Kutoa Habari Njema Kwa Mwelekeo wa Sala
1 Mtume Paulo aliandikia Wafilipi kwa njia yenye kutia moyo, “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Flp. 4:13) Sisi pia twahitaji kumtegemea Yehova kabisa kwa ajili ya imara ili kutoa habari njema kijasiri. Twaweza kufanyaje hivyo?
2 Yesu alikazia uhitaji wetu wa ‘kumwomba Mungu sikuzote, wala tusikate tamaa.’ (Luka 18:1) Paulo alisihi, “Ombeni bila kukoma.” (1 The. 5:17) Ndiyo, imara inatokana na kuomba. Twahitaji kutoa habari njema tukiwa na mwelekeo wa sala. Twaweza kuomba tupate fursa za kuwatolea wengine ushahidi, tupate hekima na ufahamu katika kazi ya nyumba kwa nyumba, na tupate mafanikio katika kufikia mioyo ya wanafunzi wetu wa Biblia. Kwa kuwa kuna uhitaji wa haraka wa kuhubiri habari njema za Ufalme kabla ya mwisho kuja, twahitaji pia kusali kwa ajili ya kusogezwa mbele kwa masilahi ya Ufalme ulimwenguni pote. (Mt. 24:14) Lazima ‘tukae tukikesha’ katika sala ili tuepuke usingizi wa kiroho na tuongeze uthamini wetu wa pendeleo letu la kunena kwa wengine juu ya makusudi ya Yehova.—Kol. 4:2; w62 uku. 497.
KATIKA MAFUNZO YA BIBLIA
3 Kwa nini sala ni ya maana hivyo wakati wa kuongoza funzo la Biblia? Kuanza funzo la Biblia kwa sala hutuweka katika hali inayofaa ya akili, na inamsaidia mwanafunzi kung’amua umaana wa yale yanayosemwa. Yeye anajifunza kumtegemea Yehova kwa ajili ya mwelekezo. Pia mwanafunzi anajifunza jinsi ya kusali kwa kielelezo chetu.—Luka 11:1.
4 Ni mambo gani yangefaa kutiwa katika sala wakati wa funzo la Biblia nyumbani? Sala ya Yesu ya kiolezo na sala za Paulo kwa ajili ya Wafilipi ni vielelezo bora. (Mt. 6:9-13; Flp. 1:9-11) Sala zetu hazihitaji kuwa ndefu, lakini zapaswa zishughulike na mambo hususa. Ni jambo la muhimu kwamba tutie ndani kumsifu Yehova kwa ajili ya kazi zake bora zisizo na hesabu. Twaweza kutia ndani utambuzi wa ukuu, adhama na sifa zake kamilifu. (Zab. 145:3-5) Kutaja jina la mwanafunzi wa Biblia, labda kukiri hali zake, na kusali kwamba afanye maendeleo ya kiroho kwaweza kunufaisha. Afanyapo maendeleo, twaweza kumwomba Yehova baraka juu ya jitihada zake za kuhudhuria mikutano na kushiriki pamoja na wengine ukweli anaojifunza. Tia ndani dua kwa ajili ya baraka za Yehova juu ya kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote.
KWA AJILI YA NDUGU NA DADA ZETU
5 Watu wote wa Yehova ni wafanyakazi wenzetu. (1 Kor. 3:9) Kwa hiyo, wakati wenye mamlaka walimwengu wanapotafuta kuingilia kuhubiriwa kwa habari njema, tunasukumwa tusali kwa ajili ya “wafalme na wote ambao wamo katika vyeo vya juu.” Kwa kusudi gani? “Ili kwamba sisi tuendelee kuishi maisha ya utulivu na kimya na ujitoaji kimungu kikamili na uzito.” (1 Tim. 2:1, 2, NW) Kwa kweli sala kama hizo zawapendelea ndugu zetu kuzunguka ulimwengu. Sisi twasali kwamba wenye mamlaka wawe na mwelekeo wenye kupendelea kazi yetu.
6 Kwa njia ya sala, twaweza kuomba kwamba ndugu zetu ambao huhubiri chini ya hali zenye magumu wapate imara na wale walio wagonjwa kiroho, kwamba waweze kupata ushiriki zaidi katika huduma. (2 The. 3:1, 2) Pia ni vizuri kusali kwa ajili ya wazee wa kundi, waangalizi wasafirio, na Baraza Linaloongoza—wale wote “wanaojitaabisha kwa ajili yenu.”—1 The. 5:12.
7 Nyakati zote twahitaji kumtupia Yehova mahangaiko yetu. (Zab. 55:22; 1 Pet. 5:7) Sisi tumehakikishiwa kwamba hata tuombe nini kupatana na mapenzi yake, atatusikia. (1 Yn. 5:14) Kwa hiyo, tukiomba usaidizi wa Yehova katika kuitimiza kikamili huduma yetu, yatupasa kuwa na uhakika kwamba yeye atasikiliza na kufanikisha njia yetu.—2 Tim. 4:5.