Kushughulikia Mahitaji ya Kiroho ya Viziwi
1 Idadi inayoongezeka ya viziwi wanavutwa kwa Mchungaji Mwema na wanaingia katika uhusiano wa kujitoa kwa Yehova Mungu. (Yn. 10:3, 11) Wengine katika kutaniko, hasa wazee, lazima wawe macho kuona mahitaji ya kiroho ya ndugu na dada viziwi.
2 Kutosheleza Mahitaji ya Viziwi: Mipango hufanywa ili kutafsiri mikutano ya kutaniko katika lugha ya ishara mahali wakalimani waliostahili wapatikanapo. Ikiwa hakuna yeyote katika kutaniko ajuaye lugha ya ishara, huenda ikafaa kuelekeza viziwi kwenye kutaniko la karibu linaloweza kuandaa utumishi huo. Bila shaka, ikiwa hakuna mpango kama huo katika eneo lenu la ujumla, huenda ikawezekana kwa wahubiri waliowekwa kuwa na zamu ya kuketi kando ya viziwi na kushiriki maandishi pamoja nao juu ya mambo makuu yanayozungumzwa.
3 Mipango ya Mzunguko na Kutaniko: Mipango ya kutafsiri lugha ya ishara kwenye makusanyiko ya mzunguko na siku za kusanyiko la pekee huratibishwa kupitia mwangalizi wa mzunguko. Mzee au mtumishi wa huduma anayestahili aweza kuchaguliwa kuwa mratibu. Ndugu na dada wanaostahili walio mfano mwema waweza kugawiwa kushiriki katika kutafsiri programu ya kusanyiko. Kanuni hiyohiyo yaweza kufuatwa katika kutaniko, ikihakikisha kwamba mahitaji ya viziwi yanashughulikiwa ifaavyo.
4 Ni afadhali viziwi waketi pale wanapoweza kuona wakalimani na jukwaa katika mstari uleule wa jicho. Ni hivyo kwenye mikutano ya kutaniko na pia kwenye makusanyiko ya mzunguko. Kwenye mikutano ya kutaniko, ikiwa idadi ya viziwi waliohudhuria ni ndogo, ni afadhali mkalimani awe ameketi. Wazee watiwa moyo wawasiliane na ndugu mkomavu aliye kiziwi, ikiwa yawezekana, ili kupata madokezo hususa juu ya mipango ifaayo ya kuketi.
5 Ikiwa mkalimani astahiliye anayetumikia akiwa mzee au mtumishi wa huduma apatikana, na idadi ya ndugu na dada viziwi yafanya ihitajiwe, wazee waweza kuamua kwamba mikutano fulani yote-yote ifanywe katika lugha ya ishara. Funzo la Kitabu la Kutaniko laweza kuwa mkutano wa kwanza wa kila juma unaopangwa kwa njia hiyo. Kama kutaniko lingependa kuwa na mikutano yoyote kati ya ile mingine mitano ya kila juma katika lugha ya ishara (au lugha nyingineyo isipokuwa lugha ya kutaniko hilo), wazee wapaswa kujulisha Sosaiti juu ya tamaa yao. Yaonekana kwamba Lugha ya Ishara ya Amerika ndiyo lugha ifundishwayo na kueleweka katika maeneo mengi katika shamba letu.
6 Ingawa mawasiliano kati ya viziwi na watu wanaosikia huenda yakahitaji jitihada za pekee kwa upande wa vikundi vyote viwili, washiriki wote wa kutaniko wapaswa wajitahidi kufahamiana ili kuwepo badilishano la kitia-moyo la kweli. (Ebr. 10:24) Roho hiyo miongoni mwa ndugu itafanya wapya wote wahisi wamekaribishwa.