Kutangaza Kweli Kila Siku kwa Kumwiga Yesu
1 Yesu alikuwa na kazi hususa ya kutimiza alipokuja duniani. Ilikuwa dhahiri: ‘Kutoa ushahidi kwa ile kweli.’ (Yn. 18:37, NW) Alitangaza kweli kuhusu sifa za ajabu na makusudi ya Baba yake. Kazi hii ilikuwa kama chakula kwake; maisha yake yote yalikazia kazi hiyo. (Yn. 4:34) Luka aliripoti kwamba Yesu aliendelea ‘kufundisha kila siku hekaluni.’ (Luka 19:47) Yesu alitumia vizuri wakati uliopatikana. (Yn. 9:4) Muda mfupi kabla ya kifo chake, aliweza kumjulisha Baba yake hivi: “Mimi nimekutukuza duniani, hali nimeimaliza kazi ile uliyonipa niifanye.”—Yn. 17:4.
2 Mioyo yetu inapojawa na uthamini kwa yote ambayo Yehova ametufanyia, sisi vilevile huhisi kusukumwa kusema kumhusu kila siku. Sisi huwa tu kama wanafunzi wa Yesu waliotangaza hivi kwa ujasiri: “Sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia.” (Mdo. 4:20) Kusema kwao kuhusu Yehova kulikuwa kwenye kuendelea, kwa kuwa rekodi yasema kwamba ‘kila siku . . . hawakuacha.’ (Mdo. 5:42) Twapaswa kujiuliza, ‘Je, mimi ni mwigaji wa Mwalimu wangu, Yesu?’
3 Kuhubiri kwa Uharaka: Yesu alitabiri kwamba wakati ujumbe wa Ufalme utakapokuwa umetangazwa duniani kote, “ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Hilo lapaswa kukazia kwetu umaana na uharaka wa kazi yetu. Kihalisi, maisha ya mamilioni yakiwa hatarini, hii ndiyo kazi ya maana zaidi kufanya. Kwa kuwa mfumo huu wa mambo unakaribia mwisho wake, wakati uliobaki wa kumaliza kazi hii ni mfupi!
4 Ripoti zaonyesha kwamba Yehova anaharakisha kukusanywa kwa watu wenye mfano wa kondoo. (Isa. 60:22) Katika sehemu nyingi za ulimwengu, kihalisi watu wanamiminika kwenye kweli, ni kana kwamba wanatangaza kwa shangwe: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi”! (Zek. 8:23) Wakati huu kuliko wakati wowote uliopita, maneno haya ya Yesu ni ya kweli: “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. . . . Mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Je, hilo halituchochei tuwe wenye bidii kama wanafunzi wa Yesu ambao ‘walikuwa daima ndani ya hekalu, wakimsifu Mungu’?—Luka 24:53.
5 Julisha Kweli Kila Siku: Kila siku, twapaswa kutafuta njia za kuwapa wengine kweli. Fursa zapatikana. Je, unaweza kuchukua dakika chache kumpigia simu rafiki au mtu ambaye unamfahamu unayehisi anaweza kukubali? Au vipi juu ya kumwandikia barua mtu ambaye hukuweza kumpata nyumbani? Je, umewaza juu ya kumtolea trakti muuzaji wa dukani unaponunua vitu? Yamkini, unaweza kufikiria fursa nyinginezo nyingi ulizo nazo kila siku za kushiriki tumaini lako pamoja na wengine. Ukijitahidi na kuonyesha ujasiri kidogo, Yehova atakusaidia.—1 The. 2:2.
6 Kwa hiyo, tuanzapo utendaji wa kila siku, twapaswa kujiuliza wenyewe, ‘Je, nitachukua hatua ya kushiriki tumaini langu pamoja na mtu fulani fursa ikijitokeza leo?’ Iga mtazamo wa Yesu, ambaye alieleza sababu aliyotumwa duniani: ‘Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Luka 4:43) Tukitaka kuwa kama Mwalimu wetu, tutafanya vivyo hivyo.—Luka 6:40.