Kutoa Habari Njema—Kwa Mafanikio Zaidi kwa Kusikiliza
1 Ili kuwa na mafanikio katika huduma yetu, ni lazima sisi tutambue kwamba hakuna watu wawili wanaofanana. Kila mmoja ana mambo tofauti aliyojionea maishani na mahangaikio na tamaa tofauti za kibinafsi. Tatizo ni kufanya ujumbe wa Ufalme umfae kibinafsi, yaani, kuonyesha mtu tunayezungumza naye unayomaanisha kwake yeye akiwa mtu binafsi. Ili kufanya hivyo kwa mafanikio, ni lazima pia tusikilize kwa uangalifu.
2 Wahubiri wengi hutumia maswali kwa busara katika tangulizi zao, na hilo huwasaidia kumhusisha mwenye nyumba katika mazungumzo. Maswali ya maoni ambayo hayamwaibishi mwenye nyumba ni yenye mafanikio zaidi. Lakini wakati mwenye nyumba anaposema, ni jambo la muhimu kwamba tusikilize anayosema. Kusikiliza kwadhihirisha upendo wa jirani na staha, na kwa kufanya hivyo twapata ufahamu wa ndani wa kufikiri kwa mtu huyo. Kujua hali za mtu hutusaidia kumwonyesha huruma, tukijiweka katika mahali pake. Ndipo tunapoweza kushiriki pamoja naye faraja na tumaini kutoka katika Biblia.
UWE MWENYE KUBADILIKANA
3 Mtume Paulo alishauri hivi kwa upole: “Jifunze jinsi unavyoweza kuongea vizuri zaidi na kila mtu unayepata.” (Kol. 4:6, New English Bible) Ingawa hatutangulii kujua barabara yale ambayo huenda kila mtu mmoja mmoja akasema, sisi twafahamiana na matatizo ambayo watu wengi hukabili kila siku. Hivyo, twaweza ‘kujifunza’ na kujitayarisha kiakili kuitikia hali tofauti-tofauti.
4 Kwa mfano, huenda tukawa tulitayarisha kuzungumzia kichwa cha habari Hali Bora Zaidi Zatungojea, lakini mwenye nyumba ataja kwamba ameachishwa kazi yake. Je! tupuuze maelezo hayo? Pasipo shaka, jambo linalolemea akili na moyo wake ni jinsi ya kuruzuku watu wa nyumba yake. Ungeweza kuitikiaje mahitaji yake? Ungeweza kumhurumia, ukionyesha kuhangaikia kikweli hali yake. Halafu kwa fadhili uelekeze fikira zake kwenye maandiko yanayoonyesha jinsi serikali ya Mungu itakavyoandaa kazi yenye kuridhisha na mahitaji yetu yote.—Isa. 65:17, 21, 22, 24.
5 Labda twajua kwamba mtu huyo au mshiriki wa familia yake alipatwa hivi karibuni na uhalifu au tendo fulani lisilo la haki. Hangaikio letu lenye huruma na kupendezwa kibinafsi na hali hizo huenda kukalainisha moyo wa mtu huyo, hilo likiwezesha tumwonyeshe kwamba Yehova Mungu ajua sana matatizo hayo yenye kuumiza na karibuni yeye atachukua hatua kuondoa uovu wote.—Ona Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, kurasa 12, 13, 328-33.
6 Mara nyingi mahusiano yasiyofaa kati ya watu mmoja mmoja hutokea kwa sababu hawakuwasiliana ifaavyo. Mtu aongeapo, huenda yule mwingine asisikilize kikweli kwa akili na moyo wake. Mazoea hayo yasiyofaa ya kusikiliza hutokeza kutoelewanwa au kukosa fursa za kusaidia mtu. Kwa kusitawisha mazoea mazuri ya kusikiliza kwa staha, twaweza kutoa habari njema kwa mafanikio zaidi, tuonyeshe kupendezwa kusiko na ubinafsi kwa Yehova katika mapendezi ya wengine, na kusaidia wengine wasitawishe uhusiano mwema pamoja na Muumba wetu mwenye upendo na watu wake.—Yak. 1:19; g74 11/22 kur. 21-3.