“Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1994
1 Watu wenye imani wameonyesha “hofu ya kimungu” kuanzia wakati wa Abeli na wa Noa mpaka sasa. (Ebr. 11:4, 7, NW) Kufanya matendo ya hofu ya kimungu kwamaanisha kuonyesha “kicho na staha ya kina kirefu kwa Muumba na mtetemo ufaao wa kutomchukiza.” (it-1-E uku. 818) Mwaka huu tutaonyesha staha hiyo ya kina kirefu kwa kuhudhuria kwetu “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya. Je! utakuwako kufurahia programu nzima, kuanzia wimbo wa kufungua mpaka sala ya mwisho?
2 Kila mwaka sisi hufika kwenye mkusanyiko wa wilaya tukiwa na tazamio la hamu nyingi. Ingawa huenda jitihada na gharama kubwa ya kibinafsi ikahusika, baraka nyingi hupokewa. Sisi hurudi nyumbani kwa kushangilia, tukiwa tumeridhika na kujengwa kiroho. (Linganisha 1 Wafalme 8:66.) Ushirika huwa wa kuchochea, na mkusanyiko huandaa badiliko kutoka yale maisha ya kawaida. Lakini kumbuka, sisi hukusanyika kumwabudu Yehova. Yeye hutuamuru tufanye hivyo. Anatufundisha jinsi ya kujinufaisha.—Kum. 31:12, 13; Zab. 122:1.
3 Mkusanyiko wa Siku Tatu: Programu itatolewa kwenye mikusanyiko 15 katika Afrika Mashariki. Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1994 imeandaa orodha ya mahali mbalimbali. Zaidi ya kuwa katika Kiingereza, mikusanyiko itafanywa katika Kiamhara, Kinyarwanda, Luganda, Kiswahili, Kitigrinya na Lugha ya Ishara ya Kiamerika. Programu kamili katika Lugha ya Ishara ya Kiamerika itatolewa katika Mombasa. Pia, programu kamili katika Luganda itatolewa Kampala, lakini hakutakuwa na tafsiri ya lugha ya Luganda kwenye mikusanyiko mingine yoyote.
4 Programu itaanza Ijumaa saa 4:20 asubuhi na kumalizika Jumapili karibu saa 10:15 alasiri. Jumamosi na Jumapili, programu itaanza saa 3:30 asubuhi. Milango itafunguliwa saa 1:30 asubuhi. Ni wale tu wenye migawo hususa ya kazi watakaoruhusiwa kuingia mapema kidogo.
5 Staha ya Kina Kirefu kwa Yehova Hutushurutisha Kuhudhuria: Paulo aliwashauri Wakristo Waebrania kwamba “[wa]mtolee Mungu ibada [“utumishi mtakatifu,” NW] ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu [“hofu ya kimungu,” NW] na kicho.” (Ebr. 12:28) Mkusanyiko wetu wa wilaya mwaka huu umetayarishwa ili kutusaidia kufanya lilohilo. Huenda vipingamizi fulani vikakabiliwa vyenye kutahini azimio letu la kuhudhuria. Huenda vikaonekana kama milima, lakini vyaweza kushindwa kwa msaada wa Yehova. (Mt. 17:20) Ikiwa huwezi kuratibu likizo lako kuhusisha mkusanyiko mzima, asubuhi ya Ijumaa mpaka alasiri ya Jumapili, je, umemfikia mwajiri wako kwa sala kuomba kwamba usiwe kazini wakati huo? (Yak. 1:6-8) Wazazi wapaswa kusaidia watoto wao wenye umri wa kwenda shule watakaokuwa wakihudhuria mmoja wa mikusanyiko masomo yakiwa yangali yaendelea kuwajulisha walimu wao kwa staha kwamba hawatakuwa shuleni Ijumaa kwa sababu ya sehemu hii ya maana ya ibada yao ya kidini.
6 Tumia kwa Faida Mapato Hayo Yenye Thamani: Ni mapato gani hayo yenye thamani? Wakati na jitihada iliyotumiwa ili kuhudhuria mkusanyiko. Kungekuwa kukosa hekima kufanya mipango ya uangalifu ili kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya wa na kumbe urudi nyumbani jioni ya Jumapili ukiwa umekosa sehemu kubwa ya programu. Je! ungetoa udhuru uondoke kwenye sherehe ya karamu ikiisha kupamba moto eti ukashughulikie mambo mengine? Kwa hiyo, ukomavu wetu wa kiroho na hofu ya kimungu hazipasi kuturuhusu kukosa lolote la yale ambayo Yehova ametutayarishia.—Linganisha 1 Wakorintho 2:9, 10.
7 Labda hatungefikiria kuondoka mapema. Hata hivyo, tungeweza bado kukosa sehemu kubwa ya programu. Hilo lingeweza kutendekaje? Ni kwa kutopanga mapema tuhakikishe kwamba twapokea manufaa ya upeo kutokana na sehemu zenye kutolewa. Twataka kuhakikisha kuianza siku mapema vya kutosha ili tupate kifungua-kinywa cha kutosha na kushughulikia mambo mengine ya lazima ili tuweze kuwa katika viti vyetu kabla programu haijaanza. Kupata usingizi mzuri wa usiku ni kwa maana pia kuhakikisha kwamba tutakuwa macho na kuweza kuweka fikira juu ya programu ya siku nzima.
8 Njia iliyothibitishwa ya kuvuna manufaa nyingi zaidi kutokana na programu ni kuandika mambo ya kiasi. Ni jambo la maana kwamba vijana pia waandike mambo sawasawa tu na vile ilivyo kwa watu wazima. Mhubiri mwenye umri wa miaka 16 asema hivi: “Mimi huandika maandiko yatajwayo wakati wa hotuba. Halafu naweza kuipitia hotuba nyumbani.” Kijana mwingine mwenye umri wa miaka 16, aongezea hivi: “Mimi huandika mawazo makuu. Hiyo hufanya akili yangu isitangetange.” Kwa kawaida vitu ambavyo wavihitaji kwelikweli kwa ajili ya programu ni Biblia, kitabu cha nyimbo, kitabu cha kuandikia chenye ukubwa wa kiasi, na kalamu ya wino au penseli. Bila shaka, wazazi wenye watoto wadogo ni lazima wawatimizie mahitaji yao, lakini ni afadhali kutojitatiza wenyewe na wengine kwa vitu vingi mno vya kibinafsi.
9 Ndugu wengine hurekodi programu, wakitumia rekoda-audiokaseti au kamera-video, ili wakarudie programu nyumbani. Kufanya hivyo ni jambo la kibinafsi, lakini wengine wameona kwamba wakiisha kurudia kawaida yao ya maisha, wakati wa kurudia yaliyorekodiwa huwa mchache. Kwa kuongezea, mambo fulani makuu katika hotuba huenda yakapita wakati wa kurekebisha kifaa cha kurekodi.
10 Twapaswa kufanya jitihada ya moyo mweupe kuwa katika viti vyetu kabla programu haijaanza. Ingawa huenda tukawa katikati ya kuelezana maono ya kufurahisha pamoja na marafiki wa zamani wakati mwenyekiti atangazapo kwamba programu yakaribia kuanza, sisi huonyesha staha kwa wale walio katika programu, na kwa ndugu zetu kwa ujumla, tukiacha upesi mazungumzo yetu na kuketi.
11 Mikusanyiko ya wilaya sikuzote huwa ni pindi zenye shangwe kwa sababu ya baraka tele za Yehova. Sisi hupokea manufaa za kiroho na kimwili pia. Ni lazima ikumbukwe kwamba gharama kubwa zahusika katika kukodi mahali pa mkusanyiko. Pia gharama za vyakula zimepanda, na Sosaiti hununua chakula cha hali nzuri cha ugawaji kwenye kila mkusanyiko. Gharama hizo na nyinginezo hulipiwaje? Ni kupitia upaji wetu wa kujitolea, uwe ni kwa fedha taslimu au kwa hundi ziandikwazo ili zilipwe kwa “Mashahidi wa Yehova.” Hiyo yapatana na roho ya Zaburi 96:8, The Old Testament in Swahili (Mombasa), ambalo latutia moyo ‘tumpe Jehova utukufu na kutwaa tunu tuje nayo kuingia nyuani mwake.’
12 Je! Mwenendo Wako Utaleta Sifa? Kila mwaka toleo la Oktoba la Huduma ya Ufalme Yetu hutukumbusha kwa fadhili umaana wa mwenendo mwema tunapohudhuria mkusanyiko wa wilaya. Bila shaka, mwenendo wetu wapasa sikuzote kuwa kielelezo chema, lakini tuwapo tumekusanyika katika idadi kubwa, kwa kawaida sisi huchunguzwa kwa makini zaidi na wale walio nje ya ile kweli. Mwenendo wetu, uwe mwema au mbaya, huenda ukasema kwa sauti kubwa kuliko kuhubiri kwetu. Sisi twataka Yehova asifiwe kwa yale tusemayo na kutenda.—Mit. 27:2; 1 Pet. 2:12.
13 Baada ya “Ufundishaji wa Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka uliopita, mlinda-usalama mahali pamoja alisema: “Hivi ndivyo vitoto vizuri zaidi ambavyo nimepata kuvichunga kwa muda mrefu.” Halafu, baada ya kueleza juu ya tabia mbaya na uharabu wa vikundi vingine vya vijana, aliongezea hivi juu ya watoto Mashahidi: “Wao hujiendesha vizuri na ni furaha kuwa pamoja nao. Laiti mikusanyiko mingine ifanywayo hapa ingekuwa kama huu.”
14 Mwandishi wa safu za magazeti akiandika katika gazeti moja alitoa maoni haya juu ya mkusanyiko: “Wanawake na wasichana walivalia mavazi mazuri, na wanaume na wavulana walivalia koti na tai. Waliandika mambo kwa bidii huku wakisikiliza wasemaji muda wa siku nne. Na ikiwa usafi ni wa pili kwa umungu, basi, Mashahidi wa Yehova wamewekea kanuni hiyo kiwango kipya.” Ingawa hivyo, si ripoti zote zimekuwa nzuri.
15 Wazazi wapaswa kuangalia watoto wao ifaavyo ili kuzuia upitapitaji wa huku na huku katika vijia vya majengo ambao hufanyiza kelele nyingi mno zenye kuwavuruga wale wanaojaribu kusikiliza. Wachache wana mambo ya lazima ya kushughulikia wakati wa programu, lakini je, haitupasi sisi wengine kuwa katika viti vyetu, tukisikiliza kwa makini?
16 Wazazi walio wengi ni thabiti kwa watoto wao juu ya kuhudhuria mikutano ya kutaniko kila juma. Je! hawapaswi kuwa thabiti kadiri hiyohiyo kuhakikisha kwamba watoto wao wameketi karibu nao na hawatangitangi katika vijia vya majengo wakati wa programu? Mahali pa mkusanyiko hugeuzwa kuwa Jumba la Ufalme lililo kubwa, lakini huu ni mfumo wa Shetani, na ingekuwa rahisi watu wasio na kanuni kuingia katika jengo wakiwa na makusudio yasiyofaa. WAHITAJI KUJUA MAHALI WATOTO WAKO WALIPO NA LILE WAFANYALO NYAKATI ZOTE.
17 Mavazi na Kujipamba: Twaishi katika muhula ambamo yakubalika kuwa na sura ya hivihivi tu, hata ya kizembe. Watu wengi huhudhuria kanisa na sherehe za vitumbuizo au mikahawa wakiwa wamevalia hivihivi mno. Maoni yaliyonukuliwa katika mafungu 13 na 14 yaonyesha kwamba kuna wale ambao wangali wakivutiwa na mavazi ya kujiheshimu, hususa kuhusiana na ibada rasmi. Mavazi ya kizembe, ya hivihivi tu na kujipamba kusikofaa hueleza mengi juu yetu. Usisahau kamwe kwamba jengo la mkusanyiko si uwanja wa michezo tena. Ni Jumba la Ufalme lililopanuliwa. Wengine huvalia kwa staha kwa ajili ya mkusanyiko lakini baada ya vipindi huenda kwingineko wakiwa wamevalia isivyofaa au kwa njia isiyo ya kiasi.
18 Wataka-kubatizwa wahitaji kukumbushwa kwamba mavazi fulani ya kuogelea hayaifai pindi hiyo. Mavazi yapasa kuwa ya kiasi na yenye kupendeza. Nani apaswa kuamua hilo? Wazee wana daraka la kuhakikisha kwamba yeyote anayebatizwa kutoka kutaniko lao hatoi kisababishi chochote cha kukwaza. (2 Kor. 6:3, 4) Hiyo ingeondolea mbali mavazi ya kuogelea yanayofunua uchi au nguo zisizobaki zikiwa za kiasi zikishikwa na maji na T-shati zenye shime au matangazo ya kilimwengu. Ingefaa wazee wazungumzie jambo hilo na mtaka-kubatizwa wanapopitia yale maswali katika kitabu Huduma Yetu.
19 Vifaa vya Kurekodi: Kama ilivyotaarifiwa mapema kidogo, kutumia vifaa vya kurekodi, na hususa rekoda-videokaseti, ni uamuzi wa kibinafsi. Ikiwa wowote waamua kurekodi, yawapasa tafadhali wawafikirie wale walio karibu nao. Huenda ikakengeusha fikira hata wakati kurekodi kunapofanywa mtu akiwa kwenye kiti chake. Hakuna mtu apaswaye kuzuia wakusanyikaji wenzake wasione wakati anaponasa mambo katika utepe. Zaidi ya hilo, hakuna vifaa vya kurekodi vya namna yoyote vipaswavyo kuunganishwa na mifumo ya nguvu za umeme au ya sauti, wala havipasi kuzuia vijia au vipito.
20 Kuketi: Matatizo yashirikishwayo na kuweka akiba ya viti yangali yahitaji kuangaliwa. Tungependa tena kukumbusha kila mmoja hivi: VITI VYAWEZA KUWEKWA AKIBA KWA AJILI YA WASHIRIKA WA FAMILIA YAKO YA KARIBU TU NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WAKISAFIRI NAWE KATIKA GARI LAKO. Kwenye mikusanyiko fulani milango ilipofunguliwa saa 1:30 kila asubuhi, kulikuwa na kukurukakara huku ndugu na dada wakiingia jengoni. Wengi walikuwa wakihifadhi karibu sehemu nzima-nzima, kisha vingi vya viti walivyohifadhi vikabaki bila kukaliwa.” Mazoea hayo ya kutofikiria wengine yaonekana yangali yapo ijapokuwa vikumbusha hutolewa kwa ukawaida. Je! hatupaswi kupekua mioyo yetu katika jambo hilo na kuzitafakari kanuni zilizo katika Wafilipi 2:3, 4?
21 Kila mkusanyiko watiwa moyo ufanye maandalizi kwa ajili ya wale wenye mahitaji maalumu, kama wazee-wazee na wasiojiweza kimwili. Tafadhali hakikisha kwamba hamkalii viti vilivyo katika sehemu zilizowekwa akiba kwa ajili ya ndugu na dada hao ikiwa hamstahili. Pia mwe macho kusaidia wale walio na mahitaji maalumu wapate kiti ikiwa hawakuandamana na mtu mwenye daraka la kuwatunza.
22 Fasihi na Utumishi wa Chakula: Tukusanyikapo kwa ajili ya mkusanyiko wa wilaya, sisi hufurahia utele wa chakula cha kimwili na cha kiroho. Vyote viwili vyapasa kupokewa kwa shukrani, bila kutapanya chochote. (2 Nya. 31:10; Mit. 3:10; Yn. 6:12) Kama wakati uliopita, twadokeza kwamba mpate tikiti za chakula mapema. Mwaweza kuanza sasa kupanga kuweka akiba ya fedha kwa ajili ya fasihi. Tafadhali onyesheni hangaiko lenye upendo kwa wengine mwapo kwenye mistari ya chakula na fasihi.
23 Katika Novemba 4, 1994, wa kwanza wa “Hofu ya Kimungu” Mikusanyiko ya Wiaya utaanza. Je! umekamilisha matayarisho yako, na je! sasa uko tayari kufurahia siku tatu za ushirika wenye furaha na mambo mema ya kiroho? Sala yetu ya moyo mweupe ni kwamba Yehova abariki jitihada zako ili ukusanyike na kulishwa kwenye meza ya Yehova ya mambo mema kwenye “Hofu ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Vikumbusha vya Mkusanyiko wa Wilaya
Ubatizo: Wataka-kubatizwa wapaswa wawe katika viti vyao katika sehemu iliyoonyeshwa kabla ya programu kuanza asubuhi ya Jumamosi. Mavazi ya kuogelea yaliyo ya kiasi na nguo ambazo hubaki zikiwa za kiasi zishikapo maji na taulo yapasa kuletwa na kila mmoja apangaye kubatizwa. Baada ya hotuba ya ubatizo na sala kutolewa na msemaji, mwenyekiti wa kipindi atatoa maagizo mafupi kwa wataka-kubatizwa halafu aitishe wimbo. Baada ya ubeti wa mwisho, wakaribishaji wataelekeza wataka-kubatizwa kwenye mahali pa uzamisho. Kwa kuwa ubatizo ambao ni ufananisho wa wakfu wa mtu ni jambo la uhusiano wa kindani na la kibinafsi kati ya mtu na Yehova, hakuna uandalizi wa yale yaitwayo mabatizo ya ushirika ambamo wataka-kubatizwa wawili au zaidi hukumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.
Kadi za Beji: Tafadhali vaa beji ya 1994 kwenye mkusanyiko na unaposafiri kwenda na kutoka mahali pa mkusanyiko. Mara nyingi hiyo hufanya iwezekane tutoe ushahidi mzuri tunaposafiri. Ilikuwa hivyo kwa njia ya kutokeza mwaka uliopita kwa habari ya mikusanyiko iliyofanywa katika Nairobi na Addis Ababa. Kadi za beji na vishikio zapasa kupatikana kupitia kutaniko lenu, kwa maana hazitapatikana kwenye mkusanyiko. Kumbuka kuja ukiwa na kadi yako ya karibuni ya Mwelekezo wa Kitiba.
Kitambulisho cha Mapainia: Mapainia wote wa kawaida na wa pekee, na waangalizi wasafirio pia watahitaji kuleta kadi yao ya Kitambulisho na Mgawo kwenye mkusanyiko. Mapainia ambao watakuwa wamekuwa kwenye orodha kwa miezi sita tangu waanze upainia wakati wa mkusanyiko wa wilaya wanaouhudhuria wanaweza kupokea tikiti za chakula za mkusanyiki wakionyesha Kitambulisho chao kwenye mkusanyiko mmoja tu. Hivyo, tunza kadi hiyo kwa uangalifu kama vile ungetunza pesa. Huwezi kupata nyingine kwenye mkusanyiko. Vichapo vyovyote vitakavyotolewa kama zawadi au vingine kwa bei ya painia vitapatikana kwa mapainia katika chumba cha vitabu, kwa kuonyesha tu Kitambulisho chao. Wale walio katika utumishi wa Betheli wanaweza kupokea maandalizi yayo hayo kwa kuonyesha Kitambulisho chao cha Betheli.
Utumishi wa Kujitolea: Je! waweza kuweka kando wakati fulani kwenye mkusanyiko usaidie katika idara mojapo? Kutumikia ndugu zetu, hata ikiwa ni kwa muda wa saa chache tu, kwaweza kusaidia sana na kuleta uradhi wa kadiri nzuri. Ikiwa waweza kusaidia, tafadhali piga ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kwenye mkusanyiko. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 waweza pia kutoa mchango mzuri kwa kufanya kazi chini ya mwelekezo wa mzazi au mtu mzima mwingine mwenye kujali daraka.
Maneno ya Tahadhari: Kwa kukaa macho kuhusu matatizo yawezayo kutokea, twaweza kujiepusha na ugumu usio wa lazima. Mara nyingi wevi na watu wengine wasiofuata kanuni watanyemelea watu walio mbali na mazingira yao ya nyumbani. Hakikisha gari lako limefungwa kwa ufunguo nyakati zote, na usiache chochote kikiwa chaonekana kushawishi mtu fulani avunje. Wevi na wadokoa-mifuko huzoa madonge makubwa kwenye makusanyano makubwa. Halingekuwa jambo la hekima kuacha vitu vyovyote vya thamani kwenye kiti chako. Huwezi kuwa na uhakika kwamba kila mtu aliyekuzunguka ni Mkristo. Mbona utoe kishawishi chochote? Ripoti zimepokewa za majaribio yaliyofanywa na watu fulani wa nje kushawishi watoto waende pamoja nao. WEKA WATOTO WAKO MAHALI UWEZAPO KUWAONA NYAKATI ZOTE.
Uangalifu wapasa kutumiwa pia ili kuepuka kujaza mno magari ya kukodiwa na kutaniko kwa kusafiri mkusanyikoni. Ni vizuri zaidi kupanga kutumia fedha zaidi za gharama za usafiri kuliko kuvunja sheria za Kaisari au hata kufanya vibaya zaidi kwa kuweka akina ndugu kwenye hatari na uwezekano wa kupatwa na aksidenti na uwezekano wa kupoteza uhai kwa sababu ya kujaza gari mno au kumtia moyo dreva aende kasi zaidi ili mfike mwendako mapema zaidi. (Rum. 13:1-7; Kum. 21:1-9) Ndugu wenye madaraka wanaosafiri katika magari hayo wapaswa kuhisi wakiwa huru kutoa shauri lenye upendo kwa habari hii ikiwa lazima.