Uwe Mwenye Nafsi Yote Katika Huduma ya Shambani
Sehemu ya 5: Faida Tele za Utumishi wa Nafsi Yote
1 Yehova anafanya faida tele zisizo na mipaka ziweze kupatikana kwa watumishi wake wenye nafsi yote. (Zab. 116:12) Tunawezaje kufurahia kadiri kamili ya mibaraka kutoka kwa Yehova katika utumishi wetu? Ni faida zipi tutakazopata? Ni lazima tufanye nini ili tujihakikishie wenyewe kibali chake na upendeleo wake?
2 Jitihada ya Kibinafsi Yatakiwa: Kadiri ile unayofurahia faida zinazotolewa na Mungu yategemea kwa kadiri kubwa jitihada zako mwenyewe za kufanya mapenzi ya Mungu. Kuhusu huduma, Paulo aliandika: “Kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu [kazi, NW] yake mwenyewe.” (1 Kor. 3:8) Acheni basi tuwe na ushiriki kamili katika utumishi kwa kadiri ile tuwezayo. Mtume Paulo alikuwa na thawabu ya binafsi ya kuwasaidia watu wengi, hata makundi mazima, kuja kumjua Mungu. Ni shangwe iliyoje ambayo alihisi akitazama imara yao katika imani! (1 The. 2:19, 20) Inaelekea kwamba hali zako hazitakuruhusu ujihusishe kikamili katika huduma kama ambavyo Paulo alikuwa. Hata hivyo, je! isingekuwa baraka kubwa kusaidia mtu au hata familia ya watu wenye mfano wa kondoo ithibitishwe kwa imara kwenye barabara inayoongoza kwenye uhai? Ni kichocheo kama nini cha kufanya kazi ya bidii katika huduma ya nyumba kwa nyumba na kufuatia ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia!
3 Faida Zaidi: Faida yenye thamani kubwa ya utumishi wa nafsi yote ni kwamba, akiwa mfanya kazi mwenzi, mtu huvutwa karibu zaidi kwa Yehova na Yesu Kristo. (Mt. 11:29, 30; 1 Kor. 3:9) Ni shangwe iliyoje kuhisi roho ya Mungu ikikusaidia katika huduma! (Mt. 10:20; Yn. 14:26) Zaidi ya hilo, kufanya kazi kwa bidii pamoja na wengine katika kundi huimarisha kifungo chetu cha upendo na umoja.
4 Hatuwezi kufurahia faida kamili kutoka kwa Yehova ikiwa hatutegemezi kikamili tengenezo analotumia kutimizia mapenzi yake katika siku hizi za mwisho. (Linganisha 2 Wafalme 10:15.) Tunapofuata kwa ukaribu na kwa moyo wote mwongozo tunaopokea kupitia kipitio cha Mungu na kuhusika kwa bidii katika utendaji wa kundi, tunalindwa kiroho kutokana na mbinu za kiufundi za Shetani. Tunawezeshwa kuwa na ushiriki wenye mazao zaidi katika huduma.
5 Mfululizo huu wa makala wenye sehemu tano juu ya kuwa wenye nafsi yote katika huduma ya shambani umekazia mambo kadha yanayohusika. Je! unakumbuka njia za kujenga uthamini wa Yehova ni zipi, ambazo husukuma mtu kuwa mwenye nafsi yote? (Julai) Kwa nini kujitayarisha ni kwa lazima katika kusitawisha shauku katika utumishi wa shambani? Tunaweza kujitayarishaje? (Agosti) Wahubiri wenye ujuzi wanawezaje kusaidia wengine kuwa wenye nafsi yote? (Septemba) Utengenezo mzuri wa kibinafsi waweza kutusaidiaje kuwa wenye nafsi yote katika huduma? (Oktoba) Je! unatumia madokezo hayo?
6 Yehova ataka tujifaidi wenyewe kwa kumtii yeye. (Isa. 48:17) Zaidi ya hilo, faida za utumishi wa nafsi yote zawafikia wale wanaokusikiliza. (1 Tim. 4:15, 16) Waweza kuwa na uhakika kwamba ukijitumikisha kwa bidii katika kazi iliyopo sasa, Yehova ataona hayo na ‘utapokea thawabu ya ule urithi,’ uhai wa milele.—Kol. 3:23, 24, NW.