Sitawisha Zoea la Kufika kwa Wakati
1. Yehova anatuwekea mfano gani kuhusu kufanya mambo kwa wakati?
1 Siku zote Yehova hufanya mambo kwa wakati. Kwa mfano, yeye huwapa watumishi wake ‘msaada kwa wakati unaofaa.’ (Ebr. 4:16) Pia, hutuandalia chakula cha kiroho “kwa wakati unaofaa.” (Mt. 24:45) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba siku yake ya ghadhabu inayokuja ‘haitachelewa.’ (Hab. 2:3) Tunafaidika sana kwa sababu Yehova hufanya mambo kwa wakati. (Zab. 70:5) Hata hivyo, kwa sababu sisi ni wanadamu wasiokamilika na wenye shughuli nyingi, huenda ikawa vigumu kufika kwa wakati. Kwa nini ni muhimu kusitawisha mazoea ya kufika kwa wakati?
2. Kwa nini kufika kwa wakati humletea Yehova sifa?
2 Kwa sababu hizi ni siku za mwisho, watu wengi wanajipenda wenyewe na hawajizuii, hivyo, inakuwa vigumu kwao kufika kwa wakati. (2 Tim. 3:1-3) Tunapofika kwa wakati kazini, kwenye ahadi tulizopanga na wengine, na kwenye mkutano, wengine huona, na jambo hilo humletea Yehova sifa. (1 Pet. 2:12) Je, kwa kawaida sisi hufika kwa wakati kwenye kazi ya kimwili, lakini mara nyingi tunachelewa kwenye utendaji wa kitheokrasi? Kufika kwa wakati katika mikutano ya Kikristo, kutia ndani kuwepo wakati wa wimbo na sala ya kufungua mkutano, kunaonyesha tuna tamaa ya kumwiga Baba yetu wa mbinguni mwenye utaratibu.—1 Kor. 14:33, 40.
3. Kwa nini tukifika kwa wakati tunaonyesha kwamba tunawajali wengine?
3 Pia, tunapofika kwa wakati tunaonyesha kwamba tunawajali wengine. (Flp. 2:3, 4) Kwa mfano, tunapofika kwa wakati kwenye mikutano ya Kikristo, kutia ndani mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani, hatutawasumbua waabudu wenzetu isivyo lazima. Kwa upande mwingine, ikiwa tuna zoea la kuchelewa, ni kana kwamba tunathamini zaidi wakati wetu kuliko wakati wao. Kufika kwa wakati kunaonyesha kwamba tunategemeka, tuna bidii, na tunaweza kutumainiwa, sifa ambazo huthaminiwa na wale wanaotuzunguka.
4. Ikiwa mara kwa mara tunachelewa, tunawezaje kurekebisha hali hiyo?
4 Ikiwa mara kwa mara unachelewa, jiulize sababu ni nini? Panga ratiba yako ukizingatia hali zako ili uweze kutimiza mambo uliyokusudia kufanya kwa wakati unaofaa. (Mhu. 3:1; Flp. 1:10) Mwombe Yehova akusaidie. (1 Yoh. 5:14) Kufika kwa wakati ni njia moja ya kuonyesha kwamba tunathamini zile amri kuu mbili za Sheria, yaani kumpenda Mungu na kumpenda jirani.—Mt. 22:37-39.