Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 6/15 kur. 26-29
  • Kuwahi na Wewe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwahi na Wewe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Iweni Waigaji wa Mungu”
  • “Kwenye Nyakati Zayo Zilizowekwa”
  • Kwa Nini Watu Fulani Huona Ni Vigumu
  • Kwa Nini Kuwahi?
  • ‘Zijue Nyakati Zilizowekwa’
  • Kwa Nini Unapaswa Kufika kwa Wakati?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Sitawisha Zoea la Kufika kwa Wakati
    Huduma Yetu ya Ufalme—2014
  • Kutunza Wakati
    Amkeni!—2016
  • Onyesha Uthamini kwa Nyumba ya Mungu
    Huduma Yetu ya Ufalme—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 6/15 kur. 26-29

Kuwahi na Wewe

MWANGALIZI Mkristo katika kundi moja la Amerika Kusini alikuwa na sifa nzuri nyingi. Lakini rafiki zake wa karibu kabisa walimwita Har–Magedoni. Kwa nini? “Twajua yeye atakuja,” wakawa wakisema, “lakini Mungu tu ndiye ajua atakuja lini!”

Ndiyo, kuwahi—au ukosefu wao—wahusu sana sifa ya mtu. Mfalme Sulemani mwenye hekima alitoa kielezi kwa njia hii: “Mainzi wafu ndio husababisha mafuta ya mfanyiza mafuta yavunde, yatoe mapovu kwa kumwagika. Ndivyo upumbavu mdogo umfanyiavyo mmoja aliye wa thamani kubwa kwa hekima na utukufu.” (Mhubiri 10:1, NW) Huenda Mkristo akawa ana sifa nzuri nyingi, lakini ataharibu uvutio wa jina lake jema asipojali wakati.

“Watu wanaowahi hunipa mimi uhakika,” akasema mwangalizi mmoja. “Wao ndio mimi hupendelea kufanya kazi nao.” Pia wao huthaminiwa katika ulimwengu wa biashara. “Fika kazini wakati ufaao; fika mikutanoni wakati ufaao; toa ripoti wakati upaswao,” chashauri kichapo Emily Post’s Etiquette. Vivyo hivyo, The New Etiquette (1987) hutaarifu kwamba, kwa ujumla, “wawasili wenye kuchelewa ni wawasili wasio na staha.” Halafu watungaji wacho wakaongezea hivi: “Pia huduma za kidini ni pindi nyingine ambapo haifai kuwasili kwa kuchelewa.”

Sisi sote huthamini wakati wengine wanapowahi. Yaonekana wazi kwamba mtume Paulo alihisi hivyo, kwa maana aliwaandikia hivi Wakristo katika Kolosai: “Nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona utaratibu wenu [mzuri, NW].” (Wakolosai 2:5) Nasi kwa uhakika twashiriki mawazo ya ndani ya Mfalme Daudi kuhusu ahadi za Yehova alipoandika hivi katika zile Zaburi: “Ee Mu-ngu wangu, usikawie [usichelewe mno, NW].”—Zaburi 40:17; 70:5.

“Iweni Waigaji wa Mungu”

Kwa kweli, Yehova hachelewi kamwe. Yeye hutokeza katika kujali kwake wakati. Hiyo yaonekana katika kazi zake zote za uumbaji. Kuanzia ulimwengu wote mzima usio na mipaka hadi kwenye vitu hai vilivyo vidogo kabisa, vyote huendesha mambo kana kwamba vyasimamiwa na saa isiyoonekana. Kwa kielelezo, namna fulani ya yungi (mmea) la baharini karibu na Japani hufungulia chembe zalo za uzazi mara moja kila mwaka katika Oktoba karibu saa tisa alasiri siku ya robo ya kwanza au ya tatu ya mbalamwezi. Katika masika yule grunioni mdogo (samaki mdogo sana) hupima wakati wa taratibu yake ya kuzalishana ili ifanyike mnamo dakika chache kabla ya maji-kujaa katika pwani ya Kalifornia.

Pia upimaji-wakati wa Yehova huwa barabara kuhusu kutimiza ahadi yake. Mathalani, kwenye Kutoka 12:41 twasoma kwamba “ilikuwa mwisho wa miaka hiyo miaka nne na thelathini, ilikuwa siku ile ile, ya kwamba majeshi yote ya BWANA [Yehova, NW] yalitoka nchi ya Misri.” Hivyo Yehova alitimiza ahadi aliyomfanyia Abramu karne nyingi mapema.—Mwanzo 15:13-16; Wagalatia 3:17.a

Yehova alituma Mwana wake, yule Mesiya, aingie ulimwenguni wakati ule ule uliotabiriwa na nabii Danieli zaidi ya karne tano mapema, hivi kwamba ‘katika wakati uliowekwa akafa kwa ajili ya watu wasiomcha Mungu.’ (Warumi 5:6; Danieli 9:25, NW) Kwa habari ya mwisho wa mfumo huu wa mambo, Biblia huonyesha kwamba Yehova ajua “siku ile na saa ile.” (Mathayo 24:36) Yeye hatachelewa. Kwa wazi, kielelezo cha Yehova katika kuwahi chastahiki kuigwa nasi.—Waefeso 5:1, NW.

“Kwenye Nyakati Zayo Zilizowekwa”

Sikuzote Yehova ametarajia watumishi wake wajali wakati, hasa kuhusu ibada yake. “Ratiba ya kila siku” ilifuatwa wakati Waisraeli walipotoa dhabihu. Yehova aliwaamuru hivi: ‘Nyinyi mwapaswa kufanya uangalifu kunitokezea matoleo yangu . . . kwenye nyakati zayo zilizowekwa.’ Pia alimpa Musa agizo hili juu ya mikutano: “Kusanyiko zima ni lazima lishike mwadi wao uliowekwa.”—Walawi 23:37; Hesabu 10:3; 28:2, NW.

Baadaye, Wayahudi waliishika “saa ya kufukiza uvumba.” (Luka 1:10) “Saa ya kusali, saa tisa,” ilishikwa na Wayahudi na wengine pia. (Matendo 3:1; 10:3, 4, 30) Na kuhusu mikutano ya Kikristo, Paulo aliandika hivi: “Mambo yote na yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.”—1 Wakorintho 14:40.

Yote haya yangalitaka nini kwa Waisraeli na Wakristo wa mapema? Kwamba wawahi katika kutimiza miadi yao iliyowekwa, hasa kuhusu ibada yao. Hakuna sababu ya kufikiri kwamba Yehova angetarajia kwa watumishi wake leo kiasi chenye kupungua hicho.

Kwa Nini Watu Fulani Huona Ni Vigumu

Maoni kuelekea wakati ni ya namna nyingi sana kutoka sehemu moja ya ulimwengu hadi nyingine. Misionari mmoja aripoti kwamba katika mji mmoja mdogo wa Amerika Kusini, nyakati fulani mke wake alikuwa ndiye mhudhuriaji wa pekee wakati yeye alipokuwa akitangaza wimbo wa kufungua mwanzoni mwa mkutano wa Kikristo. Lakini alipotangaza wimbo wa kumalizia, watu 70 wangekuwapo. Kwa upande mwingine, katika nchi moja ya Ulaya Magharibi, karibu watu elfu moja waliulizwa hivi: “Kama ungealikwa kwenye chakula saa 1:00 jioni, je! ungepaswa kuwasili dakika tano au kumi mapema, au dakika tano au kumi kwa kuchelewa, au kwa wakati barabara?” Walio wengi wakaitikia kwamba “uungwana hutaka makini nyingi sana katika kumstahi mwalikaji na kuwasili kwa dakika ile ile ipasayo.”

Hata hivyo, jambo la kuwahi ni zaidi ya upendelevu wa jimbo hili au hili. Ni tabia, sawasawa na vile kuwa safi, maridadi, au mwungwana kulivyo tabia ya kujizoeza. Bila shaka, hatuzaliwi tukiwa na tabia hizo; ni lazima tuzisitawishe. Ikiwa wewe ulifundi-shwa kuwahi ukiwa mtoto, hiyo ni baraka. Lakini wengi hutoka katika familia na malezi mlimokuwa na miadi michache iliyopangwa barabara na uhitaji kidogo wa kuratibu jitihada za mtu pamoja na jitihada za wengine. Ni baada tu ya kuwa sehemu ya kundi la Kikristo na kushiriki katika mikutano yalo na huduma ya peupe kwamba uhitaji wa kuwahi huwa jambo halisi kwao. Huenda wakaona ni vigumu kusahihisha tabia ya kuchelewa-chelewa waliyojifunza mapema maishani. Hata hivyo, upendo kwa Yehova Mungu na kwa jirani ya mtu waweza kusukuma mtu abadilike. Hata hivyo, kwa nini kufanya badiliko hilo?

Kwa Nini Kuwahi?

“Je! wewe hupenda maisha?” Benjamin Franklin akauliza hivyo wakati mmoja. “Basi usitapanye wakati, kwa maana kitu hicho ndicho maisha.” Sisi sote twatambua ukweli ulio katika taarifa hiyo. Ingawa hivyo, jambo lenye umaana sawa na hilo ni kutopoteza wakati wa wengine. “Mchelewaji,” asema misionari mmoja, “huonekana ni kama asema kwa kitendo chake, ‘Wakati wangu ni wa thamani kuliko ule wako, kwa hiyo wewe waweza kungoja mpaka mimi niwe tayari.’” Mtu asiyewahi huonekana si mkosa mpango na mkosa utegemeko tu bali mwenye kujiona pia na asiye na ufikirio kwa wengine. Wakristo wa kweli hawataki ‘kutenda neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu [udhalili wa akili, NW], kila mtu akihesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.’—Wafilipi 2:3.

Huenda watu fulani wakahisi kwamba hawapendi kuishi kwa kuongozwa na saa, kusimamiwa nayo kila hatua. Hata hivyo, kuwahi si jambo la kudhibitiwa na saa tu. Ni jambo la kuzingatia moyoni masilahi na manufaa ya watu wengine, ‘kutoangalia mambo yako mwenyewe, bali mambo ya wengine’ pia.—Wafilipi 2:4.

Kwa kielelezo, fikiria shauri hili la Biblia: “Mkaribishane ninyi kwa ninyi, kama naye Kristo alivyotukaribisha.” (Warumi 15:7) Kwa kadiri salamu halisi zihusikavyo, kwa wazi ni vigumu kufanya hivyo ikiwa mtu ana tabia ya kuchelewa kufika mikutanoni. Kwa kuwasili mapema kwa ajili ya mikutano, wewe waweza kuchangia kwa kadiri kubwa zaidi ile roho yenye upendo, urafiki na ukaribishaji ya vikusanyiko hivyo. Na kwa kweli pande zote mbili hupata manufaa. Kuwasili mapema hukuwezesha ushiriki katika wimbo na sala ya kufungua—sehemu ya maana ya ibada ya kundi yenye mwungamano. Kusikia mada au kichwa kikitangazwa kutakusaidia ujue vizuri zaidi kufuata ukuzaji wa programu.

Kuwahi upande wako huwezesha wengine waratibu jitihada zao, na tokeo ni kwamba mengi yaweza kutimizwa. Alipokuwa akishambulia jiji la Ai, Yoshua alituma sehemu ya vikosi vyake ikawe chambo cha kuwavuta adui watoke kwenye jiji huku wanaume wale wengine wakiotea ili walitwae jiji. Halafu, kwenye wasaa ule wa maana, Yoshua akaitoa ishara. Wanaume wake “wakapiga mbio mara hapo alipokuwa amekwisha unyosha mkono wake,” nalo jiji likaanguka mbele yao. Je! waweza kuwazia ingetendeka nini kama wasingalitenda kwa kuwahi?—Yoshua 8:6-8, 18, 19.

Wahudumu Wakristo leo wana sababu nyingi za kujali wakati. Kushiriki katika kuhubiri Ufalme pamoja na wengine, kufanya mazoezi ya sehemu za kusanyiko au mikutano, hata kusafisha Jumba la Ufalme, yote hayo hututaka turatibu vitendo vyetu pamoja na vya wengine. Kwa kuwahi, twaweza kutimiza mengi zaidi. Hiyo ni kweli hata katika jambo lililo sahili kama kuripoti utendaji wa kuhubiri kwa mtu mwishoni mwa mwezi. Kila mmoja ashirikianapo katika kufanya hivyo bila kukawia, ndipo ripoti sahihi na zenye kutia moyo za kundi na za ulimwenguni pote ziwezapo kujumlishwa pamoja.

Kuwahi kwahusisha kutimiza miadi iliyowekwa na mipaka ya nyakati pia, nayo ni mingi kila siku. Baadhi yayo ni ya umaana mkubwa sana, mingine ni ya umaana kidogo. Kwa kielelezo, arusi yako yapasa kuanza wakati uliowekwa. Huenda wewe ukataka yai lako lichemshwe kwa muda usiozidi dakika fulani hususa. Chochote kile, mtu mwenye kuwahi hahitaji kufanya haraka ya kibumbuazi kutoka jambo moja hadi jingine, akichelewa kwa kila jambo. Bali, yeye ni mtulivu na mwenye utengenezo. Hufanya mengi zaidi kwa sababu yeye hupanga siku yake na kuanza kwa wakati ufaao au hata mapema kidogo.

Kwa kweli, kuna sababu nyingi kwa nini Wakristo wapaswa kujali wakati. Juu ya yote, hiyo ni njia moja ya kuonyesha upendo wetu usio na ubinafsi kwa Wakristo wenzetu na staha yetu kwa mipango ya kitheokrasi kwa ajili ya ibada ya kweli.

Ingawa hivyo, mtu aweza kukuzaje tabia hiyo ya kuwahi?

‘Zijue Nyakati Zilizowekwa’

“Hata korongo . . . ajua vema nyakati zake zilizowekwa” za kuhama, na chungu “hutayarisha chakula chake hata katika kiangazi” ili kiwe tayari kwa ajili ya kipupwe, yasema Biblia. (Yeremia 8:7; Mithali 6:8, NW) Humo ndimo ilimo siri ya kuwahi na kufanikiwa kufanya mambo.

Ni lazima sisi pia ‘tujue nyakati zetu zilizowekwa.’ Yatupasa kufikiria wakati, ingawa si kushikilia mambo mno au kuwa washupavu wasio na kiasi. Twahitaji kujua si jambo tupaswalo kufanya tu bali pia wakati tupaswalo kulifanya. Twahitaji kuizoea tabia ya kufikiri mapema, kuruhusu nafasi kwa mikawizo iwezayo kutokea, na kuwa na nia ya kupunguza utendaji ulio mkononi kwa ajili ya jambo fulani lililo la maana zaidi, kama vile mikutano yetu, huduma ya shambani, na utendaji mwingine wa kitheokrasi.

Kwa habari hii, ushirikiano wa kifamilia wahitajiwa sana. Imeonwa kwamba mara nyingi baba huachia mke wake kutayarisha familia. Halafu yeye huenda nje mlangoni akiwa peke yake, huku akitazama nyuma na kuita hivi, “Fanyeni haraka, au sivyo mtachelewa!” Yakobo hakuwa hivyo; yeye alisaidia kwa ‘kuinuka na kuinua watoto wake na wake zake juu ya wale ngamia’ ulipofika wakati wa kuondoka.—Mwanzo 31:17, NW.

Basi, baba aweza kusaidiaje familia yake? Watoto waweza kufundishwa kuruhusu wakati wa kujitayarisha kwa ajili ya mambo ya maana badala ya kuacha kila jambo hadi dakika ya mwisho. Wao waweza kusaidiwa wakuze hisia ya kujali madaraka na fahari ya kujivunia kufanya mambo bila kukawia. Mkiwa familia, fikirieni vielelezo vya Biblia vionyeshavyo umaana wa kuwa tayari kwa wakati ufaao. (Mwanzo 19:16; Kutoka 12:11; Luka 17:31) Labda somo lililo zuri kabisa au lenye matokeo kabisa huandaliwa na kielelezo kifaacho cha wazazi.

Waangalizi Wakristo waweza pia kusaidia kundi kwa kuweka kielelezo kifaacho. Wao wasingaliwekwa kama wasingalikuwa ‘watu wa utaratibu.’ (1 Timotheo 3:2) Labda ndugu na dada wengine watawahi zaidi wakijua kwamba wazee watakuwapo kuwasalimu na kuchukua uongozi. Kwa hiyo waangalizi wenye kudhamiria mambo watajitahidi kuwa kwenye Jumba la Ufalme mapema ili kulisaidia kundi. Watumishi wa huduma wawasilio mapema kusalimu ndugu zao na kutumikia mahitaji yao huthaminiwa sana.

Bila shaka, kuwahi huhitaji kujidhibiti na nidhamu. La, kusudi si kufikia ukamili wa kuwahi kijeshi, bali ni kwa sababu ya upendo kwa Wakristo wenzetu na staha kwa utaratibu wa kitheokrasi. Hii ni sehemu ya utu mpya ambao sisi tunajitahidi kuuvaa. (Wakolosai 3:10, 12) Juu ya yote, sisi twataka kuwa kama Baba yetu wa kimbingu, Yehova Mungu, ambaye hutufundisha kwamba “kwa kila jambo kuna wakati uliowekwa.”—Mhubiri 3:1, NW.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa mazungumzo marefu juu ya unabii huu, ona Insight on the Scriptures, Buku 1, kurasa 460-1 na 776-7.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki