Jiendesheni kwa Namna Yenye Kustahiki Habari Njema
1 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, twataka kuletea jina la Yehova heshima. Twajua kwamba mwenendo wetu, usemi wetu, kujipamba kwetu, na mavazi yetu yaweza kuwa na uvutano juu ya jinsi wengine wanavyoiona ibada ya kweli. Hilo ni kweli hasa tunapokuwa kwenye mikutano yetu. Twataka kuhakikisha kwamba kila jambo linalosemwa na kufanywa kwenye mikutano lastahiki habari njema na lamletea Yehova heshima.—Flp. 2:4.
2 Viwango vingi vya ulimwengu vya mavazi na kujipamba havikubaliki kwa Wakristo. Hili ni jambo lipaswalo kupewa uangalifu sana na wahudumu wa habari njema. Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1989, ukurasa 20, lilisema hivi: “Nguo zetu hazihitaji kuwa za bei kubwa, lakini zinapasa kuwa safi, za kupendeza, na zenye kiasi. Viatu vyetu vinapasa kutengenezwa vyema katika sehemu vilikoharibika na viwe vyenye sura njema. Vivyo hivyo, kwenye mikutano yote, kutia na Funzo la Kitabu la [Kutaniko], miili yetu inapasa kuwa safi, na tunapaswa kuwa maridadi na kuvalia ifaavyo.”
3 Kuwahi ni alama ya ufikirio na uangalifu wenye upendo. Pindi kwa pindi, hali zisizoepukika huenda zikatuzuia tusiwasili kwa wakati kwenye mkutano. Lakini kuchelewa kwa kawaida kwaweza kuonyesha ukosefu wa staha kwa kusudi takatifu la mikutano na kushindwa kuthamini daraka letu la kuepuka kusumbua wengine. Wale wenye kuchelewa-chelewa mara nyingi hukengeusha wengine fikira na kuwazuia wasinufaike kikamili na programu. Kuwahi huonyesha staha kwa hisia na masilahi ya wote wanaohudhuria.
4 Upendo kwa majirani wetu wapaswa utufanye tuwe waangalifu kuepuka kusababisha vikengeusha-fikira wakati wa mikutano. Kunong’ona, kula, kutafuna peremende, kufanya makelele na karatasi, na kufanya ziara zisizohitajika za kwenda msalani, kwaweza kuvuruga fikira za wengine na kupunguza heshima ipasayo mahali pa ibada pa Yehova. Haifai kwa yeyote kufanya shughuli za kutaniko wala kuzungumza na wengine isipokuwa kuna hali fulani ya dharura inayotaka akina ndugu waondoke vitini mwao. Ama sivyo, wote wapaswa wawe wameketi na kusikiliza programu ili kujinufaisha wenyewe na familia zao. Adabu mbaya hazifai katika Jumba la Ufalme kwa sababu “upendo . . . haukosi kuwa na adabu.”—1 Kor. 13:4, 5; Gal. 6:10.
5 Mwenendo mwema wa watoto wetu kwenye mikutano pia huleta sifa na heshima kwa jina la Yehova. Usimamizi wa uangalifu kutoka kwa wazazi ni muhimu. Watoto wapaswa watiwe moyo kusikiliza na kushiriki. Wazazi wengi walio na watoto wachanga huchagua kuketi mahali ambapo wao waweza kutoka kwa urahisi na kushughulikia mahitaji ya wachanga wao bila kukengeusha wengine fikira mno.
6 Paulo alionya hivi kwa upole: “Jiendesheni kwa namna yenye kustahiki habari njema.” (Flp. 1:27, NW) Acheni basi, tujitahidi kuwa wenye adabu na wenye ufikirio kwa wengine tunapohudhuria mikutano. Ushirikiano wa wote utahakikisha kwamba kutakuwa na “badilishano la kitia-moyo . . . kwa kila mmoja kupitia imani ya mwingine.”—Rum. 1:12, NW.