Nufaika Kabisa Kwa “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1993
1 “Unifundishe mimi, Ee Yehova.” (Zab. 86:11, NW) Hilo lapasa kuwa ombi la bidii la kila mtumishi wa Mungu aliyejiweka wakfu. Tumeazimia hatutaacha kamwe kujifunza na hatutaacha kamwe kutumia yale tunayojifunza. Nyakati nyingine twahitaji kurekebishwa, na kama vile mtunga-zaburi, twahitaji kumsihi Mungu aungamanishe moyo wetu ili usigawanyike. Programu kwenye “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya itaandaa maagizo na marekebisho yanayotumika tunayohitaji ili kumtumikia Yehova kwa uaminifu kujapokuwa misongo ya mfumo huu wa mambo.
2 Mkusanyiko wa Siku Nne: Programu hiyo itatolewa kwenye mahali 13 pafaapo kotekote katika Afrika ya Mashariki. Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1993 yaandaa orodha kamili ya mahali hapo. Kuongezea Kiingereza, programu nzima itatolewa katika Kiamhari, Kinyarwanda, Luganda, Kitigrinya na Kiswahili. Kwenye mahali pawili kutakuwa na ufasili wa lugha ya ishara. Programu itaanza Alhamisi saa 7:20 alasiri na itamalizika Jumapili alasiri saa 10:15 hivi. Milango itafunguliwa kwenye kila mkusanyiko saa 1:30 kila asubuhi. Tafadhali angalieni kwamba hakuna mtu atakayeruhusiwa kuingia kabla ya saa 1:30 asubuhi isipokuwa kama amegawiwa kazi kabla ya wakati huo.
3 Ni mambo gani tutakayopata huko? Chakula kingi kigumu cha kiroho kikitolewa katika njia mbalimbali: hotuba, maonyesho, mahoji, na drama mbili. Usikose yoyote kati ya maagizo hayo muhimu! Kuongezea hayo, twatazamia kufanya upya urafiki wa zamani na kufanyiza mwingine mwingi. Huenda wamishonari wanaotumikia katika migawo ya kigeni wakahudhuria mkusanyiko wenu. Tumia fursa hiyo kupata kuwajua ndugu na dada hao waaminifu. Ikiwa wewe ni mzazi, watie ndani watoto wako katika mazungumzo. Roho ya shangwe na ya kujidhabihu ya wamishonari hao yaweza kuwekea msingi watoto wako wafikirie kazi-maisha katika utumishi wa wakati wote.
4 Je, Utaleta Sehemu ya Kumi Yote Ghalani? Kwenye Malaki 3:10, Yehova aliwaahidi Waisraeli kwamba ikiwa walikuwa na nia ya kumjaribu na kuleta sehemu ya kumi yote ghalani, yeye angemwaga baraka hadi kuwe hakuna upungukio zaidi.
5 Kwa watu fulani, kumjaribu Yehova kutamaanisha kumfikia mwajiri wao upesi iwezekanavyo kumwomba likizo au wakati wa livu ili kuhudhuria mkusanyiko. Nyakati nyingine ndugu wamesita kufanya hivyo, wakidhania kwamba mwajiri wao asingewapa kamwe ruhusa kuhudhuria mkusanyiko. Lakini, katika mambo yasiyohusu mambo ya kiroho, huenda wasione ugumu kumwambia mwajiri wao yale wanayokusudia kufanya.
6 Twahitaji kujiuliza wenyewe hivi: Ikiwa rafiki mpendwa alikuwa akiolewa katika sehemu nyingine, je, tusingemfikia mwajiri wetu na kuomba ruhusa ya kuhudhuria harusi hiyo? Na iwapo angeonekana kusita, je, tusingemweleza kwa heshima jinsi tungethamini sana kwenda? Kwa kweli ni jambo la maana zaidi kufundishwa na Yehova kuliko kuhudhuria harusi! Ikiwa twasadiki kikweli kwamba programu ya mkusanyiko ni muhimu kwa ukuzi wetu wa kiroho, itakuwa rahisi zaidi kusadikisha mwajiri wetu aturuhusu tuhudhurie mkusanyiko.—Yak. 1:7, 8.
7 Katika Israeli sehemu ya kumi ilitia ndani utegemezo wa kimwili kwa ajili ya mahali pa ibada pa Yehova. Katika siku yetu sehemu ya kumi inawakilisha wakati, nishati, na fedha zinazotumiwa moja kwa moja katika utumishi wa Yehova na katika kuunga mkono kazi ya Ufalme. Sehemu ya kumi inatia ndani wakati tunaotumia mikutanoni, makusanyikoni, na mikusanyikoni, kutia na katika kudumisha na kusafisha mahali petu pa kukutania. “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya utatupa fursa nyingi kuleta sehemu ya kumi yote katika ghala la kiroho la Yehova. Ni nini baadhi yazo?
8 Twaweza kuleta sehemu ya kumi kwa kusikiliza kwa uangalifu programu ya mkusanyiko, kwa kushiriki kwa idili katika kuimba kila wimbo wa Ufalme, na kwa kusikiliza kwa uangalifu kila sala, ili tuweze kuongeza amina yetu yenye kuhisiwa moyoni.
9 Maendeleo yetu katika kweli yategemea kwa kiwango kikubwa jinsi tunavyosikiliza. Katika jumba au stediamu kubwa, ni rahisi kukengeushwa na mambo wanayofanya wengine karibu nasi, na kwa hiyo ni lazima tusiache akili yetu ikengeushwe. Hakikisha unakuja kwenye mkusanyiko ukiwa umejitayarisha kabisa, ukiwa na Biblia yako, kitabu cha nyimbo, kalamu na karatasi, na toleo la Mnara wa Mlinzi litakalosomwa juma hilo. Ni jambo lenye kusaidia kuandika mambo makuu na maandiko yanayotumiwa na kila msemaji. Usiandike mambo mengi; kuandika mambo mengi mno kwaweza kuzuia kukaza fikira. Wachanga pia wapaswa kuzoezwa kuwa wasikilizaji wasikivu. Watoto waweza kuleta sehemu ya kumi pamoja na wazazi wao kwa kufuata programu kwa ukaribu kadiri iwezekanavyo.
10 Wazazi fulani hupanga kuwa na wakati mtulivu nyumbani kila siku wakati watoto wao wanapotazamiwa kusoma au kutazama picha kwenye kimojapo vichapo vya Sosaiti. Mazoezi hayo mazuri hufanya iwe rahisi zaidi kwa watoto kuketi kwa utulivu wakati wa mikutano na mikusanyiko. Wazazi ambao wamelea watoto walio kielelezo chema husema kwamba hawaruhusu kamwe watoto wao walete vitu vya kuchezea au vitabu vya kuchorea kwenye mikutano. Hata watoto wachanga sana waweza kujifunza kwamba sababu ya kuhudhuria mikutano ni kuabudu Yehova. Wazazi wanaowafundisha watoto wao yale yanayomaanishwa kwao kuleta sehemu ya kumi yote ghalani wastahili pongezi kwelikweli!
11 Twaweza pia kuleta sehemu ya kumi kwa kutoa kwa hiari wakati na nishati zetu kusaidia mpango wa mkusanyiko. Kwenye mahali pengi usafi wa kabla ya mkusanyiko hupangwa siku moja au mbili kabla ya mkusanyiko kuanza. Ikiwa wewe waishi karibu na hapo, kwa nini usipange ili familia nzima ishiriki? Baadhi ya ndugu wamewaleta mafunzo yao ya Biblia wenye maendeleo ili hata kabla ya wapya hao kubatizwa waweze kujifunza yale yanayohusika katika kutegemeza ibada ya Yehova. Kuna mengi ya kufanya ili kuhakikisha kwamba mkusanyiko utaendeshwa vizuri. Kwa nini msijitoe mkiwa familia?
12 Njia nyingine ya kuleta sehemu ya kumi ni kwa kutegemeza kifedha tengenezo. Katika kuonyesha jinsi zawadi za kimwili zingetolewa ili kutegemeza ibada safi, Yehova aliamuru taifa la Israeli hivi: ‘Msitokee mbele za Yehova mikono mitupu. Kila mtu na atoe kama awezavyo, kwa kadiri ya baraka ya Yehova, Mungu wako alivyokupa.’ (Kum. 16:16, 17) Iwe watu waliweza kutoa vingi au vichache, utoaji wao, uliotayarishwa mapema, ulimpendeza Yehova. Vivyo hivyo, ndugu wengi hutoa fikira kwa sala kwa mchango watakaotoa, iwe ni kwa fedha au kwa hundi (iliyoandikiwa “Mashahidi wa Yehova”). Je! wewe huacha watoto wako wadogo watie mchango katika sanduku wakati wowote?
13 Yapambe Mafundisho ya Mwokozi Wetu, Mungu: Kwa tabia zetu njema na mwenendo wetu ufaao, twaweza ‘kuyapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’ (Tit. 2:10) Yaani, mumo humo kwenye mkusanyiko, twaweza kuonyesha kwamba ufundishaji wa kimungu unatumiwa katika maisha zetu.
14 Vipi juu ya adabu zetu? Kuwafikiria wengine ni nadra sana leo katika ulimwengu. Lakini watu wa Yehova, wanaoongozwa na kanuni za Kimaandiko, hufikiri, si juu ya faida yao wenyewe, bali juu ya faida ya wenzao. (Flp. 2:4) Twawajali wale walio karibu nasi. Tunapopanga mistari ili kupata chakula au vichapo, hatusukumani. Twawafikiria wazee-wazee na watoto wadogo ambao huenda wakawa wanangoja katika mstari pamoja na wazazi wao na ambao kwa urahisi wangeweza kusukumwa na watu wazima ambao huenda wasiwaone. Katika mikahawa tunakuwa wapole na wenye adabu kwa wafanyakazi, si wafidhuli au wenye kudai ikiwa utumishi hauridhishi matazamio yetu. Na twafurahi kufuata ile desturi ya kuacha bakshishi ya kiasi ya asilimia 15 kwa utumishi uliotolewa.
15 Mwenendo wetu wa kimungu una matokeo halisi kwa wale walio karibu nasi. Katika jiji moja la mkusanyiko mwaka jana, polisi mmoja aliyekuwa amekuwa katika idara ya polisi kwa miaka 21 alikuwa na haya ya kusema: “Nimevutiwa na nidhamu ya watu wenu. [Wao ni] wenye kutokeza; wanakusanya takataka bila yeyote kuwaomba wafanye hivyo na ni wenye utaratibu na mkusanyiko wenu umepangwa vizuri.” Yeye aliongeza hivi: “Watu wenu wanapotuona, wao hutabasamu. Hiyo ni ishara nzuri. Sisi huwa macho kuona hiyo. Hiyo ni ishara ya urafiki na hakuna chochote cha kuficha. Na twaona pia jinsi watoto wanavyoketi na wazazi wao na ni wenye nidhamu bora. Nakuambia, nimevutiwa. Inafurahisha kupewa mgawo hapa.”
16 Maofisa fulani walifanya safari ya pekee kwenda Betheli ili kutoa mwaliko wa kufanya mkusanyiko katika jiji lao. Sosaiti ilikubali mwaliko huo wa fadhili, na wenye jiji hawakutamauka. Meneja msaidizi wa jiji alisema hivi: “Tunasisimuka sana kuwa na kikundi chenye umashuhuri kama hiki chenu kukutana jijini mwetu. Tulifanya jitihada kubwa ili mje hapa . . . na tulifurahi sana.” Kwa mwenendo wao mwema, kila ndugu na dada alichangia kwenye ushahidi bora uliotolewa huko.
17 Je! wewe binafsi utayapamba mafundisho ya Mwokozi wetu, Mungu, kwa mwenendo wako mwema? Hapa pana njia kadhaa ambazo kwazo hilo laweza kufanywa:
Mavazi na kujipamba: Wakati ambao tunahudhuria mkusanyiko, hatupaswi kujiona wenyewe kuwa likizoni. Badala ya hivyo, twajitoa kwa Yehova ili tufundishwe naye. Kwa kuwa hivyo ndivyo ilivyo, je, hatupaswi kuvaa kama vile tungevaa tunapohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme? (1 Tim. 2:9, 10) Kuongezea hilo, twapaswa kutoa fikira za uangalifu kwa yale tutakayovaa baada ya vipindi kuisha. Hata tuwe na umri gani, baada ya kurudi mahali tunapolala, je, kungekuwa kupatana kubadili mavazi yetu ya mkusanyiko yenye kiasi na staha kwa mavazi ambayo yangetupatia sura ya walimwengu waliovalia ovyo-ovyo na bila utaratibu? Je! hilo halingetokeza wazo kwamba mavazi yetu ya mikutano ni ya kuvaliwa tu kwa kusudi fulani badala ya kuwa wonyesho wa njia yetu ya maisha? Kumbuka, tunalichukua jina la Yehova, na kila mmoja wetu lazima ahakikishe kwamba shtaka halali haliletwi dhidi ya njia ya kweli.
Watakaobatizwa wapaswa wakumbushwe kwamba haifai kuvaa T-shati zenye shime na maneno ya kilimwengu au zenye matangazo ya kibiashara kwenye pindi hiyo takatifu. Wazee wapaswa wahakikishe kwamba maswali ya ubatizo yapitiwa mapema sana na kwamba kila atakayebatizwa aambiwa mapema kama amekubaliwa kubatizwa au la. (Mnapopitia maswali, huenda huo ukawa wakati mzuri wa kutoa madokezo kuhusu mavazi yafaayo, yenye kiasi kwa ajili ya ubatizo.) Haitakuwa lazima kwa watakaobatizwa waliokubaliwa na wazee kujiandikisha kwenye mkusanyiko.
Hoteli na moteli: Onyesha matunda ya roho unapoingia kwenye hoteli au moteli yako. Huenda wafanyakazi wa hoteli wasiweze kushughulikia kikundi kikubwa katika muda mfupi. Uwe mwenye subira, mwenye hisia-mwenzi, na kutoa bakshishi ifaavyo.
Watoto waweza kufanya sehemu yao kwa kuonyesha staha kwa mali ya hoteli na kwa kutii sheria zinazoongoza utumizi wa bwawa la kuogelea na vifaa vinginevyo. Ni jambo lenye kusaidia ikiwa wazazi wangetumia wakati fulani kabla ya mkusanyiko kukumbusha watoto wao aina ya tabia watakayotazamiwa kuwa nayo, wakiwakumbusha juu ya daraka lao la kibinafsi la kushikamana na viwango vya mwenendo wa Kikristo.
Vifaa vya Kurekodia: Ingawa kamera za vidio zakubaliwa, twajua kwamba mtawafikiria wengine. Hakungekuwa kuonyesha upendo kuwaziba wanamkusanyiko wenzetu wasione huku tukinasa programu. Ikiwa waweza kurekodi kwa busara ukiwa kwenye kiti chako, hakuna ubaya wa kufanya hivyo. Hata hivyo, tafadhali kumbuka kwamba kamera au vifaa vya kurekodia havipaswi kuunganishwa na mfumo wa umeme au wa sauti kwenye mkusanyiko, wala vifaa havipaswi kuwekwa kwenye vijia au mahali pa watu kupitia.
Viti: Tafadhali kumbuka kwamba VITI VYAWEZA KUHIFADHIWA TU KWA WASHIRIKI WA KARIBU WA FAMILIA YAKO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE KATIKA GARI LAKO. Sehemu za pekee kwa ajili ya walio wazee-wazee na walemavu zitapatikana kwenye mikusanyiko yote. Tafadhali wafikirieni wazee-wazee. Katika nyakati zilizopita, ndugu fulani wenye umri mkubwa wamelazimika kutafuta viti katika sehemu zisizofikiwa kwa urahisi kwa sababu wachanga walijaza viti katika sehemu ya wazee-wazee. Twasikitika kwamba haiwezekani kushughulikia maombi ya kupata sehemu au vyumba vya pekee kwa wale wenye matatizo kama vile mizio (allergies).
Vifaa vya Kibinafsi: Inadokezwa kwamba vifaa vya kibinafsi unavyoleta kwenye mkusanyiko viwe vichache kadiri iwezekanavyo. Ikiwa kifaa hakitoshei chini ya kiti chako, huenda ikawa afadhali kukiacha nyumbani au katika mahali pa mizigo kwenye gari. Vifaa vikubwa vya kuhifadhi baridi ya chakula haviruhusiwi katika vijia kwa sababu ya usalama, na ikiwa vinawekwa juu ya kiti kando yako, mtu fulani huenda akakosa kiti.
Utumishi wa Fasihi na Chakula: Sisi sote twataka kuonyesha uthamini kwa zawadi nzuri za Mungu, tukihakikisha kwamba hakuna kitu kinachotumiwa vibaya. (Yn. 6:12) Kama vile katika nyakati zilizopita, twadokeza kwamba mpate tikiti zenu za chakula mapema. Mwaweza kuanza kupangia sasa kuweka kando fedha fulani kwa ajili ya fasihi. Tafadhali onyesheni ufikirio wenye upendo kwa wengine mnapopanga mstari ili kupata chakula au fasihi.
18 Kwa kuwafikiria wengine kwa upendo, panga kufika mapema kila siku, hasa Alhamisi wakati ambapo itakuchukua wakati mwingi zaidi kuliko kawaida kupata mahali pa kuegesha na pa kuketi.
19 Tuna pendeleo kama nini kufundishwa na Yehova! Utumizi wetu wa wakati, nishati, na mali za kimwili ili kuunga mkono “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya utatokeza manufaa za kiroho zenye kudumu kwetu wenyewe na kwa familia zetu.
Vikumbusha vya Mkusanyiko wa Wilaya
Adabu Nzuri: Ni jambo la maana kwamba wote wanaohudhuria mkusanyiko wawe na adabu nzuri, wakiona kwa kicho chenye staha mahali pa mkusanyiko kuwa ‘nyumba ya Mungu.’ (Zab. 55:14) Wakati wa hotuba, drama, nyimbo, na hasa sala, tafadhali epuka kufanya jambo lolote ambalo lingeweza kukengeusha fikira za wengine wasisikilize programu. Kwenda huku na huku bila lazima, kuwa na mazungumzo, au kutumia kamera zenye mmweko au vidio za kurekodi kwa njia inayokengeusha wale wanaojaribu kukazia akili yale yanayosemwa hakungekuwa kuonyesha staha. Ufikirio wetu na mwenendo mwema utaonyesha kwamba twathamini kikweli ufundishaji wa kimungu na tumekuja kwenye mkusanyiko ili kuagizwa na Yehova.
Mahali pa Kulala: Ushirikiano wenu katika kutumia mahali pa kulala palipoorodheshwa tu na mkusanyiko wathaminiwa sana. Ikiwa unapanga kulala katika jiji la mkusanyiko na bado hujahakikisha juu ya kupata mahali pa kulala, tafadhali fanya hivyo mara hiyo. Ukiona ni lazima uondoe ombi lako la mahali pa kulala, wapaswa uandike au upige simu moja kwa moja kwa moteli hiyo, ukifanya hivyo mapema kadiri iwezekanavyo ili chumba hicho kiweze kupewa mtu mwingine.
Waandishi wa makutaniko wapaswa wahakikishe kwamba fomu za Mahitaji ya Pekee ya Mahali pa Kulala zinapelekwa bila kukawia kwenye anwani ifaayo ya mkusanyiko. Ikiwa ni lazima uondoe ombi la mahali pa kulala lililofanywa kupitia mpango wa mahitaji ya pekee, wapaswa ujulishe mara hiyo mpangaji au moteli na Idara ya Mahali pa Kulala ya mkusanyiko ili mahali hapo papewe mtu mwingine.
Vigari vya Kusukumia Watoto: Katika mahali pengi huenda vigari vya kusukumia watoto visitumiwe katika mahali pa kusanyiko la umma. Kanuni za moto hukataza kuviegesha katika vipitio na vijia au kati ya safu za viti. Kwa kuwa umati mkubwa waweza kusababisha hali ya msongamano, viti vya kusukumia watoto vyaelekea kuwa hatari si kwa mtoto tu bali pia kwa yeyote ambaye aweza kujikwaa kwavyo. Hivyo tafadhali msivilete kwenye mahali pa mkusanyiko. Hata hivyo, viti vya watoto wachanga au vya gari vinaruhusiwa, kwa kuwa hivyo vyaweza kuwekwa salama katika viti kando ya wazazi. Ushirikiano wenu katika jambo hilo unathaminiwa.
Ubatizo: Watakaobatizwa wapaswa kuwa kwenye viti vyao katika sehemu iliyoonyeshwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Mavazi yenye kiasi na taulo yapasa kuletwa na kila mmoja anayepanga kubatizwa. Baada ya hotuba ya ubatizo na sala ya msemaji, mwenyekiti wa kipindi atatolea watakaobatizwa maagizo mafupi na kisha ataomba wimbo uimbwe. Baada ya mstari wa mwisho, wakaribishaji watawaelekeza watakaobatizwa kwenye mahali pa uzamisho au kwenye magari yatakayowapeleka hapo. Kwa kuwa ubatizo kwa kufananisha kujiweka wakfu kwa mtu ni jambo la siri na la kibinafsi kati ya mtu na Yehova, hakuna uandalizi kwa ule unaoitwa eti ubatizo wa shirika ambao watu wawili au zaidi watakaobatizwa hukumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.
Utumishi wa Kujitolea: Msaada wa kujitolea wahitajiwa ili mkusanyiko wa wilaya uendeshwe vizuri. Hata ikiwa waweza kufanya kazi kwa sehemu fulani tu ya mkusanyiko, utumishi wako utathaminiwa. Ikiwa waweza kusaidia, tafadhali piga ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kwenye mkusanyiko. Watoto wa umri ulio chini ya miaka 16 waweza kuchangia pia kufanikiwa kwa mkusanyiko, lakini watakwa wafanye kazi pamoja na mzazi au mtu mwingine mzima anayeweza kuchukua daraka.
Kadi za Beji: Tafadhali vaa kadi ya beji iliyofanyizwa kipekee kwenye mkusanyiko na unaposafiri kwenda na kutoka mahali pa mkusanyiko. Mara nyingi hii hutuwezesha tutoe ushahidi mzuri tunaposafiri. Kutambulishwa kuwa mjumbe wa mkusanyiko kwa kadi ya beji iliyoandikwa waziwazi kutawezesha uendeshaji wa mpango wa utumishi wa chakula uliorahisishwa. Wapaswa upokee kadi ya beji kupitia kutaniko lako kwa sababu hazitapatikana kwenye mikusanyiko.
Kitambulisho cha Kibinafsi: Kuongezea kadi ya kunjo la koti ya “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko, kila mtu atiwa moyo awe na kadi yake ya Mwelekezo wa Kitiba. Washiriki wa familia ya Betheli na mapainia wapaswa pia wawe na kadi zao za kitambulisho.
Maneno ya Tahadhari: Hata uwe waegesha wapi, funga gari lako nyakati zote na usiache ndani kamwe kitu chochote kinachoonekana. Fungia mizigo yako katika mahali pa mizigo, ikiwezekana. Pia, ujilinde dhidi ya wevi na wakwepuzi wa mifuko wanaovutiwa na vikusanyiko vikubwa. Hii yatia ndani kutoacha kitu chochote chenye thamani juu ya viti bila mtu wa kukitunza kwenye mkusanyiko. Hata kumekuwa na ripoti chache juu ya watu wapotovu wanaojaribu kuwashawishi watoto waende mbali na sehemu ya mkusanyiko. Tafadhali iweni waangalifu.
Uangalifu wapaswa pia kutolewa ili kuepuka kupakia watu wengi kupita kiasi katika magari yaliyokodiwa au kupangwa na kutaniko kwa ajili ya usafiri wa kwenda kwenye mkusanyiko. Ni afadhali kupanga kutumia fedha za ziada katika gharama za usafiri kuliko kuvunja sheria za Kaisari au lililo baya hata zaidi, kuwahatarisha akina ndugu wapatwe na aksidenti na hata uwezekano wa kupoteza uhai kwa sababu ya kupakia watu wengi kupita kiasi au kumtia shime dereva aongeze mwendo ili mfike mapema zaidi mnakoenda. (Rum. 13:1-7; Kum. 21:1-9) Ndugu wenye daraka wanaosafiri katika magari kama hayo wajihisi huru kutoa shauri lenye upendo kuhusu jambo hilo ikiwa inahitajiwa.