Kudhihirisha Imani kwa Matendo Mema
1 Matendo mema ni ithibati ya imani hai. Kwa mfano, imani huwasukuma Wakristo kutenda kwa huruma kuelekea wale wenye uhitaji. (Yak. 2:14-17, 26) Imani kama hiyo imedhihirika zaidi kwa njia ya kutokeza katika utegemezo unaotolewa kwenye programu ya ujenzi wa Jumba la Ufalme. Ingawa wanakumbwa na misongo yenye kuongezeka ya maisha ya kila siku, pamoja na gharama za ujenzi zinazoongezeka, Mashahidi wa Yehova katika sehemu zote za dunia wamethibitika kuwa “wale walio na juhudi katika matendo mema” kwa kujitolea kazi na kutoa fedha kulipia vifaa zaidi vya Majumba la Ufalme. (Tit. 2:14) Wakati “vitu vinavyotamaniwa na mataifa” vinapozidi kuingia katika tengenezo la Yehova, sisi tuna pendeleo la kuendelea kudhihirisha imani yetu kwa matendo yetu kwa niaba yavyo.—Hag. 2:7.
2 Uhitaji wa Sasa: Katika maeneo yote yaliyo chini ya tawi, sasa tuna jumla ya makundi 361. Kati ya hayo, sasa makundi 165 ama yana Majumba ya Ufalme yao au yanajenga Jumba la Ufalme. Vizuri sana! Hata hivyo, kama mwezavyo kuona, makundi mengi bado hukutana katika majumba yaliyokodishwa, kama vile katika majumba ya starehe na shule. Ratiba za mikutano zaweza kubadilishwa wakati wowote, au utumizi wa jumba waweza kukataliwa na wasimamizi kama wapendavyo. Hilo laweza kutukia kwa sababu ya ratiba zenye kuhitilafiana, shughuli za umma, na kadhalika. Katika hali hizo zote, vifaa vyote na viti ni vya kuondolewa, ikitaka kupangwa tena kwa kila mkutano na kubomoa baadaye. Nyakati nyingine sehemu hizo zinapambwa ndani na nje kulingana na kipindi cha sikukuu za kilimwengu. Pia, huenda jumuiya ikawa na maoni kwamba kundi halina udumifu, na hilo huzuia ukuzi. Hata hivyo, kwa sababu ya hali zenye kubadilika katika nchi fulani fulani, makundi mengi, katika eneo letu sasa yanaweza kuwa na Jumba la Ufalme lao wenyewe.
3 Makundi Yaweza Kusaidia: Kuna mengi ambayo kila kundi laweza kufanya ili kutegemeza programu ya ujenzi wa Jumba la Ufalme. Tunapotazamia mbele kwenye baraka ya Yehova kwa makundi yetu, ni lazima pia tufanye linalowezekana kwa habari ya muundo wa ujenzi ili kuweza kulipia uhitaji huo, bila kuweka mzigo usiohitajiwa juu ya marafiki. Tawi lina plani kadhaa za miundo ya Majumba ya Ufalme ambazo zapatikana kwa makundi yanayohusika katika miradi ya ujenzi. Hizo zitaandaliwa kwa wazee iwapo wataandika barua ya ombi. Ufikirio wa uangalifu wapaswa utolewe kwa kuchagua plani ambayo itatia ndani mahitaji ya sasa ya (ma)kundi na kuruhusu ukuzi wa kiasi kinachofaa. Mambo yote yapasa kuchunguzwa kwa uangalifu ili kujenga jumba ambalo si kubwa sana isivyohitajiwa au si ndogo sana.
4 Mnapoanza mradi wa ujenzi wa Jumba la Ufalme, uhitaji wa utegemezo wa kifedha kutoka kwenu wenyewe waweza kuzungumzwa kinaganaga na (ma)kundi linalohusika. Kadiri akina ndugu wa kwenu watakavyotoa kiasi kikubwa cha fedha kwa michango na mikopo, ndivyo uhitaji wa kukopa utakavyokuwa mdogo zaidi. Hilo huruhusu kiasi kikubwa zaidi cha msaada wa Sosaiti kiweze kupatikana kwa makundi mengine kutumia katika kujenga Majumba ya Ufalme yao. Ingawa Sosaiti iko tayari kusaidia kwa mikopo ya ujenzi ni vema kuchunguza kabisa kabisa uwezekano wa kupata fedha kutoka kwenu wenyewe kabla ya kuomba mkopo kutoka kwa Sosaiti.—Luka 14:28-30.
5 Uhitaji Ni wa Haraka: Mahali pekee pa mikutano panapotumiwa na makundi ya Mashahidi wa Yehova ni Jumba la Ufalme. Hivyo lina sehemu ya maana katika ukuzi wa ibada ya kweli. Tukiwa mashahidi waliojiweka wakfu wa Yehova, tukifundishwa naye, sisi hukusanyika pamoja kwa ukawaida “kuhimizana katika upendo na kazi nzuri.” (Ebr. 10:24) Ni baraka iliyoje kuona hesabu zinazoongezeka za watu wakijiunga pamoja nasi kwa sababu wao, pia, wanataka kuagizwa na Yehova na kutembea katika njia zake! (Isa. 2:3) Baada ya kupita kwa wakati, ukuzi huu wenye kuendelea wataka ujenzi wa Majumba ya Ufalme mengine zaidi.
6 Sosaiti inajua kwamba hali za kiuchumi leo zimefanya iwe vigumu kwa makundi mengine kupata vifaa vifaavyo vya mikutano na kwamba kuna uhitaji wa haraka wa kusaidia makundi hayo. Hiyo ndiyo sababu moja kwa nini Sosaiti iko tayari kusaidia makundi kifedha kwa ujenzi wa Majumba ya Ufalme yanayohitajiwa.
7 Tunapotazama mbele kwenye wakati ujao, tunaomba baraka za Yehova zenye kuendelea juu ya programu za ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Kwa utegemezo wetu wa moyo wote, tunaweza kuonyesha uthamini kwa Jumba la Ufalme na sehemu yayo katika kutusaidia kutiana moyo. (Ebr. 10:25) Hilo latia ndani utunzaji wa uaminifu wa Jumba la Ufalme letu wenyewe na kusaidia wengine kwa michango, kazi ya kujitolea, na utegemezo mwingine unaohitajiwa kadiri tuwezavyo. Kuhusiana na hilo acheni sote kwa kuazimia “tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.”—Gal. 6:9.