Kutangaza Habari Njema-Kwa Kuvuta kwa Maneno ya Usadikisho
1 Je! inafaa wahudumu wa habari njema wawavute watu kwa maneno ya usadikisho waukubali ukweli? Hakika inafaa! (Mdo. 18:4) Mtume Paulo alimkumbusha Timotheo kwamba yeye alikuwa amevutwa kwa maneno ya usadikisho na mama na nyanya yake awe mwamini. (2 Tim. 3:14) Kumvuta mtu kwa maneno ya usadikisho kunamaanisha kumwongoza mtu kwa kumsihi, kusababu kwa bidii pamoja naye kuhusu imani fulani, hali, au mwendo wa tendo.
2 Mtume Paulo alitumia vizuri ustadi wa kuvuta watu kwa maneno ya usadikisho. Alipokuwa Athene, “kuona jinsi mji ule ulivyojaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana ndani yake.” (Mdo. 17:16) Hata hivyo, aliposimama katikati ya Areopago, Paulo hakuwaambia waziwazi wale waliokuwapo kwamba ibada yao ya sanamu ilikuwa bure. Kwa ustadi akiepuka kukabiliana nao kwa ukali, alielekeza fikira zao kwenye “madhabahu iliyoandikwa maneno haya, KWA MUNGU ASIYEJULIKANA.” Baada ya hapo alitoa ushuhuda wa nguvu, akawa na matokeo mazuri.—Mdo. 17:23, 28, 29, 34.
UWE MWENYE UFAHAMU
3 Paulo alionyesha waziwazi kwamba kuvuta mtu kwa maneno ya usadikisho kunahitaji zaidi ya mahubiri ya kuvuta hisia tu au wingi wa maneno. Lazima tuwe na muono-ndani na kuwa wenye kufahamu hisia, imani, na mapendezi ya watu tunaozungumza nao. Tunahitaji kuwa macho na wenye haraka ya kutambua wakati hisia za mwenye nyumba huenda zikawa ndizo zinazozuia mazungumzo ya mafundisho ya Biblia kwa akili zilizofunguka.—Mit. 16:23.
4 Kwa kielelezo, huenda mtu akaamini kwamba nafsi haifi kwa sababu ya ufungamano wa kihisia wa kumbukumbu za upendo wa mpendwa aliyekufa. Ni njia gani yenye kuvuta kwa maneno ya usadikisho ambayo kwayo tungeweza kumsaidia na ukweli? Badala ya kumwambia moja kwa moja kwamba imani yake ni yenye makosa na kwamba nafsi hufa, je! halingekuwa jambo zuri kumvuta kwa maneno ya usadikisho ili kupenya kizuizi cha hisia ambacho huenda akawa nacho na kusababu naye? Tunaweza kumwambia kwamba tunafahamu hisia zake kwa sababu sisi pia tumepoteza wapendwa katika kifo. Tumepata faraja katika ahadi ya ufufuo, wakati ambapo tutaunganishwa tena na wapendwa waliokufa na kwa mara nyingine tena tushangilie ushirika wao. Kisha maandiko yanayofaa yanaweza kusomwa na kuzungumzwa. Tukiwa wenye ufahamu na kukoleza mazungumzo yetu kwa chumvi, tunaweza kuwa wenye kuvuta kwa maneno ya usadikisho katika kutangaza habari njema.—Mit. 16:21; Kol. 4:6.
TUMIA VIELEZI
5 Vielezi vinaweza kuwa na matokeo mazuri katika kuwavuta watu kwa maneno ya usadikisho warekebishe kufikiri kwao. Kielelezo kinachopaswa kukumbukwa ni njia yenye busara ambayo Nathani alitumia kufikia moyo wa Mfalme Daudi. (2 Sam. 12:1-14) Vielezi vinavyochaguliwa vizuri vinavuta akili na kugusa moyo. Vinafanya watu wafahamu mawazo mapya kwa urahisi. Kwa kielelezo, dunia inaweza kulinganishwa na makao na watu wapangaji. Ikiwa wapangaji wanashindwa kutunza makao vizuri, mwenye nyumba hataharibu nyumba ile, bali atawafukuza wapangaji. Kwa sababu hiyo, Mungu hataharibu dunia, bali ataondoa watu wabaya.—Isa. 45:18.
6 Kuvuta watu kwa maneno ya usadikisho kuna mipaka. Ikiwa watu hawataki kuamini au kufanya mabadiliko maishani mwao, watabaki kama walivyo. (Mt. 13:14, 15) Hata hivyo, kungali kuna watu wenye mioyo ya ufuataji haki katika ulimwengu wanaoweza kufikiwa kwa ujumbe wa Ufalme. Ili kuwasaidia, tunapaswa kujitahidi kikweli kukuza na kutumia ustadi wa kuvuta watu kwa maneno ya usadikisho katika huduma yetu.