Tayarisha Utoaji Wako wa Februari
1 Wakati wa Februari, tunatoa kitabu chochote cha kurasa 192 kilichochapishwa katika 1983 au mapema zaidi au kitabu Usalama Ulimwenguni Pote. Chochote cha vichapo hivyo vizuri chaweza kutumiwa kutoa habari njema kwa njia nyingi. Bila shaka utaona kuwa inafaa kujifunza na kutumia utoaji mmoja au wote ufuatao uliodokezwa.
2 Dunia—Makao ya Kudumu ya Mwanadamu: Ikiwa unataka kuanza mazungumzo pamoja na watu wanaoihangaikia dunia na mazingira yayo, jaribu kichwa “Dunia Kudumu Milele Ikiwa Makao ya Ainabinadamu.” Kichwa hiki ni chenye kunyumbulika vya kutosha kuvutia fikira za watu wenye familia, wapenda uumbaji wa asili, na wanamazingira. Andiko la kutumia ni Mhubiri 1:4. Kichwa hicho na andiko limeelezwa katika kitabu Usalama Ulimwenguni Pote, kurasa 98-9, mafungu 2 na 3.
3 Baada ya kujijulisha, ungeweza kusema:
◼ “Ninazuru kifupi kuzungumza jambo linalohangaisha kila mmoja wetu. Dunia ni makao yetu, na bila shaka hata wewe unahangaikia jinsi inavyoharibiwa. Wanasayansi na wanamazingira wanaendelea kuonya kwamba ikiwa uchafuzi unaendelea, dunia ingeweza kuwa mahali pasipoweza kukalika. Je! unaona suluhisho lolote kwa tatizo hilo? [Tua ili mwenye nyumba aeleze ikiwa ataka.] Ningependa kukuonyesha kifupi yale ambayo Biblia husema kuhusu wakati ujao wa dunia kwenye Mhubiri 1:4.” Soma andiko hilo, na uonyeshe maelezo katika mafungu 2 na 3 kwenye kurasa 98-9 za kitabu Usalama Ulimwenguni Pote.
4 Uovu Utaondolewa: Ili kuwavutia watu wanaohangaikia uhalifu, jeuri, na vita, labda utapenda kuzungumza nao kuhusu kichwa “Uovu Kuondolewa Ili Wale Wanaompenda Mungu Waweze Kufurahia Maisha na Amani.” Zaburi 37:9-11 inatokeza jambo hilo na imeelezwa katika kitabu Usalama Ulimwenguni Pote, kurasa 118-20, mafungu 13-15.
5 Kufuatia utangulizi wa kawaida, ungeweza kusema:
◼ “Je! unafikiri wakati utakuja ambapo hatutakabiliana tena na uhalifu na jeuri? [Ruhusu itikio la mwenye nyumba.] Biblia inaelekeza kwenye suluhisho la kudumu hapa kwenye Zaburi 37:9-11.” Soma andiko hilo na ufungue kurasa 118-20 katika kitabu Usalama Ulimwenguni Pote ili usome sehemu zilizochaguliwa za mafungu 13-15.
6 Tumaini la Ufufuo: Kwa kuwa wakati fulani kila mtu amepoteza mpendwa wake katika kifo, lingekuwa jambo la kufariji kuanzisha mazungumzo juu ya kichwa “Utawala wa Ufalme Utarudisha Kwenye Uhai Wapendwa Waliokufa Chini ya Hali za Paradiso.” Ungeweza kutumia ama Yohana 5:28, 29 ama Luka 23:43 na kuonyesha maelezo juu ya kichwa na andiko hilo yanayopatikana katika kitabu Usalama Ulimwenguni Pote, kurasa 166-7, mafungu 12 na 13.
7 Ungeweza kuanza mazungumzo yako kwa utangulizi wa kwanza katika ukurasa wa 14 wa kitabu “Kutoa Sababu” halafu useme:
◼ “Wakati mmoja au mwingine wengi wetu hufikiria wapendwa wetu tuliopoteza katika kifo. Lakini unafikiri tutaweza kuwaona tena? [Mpe mwenye nyumba nafasi ya kujieleza.] Watu wengi tunaosema nao hushangaa kujifunza yale Neno la Mungu limeahidi na kwamba taraja hilo litatimizwa hapa hapa duniani. Angalia ahadi ya Biblia kwenye . . . ” Tumia ama Yohana 5:28, 29 ama Luka 23:43, na uunganishe na maelezo katika mafungu 12 na 13 kwenye kurasa 166-7 za kitabu Usalama Ulimwenguni Pote au vielezi katika kurasa 164-5.
8 Tayarisha na utumie utoaji mmoja au wote huo mwezi huu. Haipasi kuwa vigumu kupata manukuu na vielezi vinavyofaa katika vichapo vyovyote utakavyotumia. Ikiwa kichapo hakichukuliwi, toa trakti yenye kichwa kinachohusiana.