tunaposhiriki mambo yaliyoonwa na kufanya pitio la mambo makuu ya mkusanyiko. Inatuletea furaha na utukufu kwa Mungu Yehova tunapojiendesha “kwa namna inayostahili zile habari njema.”—Flp. 1:27, NW.
22 Kikumbusha kimoja cha mwisho chenye fadhili kinahusiana na kutembeleana na kuzungumziana wakati vipindi vinapoendelea. Ni wazi kwamba tunashangilia kuona marafiki kwenye mkusanyiko, lakini staha kwa Yehova na kuwafikiria ndugu zetu kwapasa kuwe jambo kuu akilini. Kwa sababu hiyo, hatungetaka kuwa tukisumbua au kukengeusha fikira za wengine wakati wa programu. Ikiwa inakubidi kuacha kiti chako kwenda kwenye shughuli fulani ya maana, fanya hivyo upesi na kwa utulivu iwezekanavyo. Pia, programu inapoendelea, hakuna mtu anayepaswa kuwa akitembelea wengine kwenye ukumbi. Tuko huko ili tusikilize na kujifunza.—Luka 8:18.
23 MAHITAJI YA CHAKULA: Kama mjuavyo, Sosaiti imerahisisha utumishi wa mpango wa chakula kwenye mikusanyiko ya wilaya. Hilo linawezesha wengi zaidi wa ndugu na dada zetu ambao wanafanya kazi katika kutayarisha chakula wajiunge pamoja nasi wasikilizaji na kunufaika na chakula cha kiroho kinachotolewa. Tunathamini sana hiari ya wale ambao wanajitoa kututumikia kwenye mikusanyiko ya wilaya.
24 Wote wenye kuhudhuria mkusanyiko wataona kwamba chakula kinachopatikana kitakuwa chenye kutosha na chenye kulisha mwili, kikiwa cha unamna-namna mzuri kwa siku nne. Uangalizi mkubwa umefanywa kununua chakula cha hali ya juu zaidi. Kutumia kikamilifu maandalizi yanayopatikana kupitia Idara ya Utumishi wa Chakula kutasaidia kulipia baadhi ya gharama za mkusanyiko.
25 UTUMISHI WA KUJITOLEA: Ule mkazo wa kurahisisha mambo unaonekana hasa kuhusiana na saa nyingi zilizohitajiwa kupangia na kuendesha mkusanyiko wa wilaya. Wale ambao wamekuwa katika ukweli kwa miaka mingi wanakumbuka kwamba wakati uliopita, kabla na wakati wa mikusanyiko mikubwa, makumi ya maelfu ya wenye kujitolea walihitajiwa, wakitumia saa nyingi za wakati wao katika idara mbalimbali za mkusanyiko. Utumishi huo wa upendo ulithaminiwa sana sana, lakini mara nyingi tokeo lilikuwa kwamba wengi wa wenye kujitolea walikosa sehemu kubwa ya programu.
26 Ingawa wenye kujitolea wachache zaidi na saa chache zaidi zinatakwa sasa kufanya ile kazi, msaada wa wenye kujitolea ungali unahitajiwa kwa uendeshaji wa utaratibu wa mkusanyiko wa wilaya. Je! wewe unaweza kushiriki? Hakuna mmoja yeyote anayepaswa kuhisi kwamba kujitolea kutamaanisha kukosa sehemu iliyo kubwa ya programu kama ilivyokuwa kwa wengine katika wakati uliopita.
27 Uwasilipo kwenye mahali pa mkusanyiko, onana na Idara ya Utumishi wa Kujitolea. Hata kama utaweza kufanya kazi kwa sehemu tu ya mkusanyiko, utumishi wako utathaminiwa. Watoto wa umri ulio chini ya miaka 16 wanatakwa wafanye kazi pamoja na mzazi au mlezi.
28 KUNASA SAUTI: Linaonekana kuwa jambo la wakati unaofaa kueleza wazi msimamo wa Sosaiti kuhusu matumizi ya kamera za vidio na vilevile vifaa vya kunasia sauti. Mwongozo thabiti unatakwa kwa mikutano yote—mikusanyiko ya wilaya, makusanyiko ya mzunguko, siku za pekee za kusanyiko, na katika Majumba ya Ufalme. Ingawa hakuna katazo la kutumia vifaa hivyo, inaonekana lazima kudhibiti na kuwekea mpaka matumizi yavyo. Wakaribishaji wanapaswa kuwa chonjo kuona kwamba wale wanaotumia kamera za vidio na vyombo vya kunasia sauti hawasumbui wengine na kuwakengeusha fikira kutoka kwenye programu inayoendelea. Akina ndugu wanaotumia vifaa hivyo wanapaswa kushirikiana pamoja na wakaribishaji na wazee wanaosimamia mambo na kutojipendeza wenyewe tu. Vifaa kama hivyo havipaswi kuwekwa kwenye vijia au kwenye miingilio. Vifaa hivyo havipaswi kuunganishwa kwenye mfumo wa kuhutubia watu wote au matundu ya umeme, wala taa zenye mwangaza mwingi haziruhusiwi. Katika visa fulani, vifaa hivyo vinaweza kuwekwa mahali ambapo havitasumbua wasikilizaji, kama vile nyuma ya majumba.
29 UMALIZIO: Kuna sababu nzuri kwa nini tunataka kuwa kwenye “Haki ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya ambapo tunaweza kuabudu Yehova pamoja na maelfu ya akina ndugu. Pia, mikusanyiko ni karamu za kiroho zinazotia nguvu imani yetu na kuongeza kina cha uthamini wetu kwa ukweli. Mnabii Isaya alitangaza kwamba watumishi wa Yehova “hawataona njaa, wala hawataona kiu; hari haitawapiga, wala jua; kwa maana yeye aliyewarehemu atawatangulia, naam, karibu na chemchemi za maji atawaongoza.” (Isa. 49:10) Kwa kweli, watu wa Yehova hawaoni njaa ya kiroho au kiu ya ukweli. Wala hari yenye kuchoma ya hukumu kali za Mungu haiwaangukii. Sisi tunajua jinsi maandalizi ya kiroho yalivyo na ladha nzuri na jinsi yanavyotia nguvu. Hiyo ndiyo sababu sisi tunashangilia kuwa na fursa ya kukusanyika pamoja kwa ajili ya “Haki ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wilaya.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Vikumbusho vya Mkusanyiko wa Wilaya
MAHALI PA KULALA: Mipango kwa mwaka huu, kwa sehemu iliyo kubwa, itafuata kiolezo cha miaka iliyotangulia. Unaweza kupeleka fomu ya maombi ya mahali pa kulala iliyojazwa kupitia msawazishaji wa mkusanyiko katika kundi lenu.
SAA ZA PROGRAMU: Ni mwendo wa hekima na unaoonyesha uthamini kuwa tumeketi programu inapoanza. Katika miji yote ya mikusanyiko programu itaanza na muziki, kisha wimbo na sala Alhamisi saa 7:30 alasiri na vipindi vitamalizika saa 11:10 jioni. Programu ya Ijumaa na Jumamosi itaanza saa 4:20 asubuhi na kumalizika saa 11:40 jioni Ijumaa na 11:55 jioni Jumamosi. Jumapili programu itaanza saa 3:30 asubuhi na kumalizika karibu saa 10:00 alasiri. Hotuba ya watu wote Jumapili itaanza na wimbo na sala saa 8:00 alasiri.
MKUTANO WA BETHELI: Kutakuwa na mkutano Jumamosi kwenye baadhi ya mikusanyiko kwa wahubiri wowote waliojiweka wakfu wenye umri wa miaka kati ya 19 na 35 ambao ni wenyeji wa Kenya na ambao wangependa kuingia utumishi wa Betheli. Matangazo yatafanywa kwenye mji wa mkusanyiko kuhusu wakati na mahali hasa pa mkutano huu.
KITAMBULISHO CHA MAPAINIA: Mapainia wote wa kawaida na wa pekee na waangalizi wasafirio watahitaji kuleta Kitambulisho na kadi yao ya Mgawo [S-202] kwenye mkusanyiko. Wale ambao watakuwa wamefikisha miezi sita tangu waanze upainia wakati wa mkusanyiko wa wilaya watakaouhudhuria wanaweza kupokea tikiti za chakula za mikusanyiko wakionyesha kitambulisho chao kwenye mkusanyiko huu mmoja tu. Tunza kadi hiyo kama pesa. Huwezi kupata nyingine kwenye mkusanyiko. Vichapo vyovyote vitakavyotolewa kama zawadi au vingine kwa bei ya painia vitapatikana kwa mapainia katika chumba cha vitabu tu, kwa kuonyesha kitambulisho chao. Wale walio katika utumishi wa Betheli wanaweza kupokea maandalizi yayo hayo kwa kuonyesha kitambulisho chao cha Betheli.
KADI YA SHAVU LA KOTI: Kadi hizo zinatolewa kama njia ya kutangaza mkusanyiko na pia kusaidia kuwatambua ndugu na dada zetu wanaohudhuria. Ili kutimiza hili, tafadhali vaa kadi yako ya shavu la koti iliyotayarishwa kipekee kwenye mkusanyiko na pia unaposafiri kwenda na kutoka mahali pa mkusanyiko. Si kwamba tu kadi inasaidia kutambulisha bali pia mara nyingi inatokeza kutoa ushuhuda mzuri tunaposafiri. Unapaswa uzipokee kupitia kundi lako kwa sababu hazitapatikana kwenye mkusanyiko. (Kadi za shavu la koti zimekwisha kupelekwa kwenye kila kundi na Sosaiti, lakini vifuko vya plastiki lazima viagizwe na kundi.)
TAHADHARI: Bila kujali mahali unapoweka gari lako, lazima ufunge gari lako wakati wote na usiache ndani kitu chochote kinachoonekana. Fungia mizigo yako yote nyuma ya gari, ikiwezekana. Pia, ujilinde dhidi ya wevi wanaovutiwa na mikusanyiko mikubwa. Hii inatia ndani kutoacha kitu chochote chenye thamani bila mtu wa kukitunza katika viti kwenye mikusanyiko. Kuongezea, imeripotiwa kwamba kuna hatari kubwa zaidi ya kuanguka juu ya ngazi wakati akina dada wanapovalia viatu vyenye visigino virefu. Tafadhali iweni waangalifu.