Tumia Biblia Katika Utumishi wa Shambani
1 Maneno yaliyopuliziwa roho ya Biblia yaweza kuwa na athari yenye nguvu nyingi kwa watu. Kwa sababu hiyo, Wakristo wa karne ya kwanza, walitumia vizuri Maandiko wakati walipokuwa wakitangaza habari njema. Paulo ‘alitoa sababu kwa kutumia Maandiko,’ akifafanua na kuthibitisha mambo yake kwa marejezo. (Mdo. 17:2, 3) Apolo, alipokuwa akitolea Wayahudi ushuhuda, ‘alionyesha kwa maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo.’—Mdo. 18:24-28.
2 Leo Mashahidi wa Yehova hufuata kielelezo hicho. Kama ilivyotaarifiwa katika Mnara wa Mlinzi wa Machi 1, 1986, ukurasa 21: “Wanaposhiriki katika huduma ya waziwazi, wanataka watu watambue kwamba sio waliouanzisha ujumbe wanaoutangaza bali umetokana na Neno la Mungu mwenyewe. Kwa hiyo wao wanafanya matumizi ya moja kwa moja ya Biblia wakiwasomea wengine wakati inapowezekana.” Je, wewe unatumia kikamili Biblia katika huduma yako?
SABABU KWA NINI INA MATOKEO
3 Kwa nini Biblia ina matokeo sana? Kwa sababu hiyo ni Neno la Mungu na “li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.” (Ebr. 4:12) makusidio ya kweli ya watu mmoja mmoja hujitokeza wakati yafunuliwapo wazi kwa kweli ya Kimaandiko. Watu wa mioyo minyofu wanavutwa kwalo. Kwa mfano, wenzi wa ndoa wawili vijana waliofanya maendeleo ya haraka katika kumtumikia Yehova waliulizwa kwa nini waliitikia kwa haraka sana hivyo habari njema. Jibu lao lilikuwa nini? “Ni Biblia.” Wahubiri waliowatembelea walipoelekeza fikira zao kwenye Biblia, walitambua sauti ya “mchungaji mwema.”—Yn. 10:14. wSW78 11/1 kur. 11-12.
4 Je! nyakati nyingine wewe hujihisi kuwa unapungukiwa unapokuwa ukitumia Biblia yako katika utumishi wa shambani? Programu nzuri ya funzo la kibinafsi, kutia na kujitayarishia na kuhudhuria mikutano yote ya kundi, kutakutayarisha kwa kila kazi njema na kukupa uhakika zaidi. (2 Tim. 3:16, 17) Wenzi katika utumishi na washiriki wa familia waweza kufanya mazoezi pamoja ya kutumia Kichwa cha Mazungumzo. Pia, yaliyo mengi ya matangulizi katika kurasa 9-15 ya kitabu Kutoa Sababu yanahusu kusoma andiko mapema mwanzoni mwa mazungumzo. Kwa nini usijizoeze hayo? Tumia yale yanayoweza kutumika na yanayonasa kupendezwa kwa watu katika eneo lenu.
TUMIA UAMUZI MZURI
5 Kuna nyakati ambazo tutataka kumwalika mwenye nyumba alete nakala yake mwenyewe ya Biblia na kuangalia andiko pamoja nasi. Tumia uamuzi mzuri katika hali hizo. (Ona kitabu Kutoa Sababu, ukurasa 49, fungu la 2, na ukurasa 251, fungu la 4) Inapohitajiwa tufupize mazungumzo, twaweza kuamua kusoma andiko moja tu katika Kichwa chetu cha Mazungumzo. Au ikiwa wazi kwamba mwenye nyumba ana shughuli, twaweza kunukuu tu fungu la maneno lifaalo, tukimjulisha mwenye nyumba kwamba latoka katika Biblia. Yesu na mitume hawakuwa na nakala zao wenyewe za Maandiko ya Kiebrania za kwenda nazo walipokuwa wakihubiri. Hata hivyo wao walinukuu sana kutoka kwayo. Sisi pia twapaswa kujitahidi kushika maandiko ili tuwe nayo akilini tuyatumie katika huduma yetu.
6 Paulo alimhimiza Timotheo ‘atumie kwa halali neno la kweli.’ (2 Tim. 2:15) Onyo ilo hilo la upole latumika kwetu leo. Sisi twataka kumwiga Yesu na mitume kwa kutumia Biblia mara nyingi katika huduma yetu ya shambani. Isome wakati wowote inapowezekana, lakini ikihitajiwa, nukuu kutoka kwa yale uliyoshika akilini. Kufanya hivyo kwa mafanikio kutaifanya iwe wazi kwamba sisi ni wahudumu wa Mungu na kwamba msingi imara wa ujumbe wetu ni Neno lake.