Kuzidi Kutoa Ushahidi Mwisho Ukaribiapo
1 Majira ya mavuno huwa wakati wenye shangwe. Pia huwa wakati wa kazi ngumu. Kuna wakati mchache tu wa kukusanya mazao. Wafanyakazi huwa hawachezichezi katika kazi yao.
2 Akisema kitamathali, Yesu alilinganisha “umalizio wa mfumo wa mambo” na wakati wa mavuno. (Mt. 13:39) Tunaishi katika umalizio wa huu mfumo wa mambo, tukibaki na wakati mchache wa kutoa ushahidi “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Mwisho ukaribiapo zaidi, twahitaji kuzidisha ushiriki wetu katika huduma. Kwa nini? Yesu alieleza: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.”—Mt. 9:37, 38; Rom. 12:11.
3 Ifanye kwa Hima: Yesu alipoanza kazi yake kuu ya kuhubiri, alikuwa na muda wa miaka mitatu na nusu tu ili kutimiza kile alichokuwa amegawiwa kufanya. Alihubiri akiwa na hisi ya uharaka, akisema: “Lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu kwa ajili ya hili nilitumwa.”—Luka 4:43.
4 Yesu alifanya wanafunzi wake waone uharaka kama huo. (Mr. 13:32-37) Ndiyo sababu “kila siku katika hekalu na kutoka nyumba hadi nyumba wa[li]endelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.” (Mdo. 5:42) Shughuli zisizo na maana sana hazikutangulizwa maishani mwao. Ingawa walikuwa wachache, walifaulu kuhubiri habari njema “katika viumbe vyote chini ya mbingu.”—Kol. 1:23.
5 Kuna sababu kubwa zaidi kwetu kusitawisha hisi ya uharaka kama hiyo sasa, kwa kuwa “mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Pet. 4:7) Yehova ameweka siku na saa ya mwisho wa huu mfumo wa mambo. (Mt. 24:36) Kazi ya kuhubiri itakamilishwa katika wakati uliobaki. Ndiyo sababu tunazidisha jitihada zetu za kufikia watu wengi zaidi tukiwa na habari njema.
6 Kwa kuzidi kutoa ushahidi mwisho ukaribiapo, tutaridhika kumwambia Yehova, kama Yesu alivyomwambia: ‘Tumemaliza kazi ambayo umetupa kufanya.’—Yn. 17:4.