Muono-Ndani Juu ya Habari
Kwa Nini Kueneza Evanjeli?
Ukosefu wa kueneza evanjeli kwa upande wa waenda-kanisani umetajwa na wenye mamlaka fulani kuwa wahusiana na upungufu wa washirika wa kanisa miongoni mwa dini zile kubwa-kubwa. Hangaiko juu ya tatizo hili katika 1988 liliharakisha United Church of Christ lipitishe uamuzi kwamba jambo la kutangulizwa kwanza kwa muda wa miaka minne ni lile suala la “kueneza evanjeli na kukuza ushirika.”
Gazeti St. Petersburg Times laripoti kwamba madhehebu nyingine kubwa-kubwa katika United States, kutia na Kanisa la Kipresbiteri na Kanisa Episkopali, zimetenda hali moja. Hata hivyo, uchunguzi wa hivi majuzi wa makundi zaidi ya 200 ya United Church of Christ ulifunua kwamba wengi wa washiriki walo milioni 1.6 hawadhihirishi upendezi mwingi katika kuongea na wengine juu ya imani yao. Mshiriki mmoja aliuliza hivi: “Mbona tulazimike kuongea na wengine ikiwa twatenda mema?” Mwingine alisema: “Ukiishi kulingana na imani yako, si lazima uongee juu yayo.”
Na bado, katika kitabu chake American Mainline Religion, mtungaji mwenzi Wade Clark Roof alikiri kwamba “kudumu kwa imani yenyewe kwahusiana sana na jinsi watu waongeavyo juu ya maisha zao za kidini na za kiroho.”
Ikiwa ‘kufanya mema’ na kuwa na “imani” kwatosha ili kumpendeza Mungu, mbona mtume Paulo aliandika hivi: “Ole wangu nisipoihubiri Injili”? Aliwaeleza hivi waamini wenzake katika Roma: “Ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini [kujizoeza imani, NW] moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.”—1 Wakorintho 9:16; Warumi 10:9, 10.
Kutumia Ngono kwa Faida ya Ubinafsi
Zaidi ya hadithi za vichekesho zipatazo 1,100 zilizotokea katika vichapo mbalimbali vya Kijapani, kutia na vile vya watoto, zilisimulia vitendo vya ngono, akasema Profesa Mamoru Fukutomi. Yeye aliongoza uchunguzi mmoja katika Tokyo wa magazeti zaidi ya 390 na vichapo vingine vilivyonunuliwa kwa mwezi mmoja.
‘Yaliyo mengi ya masimulizi ya kitendo cha ngono,’ asema Profesa Fukutomi, ‘hufuata kigezo cha wanaume wenye kulazimisha wanawake wasiotaka [ili wafanye mwingiliano wa kingono] na hatimaye wanawake wakiitikia kwa utendaji.’ Karibu asilimia 80 ya foto zile 6,861 zilizochanganuliwa katika magazeti maarufu ya Kijapani “zilionyesha wanawake wakiwa katika hali ya kuchochewa kingono,” laripoti The Daily Yomiuri. Ijapokuwa walio wengi wa wanawake katika picha hizo walikuwa “wamevaa mavazi ya ndani, mavazi ya kuogelea au wakiwa uchi” na ni asilimia 40 tu waliokuwa na nguo, asilimia 75 ya wanaume walio katika picha zilizochunguzwa walikuwa na nguo.
Utumizi huo wa ngono kwa faida ya kibinafsi utawaathirije wachanga? Kitabu cha Biblia cha Mithali hueleza wazi sana juu ya mwanamume kijana ‘asiye na kusudio jema’ akivutwa kwenye nyumba ya malaya fulani. (Mithali 7:7, Reference Bible, kielezi cha chini) Namna gani yule malaya? “Mara yuko nje-nje, mara yumo katika nyanja za watu wengi, naye aotea-otea karibu na kila kona. Naye amemshika imara kijana huyo.” (Mithali 7:8-13, NW) Katika nyakati za ki-siku-hizi hata vichapo ‘huotea-otea ili kuwashika imara’ vijana. Hata hivyo, Biblia huonya hivi: “Moyo wako usizielekee njia zake, [wala] usipotee katika mapito yake.”—Mithali 7:25.
Ni Nani Aliye Mkristo
“Mzuri Zaidi”?
“Hata uwe ni uamuzi gani ambao Mkristo hufanya, uwe ni wa kuwa askari au wa kuwa mkataaji kwa sababu ya dhamiri, lingekuwa kosa kwake kujidaia mwenyewe kadiri ya juu zaidi ya Ukristo kuliko ya yule mwingine, au hata kutilia shaka Ukristo wa yule mwingine kwa sababu ya kuunga mkono msimamo ulio tofauti na wake mwenyewe.”
Taarifa hiyo ilitolewa na Baraza la Ujeremani la Kanisa Evanjeliko la Kilutheri katika Julai 1989. Kwa nini? Maofisa walisema kwamba ilikuwa ili kupinga msimamo uliochukuliwa na watu fulani katika kanisa kwamba ukataaji wa kidhamiri ni “ishara iliyo chanya” zaidi ya kuwa Mkristo kuliko vile utumishi wa kijeshi ulivyo. Ingawa lilikubali kwamba Wakristo wangeweza kukomesha vita kwa “kujiepusha kibinafsi na jeuri,” Baraza la Kanisa lilibisha kwamba jambo hilo lingaliweza pia kufanywa kwa kupambana na jeuri kwa kutumia uwezo wa kijeshi ili kuleta amani.
Katika kitabu chake History of Christianity, Edward Gibbon aliandika kwamba Wakristo wa karne ya kwanza “walikataa ushiriki wowote wa bidii katika usimamizi wa kiserikali au ulinzi wa kijeshi wa ile milki,” na kwamba “ilikuwa haiwezekani Wakristo kujitwalia sifa ya kuwa askari, ya kuwa mahakimu [majistreti], au ya kuwa wana-wafalme, bila kukana wajibu ulio mtakatifu zaidi.”
Kwa hiyo, swali si juu ya ni nani aliye Mkristo “mzuri zaidi,” bali ni kama mtu anayefuatia mwendo ulio kinyume cha Ukristo wa mapema ni Mkristo kweli kweli. Paulo aliandika hivi: “Ingawa tunaenenda katika mwili, hatufanyi vita kwa jinsi ya mwili; maana silaha za vita vyetu si za mwili.”—2 Wakorintho 10:3, 4.