Mashamba Ni Meupe kwa Ajili ya Kuvunwa
1. Ni kazi gani muhimu inayoendelea leo?
1 Baada ya kumhubiria mwanamke Msamaria, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yoh. 4:35, 36) Uvunaji wa wale wanaokubali ujumbe wa Biblia ulikuwa umeanza, na Yesu aliweza kutambua kimbele kwamba kazi hiyo ingeenea duniani kote. Akiwa katika cheo chake mbinguni, Yesu ana sehemu kubwa sana katika kazi ya mavuno. (Mt. 28:19, 20) Nini kinachoonyesha kwamba kazi hii inazidi kuongezeka na kuwa ya uharaka zaidi kadiri tunavyokaribia upeo wake?
2. Ni mambo gani yanayoonyesha kwamba kazi ya uvunaji ya ulimwenguni pote inaongezeka?
2 Mavuno Ulimwenguni Pote: Katika mwaka wa utumishi wa 2009, kulikuwa na ongezeko la asilimia 3.2 ya wahubiri ulimwenguni pote. Kulikuwa na ongezeko la asilimia 14 katika nchi ambazo kazi ya kuhubiri iko chini ya vizuizi. Idadi ya mafunzo ya Biblia yaliyoripotiwa kila mwezi ilikuwa zaidi ya 7,619,000. Idadi hiyo inazidi idadi ya kilele cha wahubiri na ni karibu nusu milioni zaidi ya mafunzo ya Biblia yaliyoripotiwa mwaka wa 2008. Kadiri kazi inavyozidi kuongezeka katika maeneo mengi, ndivyo kulivyo na uhitaji mwingi wa wamishonari waliozoezwa katika Shule ya Gileadi. Katika nchi nyingi, maeneo ya lugha ya kigeni yana matokeo makubwa. Ni wazi kwamba Yehova anaharakisha kazi wakati wa umalizio wa mavuno. (Isa. 60:22) Je, una maoni yanayofaa kuelekea “mashamba” yenu?
3. Huenda wahubiri fulani wakakata kauli gani kuhusiana na mavuno katika eneo lao?
3 Mavuno Katika Eneo Lenu: Huenda wengine wakasema, “Eneo letu halina matokeo sana.” Ni kweli kwamba maeneo fulani hayaonekani kuwa na matokeo kama mengine, au hayana mazao kama yalivyokuwa hapo awali. Hivyo basi, huenda Mashahidi wengine wakakata kauli kwamba mavuno yameisha na sasa kazi iliyobaki tu ni ya kuokota masalio. Je, hivyo ndivyo mambo yalivyo?
4. Tunapaswa kusitawisha mtazamo gani mzuri kuelekea huduma yetu, na kwa nini?
4 Kuanzia mwanzo hadi mwisho, wakati wa mavuno ni pindi yenye shughuli nyingi sana. Ona mtazamo wa uharaka unaokaziwa na maneno haya ya Yesu: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Yehova, Bwana wa mavuno, anajua ni lini na ni wapi kuna matokeo. (Yoh. 6:44; 1 Kor. 3:6-8) Hivyo basi, fungu letu ni gani? Biblia inajibu hivi: “Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike.” (Mhu. 11:4-6) Ndiyo, kwa kuwa kazi ya mavuno inakaribia upeo wake, huu si wakati wa kuacha mikono yetu ipumzike!
5. Kwa nini tunapaswa kuendelea kuhubiri kwa bidii hata katika maeneo yanayoonekana kuwa hayana matokeo?
5 Endelea Kuvuna: Hata ikiwa eneo letu limehubiriwa tena na tena na linaonekana kuwa halina matokeo, tuna sababu nzuri za kuendelea kulihubiri kwa bidii na tukiwa na mtazamo wa uharaka. (2 Tim. 4:2) Matukio makubwa na mabaya katika ulimwengu yanawafanya watu wabadili mitazamo yao na wafikirie kwa uzito zaidi kuhusu wakati ujao. Vijana wanapoendelea kukomaa, huenda wakahisi kwamba wanahitaji kutafuta usalama na amani ya akili. Na huenda wengine wakavutiwa na bidii yetu. Ndiyo, watu ambao hawakutusikiliza hapo awali, huenda wakakubali ujumbe wa Biblia baadaye. Hata wale wanaokataa ujumbe wetu kimakusudi wanahitaji kupewa onyo.—Eze. 2:4, 5; 3:19.
6. Ikiwa eneo letu linaonekana kuwa halina matokeo, ni nini kitakachotusaidia kudumisha bidii?
6 Ikiwa eneo letu linaonekana kuwa halina matokeo, ni nini kitakachotusaidia kudumisha bidii? Mbali na kuhubiri nyumba kwa nyumba, tunaweza kujaribu njia nyingine kama vile kuhubiri maeneo ya biashara au kuhubiri kwa simu. Au tunaweza kubadili mtindo wetu wa kuhubiri. Pia, tunaweza kubadili ratiba yetu ili tushiriki utumishi wa jioni au tuhubiri nyakati ambazo yaelekea watu wengi wanapatikana nyumbani. Labda tunaweza kujitahidi kujifunza lugha mpya ili kuwafikia wengi na habari njema. Vilevile, tunaweza kupanua utumishi wetu kwa kuchukua upainia wa kawaida. Au, tunaweza kuhamia eneo lililo na wavunaji wachache. Tukiwa na mtazamo unaofaa kuelekea kazi hii muhimu ya mavuno, tutajitahidi kadiri iwezekanavyo kuishiriki kikamili.
7. Tutaendelea na kazi ya kukusanya mavuno mpaka lini?
7 Wakulima wana muda mfupi wa kukusanya mazao, hivyo, hawazembei wala kulegeza mwendo mpaka wamalize kuvuna. Uvunaji wa kiroho unahitaji mtazamo huohuo wa uharaka. Tutaendelea na kazi hii ya kukusanya mavuno mpaka lini? Katika kipindi chote cha “umalizio wa mfumo wa mambo” na mpaka wakati wa “ule mwisho.” (Mt. 24:14; 28:20) Kama Yesu, yule Mhudumu mkuu wa Yehova, tunataka kumaliza kazi tuliyopewa. (Yoh. 4:34; 17:4) Kwa hiyo, acheni tuendelee kuhubiri kwa bidii, shangwe, na mtazamo unaofaa mpaka mwisho. (Mt. 24:13) Mavuno hayajaisha!
[Blabu katika ukurasa wa 2]
Kuanzia mwanzo hadi mwisho, wakati wa mavuno ni pindi yenye shughuli nyingi sana