Upanuzi Wenye Kuendelea Waongeza Uhitaji wa Majumba ya Ufalme
1 Zamani za kale nabii wa Yehova alitabiri kwamba “vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja.” (Hag. 2:7) Kwa hakika tunaona uthibitisho wa jinsi ufundishaji wa kimungu unavyowawezesha wengi sana wajifunze kweli na kuwa waabudu wa Yehova. Yasisimua kama nini kuona kwamba watu 2,735 walibatizwa katika mwaka wa utumishi wa 1993 katika Afrika Mashariki! Ili kuendelea kusaidia wapya hao wote, twahitaji ‘kuzitafakari njia zetu’ ili kuhakikisha kwamba tunaitegemeza kazi ya Mungu kadiri iliyo kamili zaidi sana iwezekanavyo. (Linganisha Hagai 1:5.) Ndiyo, sehemu ya maana ya kutegemeza kwetu kazi ya Mungu yaendelea kuwa kule kusaidia kwetu kuandaa nyumba zifaazo za ibada kwa ajili ya umati mkubwa wa wasifaji wapya wa Yehova.
2 Sosaiti imeendelea kuandalia makutaniko fedha za kupata Majumba ya Ufalme mapya. Katika mwaka wa utumishi wa 1993, makutaniko 14 katika nchi 4 yalipokea mikopo kwa ajili ya miradi yao ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Jambo lipendezalo kwelikweli ni bidii na azimio la ndugu katika nchi zote la kupata ploti na kujenga Majumba ya Ufalme. Fedha ambazo zimekopeshwa makutaniko zinarudishwa kwenye hazina pamoja na riba ambayo imepatikana hivi kwamba fedha zote ambazo zimetolewa zikiwa upaji zaendelea kutumiwa, mwaka baada ya mwaka, ili kujenga Majumba ya Ufalme mapya.
3 Msaada Kutoka Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa: Twafurahi kutangaza kufanyizwa kwa Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa ya kwanza katika eneo letu hapa Nairobi. Mipango imeanza tayari ya kufanyiza Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa katika Mombasa, Magharibi mwa Kenya, Addis Ababa, na Kigali. Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa zitawasaidia wazee wanaohusika katika utendaji mbalimbali wa ujenzi kuhusiana na Majumba ya Ufalme mapya na miradi ya kutengeneza upya majengo. Zitasaidia kukadiri uhitaji wa Jumba la Ufalme jipya au mradi wa kutengeneza upya jengo fulani na kuandaa msaada wa nje kama uhitajiwavyo tangu wakati kabla ya ploti kupatikana hadi wakati Jumba la Ufalme linapokamilishwa. Kila kutaniko katika maeneo yaliyotajwa juu yatagawiwa mojayapo halmashauri hizo.
4 Katika nchi nyinginezo maelfu ya wafanyakazi wamejitolea kwa hiari kushiriki katika programu ya Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa. Wenye kujitolea hao, kutia ndani wengi wenye ustadi na mafundi wengi, hutoa kwa hiari wakati na jitihada zao katika mambo kama vile kununua ploti, kuweka rekodi ya hati za kisheria, kupanga ujenzi, na kufanyiza orodha za vifaa za kununuliwa. Wao husaidia pia kununua vifaa vya hali ya juu kwa bei nafuu, kumaliza kazi ya kwanza ya kutayarisha mahali pa ujenzi, na kusimamia ujenzi halisi. Twatarajia kuona utoaji uo huo wenye ukarimu wa watu waliojitolea kwa niaba ya masilahi ya Ufalme katika shamba letu. Hilo lastahili pongezi sana na laleta baraka nyingi kutoka kwa Yehova.—Mit. 11:25.
5 Wazee wapaswa kuwasiliana na Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa ya eneo lao wakati kutaniko lao lianzapo kwa mara ya kwanza kufikiria kutengeneza upya Jumba la Ufalme lililoko au ujenzi wa Jumba la Ufalme jipya. Kwa nini? Halmashauri za kimkoa zitakuwa na miongozo iwezayo kusaidia makutaniko katika yale wanayofikiria mwanzoni. Kuteua mahali au kufuatia mahali ambapo pamegawiwa huhusisha mambo mengi. Mambo mengine yangeweza kuongeza sana bei halisi ya ploti na ya ujenzi, kama vile kazi nyingi ya kutayarisha mahali, kuondoa vitu hatari au vyenye sumu, au matatizo ya kisheria. Ikiwa kutaniko lahitaji msaada wa kifedha kutoka kwa Sosaiti, halmashauri za kimkoa zaweza kusaidia wazee wa kutaniko wakadiri mahitaji yao ifaavyo na kutolea Sosaiti ombi la mkopo wa ujenzi.
6 Halmashauri za Ujenzi za Kimkoa zitakuwa zimedokeza plani mbalimbali za Majumba ya Ufalme. Kabla ya kuteua namna fulani ya jengo, wazee wa kutaniko wapaswa kuwasiliana na halmashauri ya kimkoa na kuzungumzia sura ya ujumla ya jengo hilo, wakitumia plani zilizoandaliwa na Sosaiti zikiwa mwongozo. Hilo halitapunguza tu gharama za ujenzi bali pia litasaidia kutaniko lichague jengo litakalokuwa la kiasi na bado liwezalo kutumiwa na ambalo litafaa njia ya ujenzi wa haraka.
7 Ni lazima rekodi za kifedha zilizo sahihi na zenye kutia mambo yote ndani ziwekwe. Ndugu wenye ujuzi watafanya kazi pamoja na halmashauri za kimkoa ili kusaidia makutaniko yawe na mfumo wa kuweka hesabu unaohitajiwa na kuudumisha muda wote wa mradi wa ujenzi. Hilo litasaidia sana, kwa kuwa kwa kawaida wazee wa mahali hawafanyi kazi ya kuendelea na rekodi hizo za kifedha za Majumba ya Ufalme. Mwisho wa mradi huo wa ujenzi, halmashauri ya kimkoa yapaswa ipokee nakala iliyokamilishwa ya rekodi za hesabu zilizowekwa kwa ajili ya mradi huo wa ujenzi.
8 Wenye Kujitolea Wahitajiwa: Halmashauri za kimkoa hujaribu kutumia stadi zinazopatikana ndani ya makutaniko ambayo yatakutana katika Majumba ya Ufalme mapya au yale yanayotengenezwa upya. Wao pia hufanya kazi pamoja na ndugu wa mahali, hasa wazee na watumishi wa huduma, ili kuwazoeza katika kufanya kazi zilizopo. Wakiwa wamekuza stadi zitakazotumika katika ujenzi wa Jumba la Ufalme, ndugu hao waliokomaa kiroho waweza kusaidia baadaye na miradi mingine ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme iliyoratibiwa katika mkoa huo. Hivyo, wale wanaoshirikiana na makutaniko yanayohusika katika mradi fulani wa ujenzi wa Jumba la Ufalme wanahitaji kuonyesha roho ya kujitolea kwa hiari na ya ushirikiano, bila kutazamia kwamba halmashauri ya kimkoa na wale wafanyao kazi nayo ndio watashughulikia kazi yote ya Jumba la Ufalme lao. (Neh. 4:6b) Baada ya kupokea mazoezi, ndugu wapaswa kuchochewa na upendo ili kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme kwa ajili ya makutaniko mengine yanayohitaji sana majengo mapya au kuboreshwa.—Neh. 5:19; Flp. 2:3, 4.
9 Wahubiri waliobatizwa ambao wana stadi zifaazo na ambao wana msimamo mzuri kutanikoni wanatiwa moyo wajitolee kusaidia na mgawo huo mkubwa sana wa kazi. Stadi za ujenzi na pia zisizo za ujenzi zahitajiwa. Wenye kujitolea waweza kujulisha tamaa zao kwa mwangalizi-msimamizi au mwandishi ambaye atapeleka pendekezo la baraza la wazee kwa halmashauri ya kimkoa. Wenye kujitolea wapaswa waonyeshe maarifa yao wakiwa mafundi au katika sehemu nyingineyo, kama vile utumishi wa chakula, usalama, kushughulikia vifaa, kutunza hesabu, na kufanyia kazi hati za kisheria. Kuitikia katika njia hiyo ni uthibitisho wa upendo wetu kuelekea majirani wetu wa karibu zaidi—ndugu zetu Wakristo.—Mt. 7:12; 22:39; Yn. 13:35.
10 Msaada wa Kujitolea Wathaminiwa: Kabla ya kuhusika katika mradi wa ujenzi wa Jumba la Ufalme, ni wachache wanaotambua jinsi ilivyo kazi kubwa kukamilisha mradi wa jinsi hiyo. Baada ya mradi mmoja wa ujenzi wa Jumba la Ufalme kumalizwa, wazee waliandika hivi: “Mwelekezo wenye saburi uliopokewa kutoka kwa ndugu wa Halmashauri ya Ujenzi ya Kimkoa ulikuwa baraka kubwa kwetu. Tufikiriapo utegemezo waliotupa sisi kupitia mwelekezo na pia kuratibu wafanyakazi wenye stadi, twalazimika kukumbuka 1 Petro 5:2, 3, ambapo twasoma juu ya kuchunga ‘si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo; wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.’ Kwa kweli ndugu hao walikuwa vielelezo vyema vya utumishi wenye kujitolea kwa Yehova. Muda wote wa mradi huo, kulikuwa na pindi nyingi mno zisiweze kuhesabiwa, ambazo ndugu walisafiri kutoka sehemu za mbali, walitumia muda mrefu wa saa, walitoa mashine na vyombo vyao viweze kutumiwa, na hata kutoa upaji wa vifaa, ili kutusaidia katika ujenzi wa Jumba la Ufalme letu jipya. Ukarimu wa ndugu hao ni wonyesho mtukufu kwamba wana ‘upendo kwa ajili ya ushirika mzima wa ndugu’ na hicho kimekuwa kitia-moyo kama nini kwetu!—1 Petro 2:17, NW.”
11 Michango ya Kifedha Yaendelea Kusaidia: Michango yenye ukarimu imesaidia makutaniko katika wakati uliopita yapate ploti na kulipia mikopo kwa uaminifu na tuna hakika kwamba hilo litaendelea katika wakati ujao. Je! Yehova Mungu mwenyewe haongozi katika kutoa bila ubinafsi? (Yak. 1:17) Ingawa ni kweli kwamba uwezo na fursa zetu mbalimbali za kutoa hutofautiana, huenda tukaona kwamba kwa kurekebisha matumizi yetu ya kibinafsi, twaweza kushiriki kikamili katika kutegemeza kazi ya ujenzi. Kwa hakika ukarimu huo huuletea moyo wa Yehova shangwe, pamoja na kitia-moyo kikubwa kwa ndugu zetu.
12 “Umati mkubwa” unaitikia ujumbe wa Ufalme leo, kwa wingi zaidi. “Vitu vinavyotamanika” vinamiminika ndani ya hekalu la Yehova la kiroho, naye ‘anaijaza nyumba yake utukufu.’ (Ufu. 7:9; Hag. 2:7, NW) Kama vile Wayahudi waaminifu wa wakati wa Hagai, na tukaze mioyo yetu juu ya kazi ya Mungu, tukitegemeza kikamili ule uhitaji mkubwa wa Majumba ya Ufalme zaidi. Hata ingawa maelfu mengi ya Majumba ya Ufalme mazuri yamejengwa katika miaka ya karibuni, ukuzi waendelea kwa mwendo ulioongezeka. Utegemezo wetu wenye kuendelea wa miradi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme ni njia bora kabisa ya kushiriki katika kazi ya Mungu.