Sanduku La Swali
◼ Ni matumizi gani yafaayo ya misemo “ndugu” na “dada”?
Inapotumiwa kwa njia halisi, misemo “ndugu” na “dada” hurejezea watu mmoja-mmoja walio wa wazazi walewale. Uhusiano huu wa asili kwa kawaida huleta ukaribu mchangamfu, na ukaribiano wanaopata watu hawa huongezwa zaidi na muungano wa kijamii, kimazingira, na kihisia-moyo.
Yesu alifundisha wanafunzi wake kumwita Yehova katika sala “Baba Yetu.” Matumizi ya msemo huo huonyesha kwamba tukiwa Wakristo, sisi sote ni sehemu ya kikundi cha familia ambapo tunafurahia uhusiano mzuri wa kiroho. Hili lilikaziwa zaidi na Yesu alipowaambia wafuasi wake kwamba “nanyi nyote ni ndugu.”—Mt. 6:9; 23:8.
Kwa sababu ya miungano yetu ya karibu ya kiroho katika nyumba ya Mungu, tunaitana “Ndugu” na “Dada,” hasa katika mikutano ya kutaniko. Wakati wa pindi hizi za kiroho, yule anayeongoza mkutano hutambua watu mmoja-mmoja waliobatizwa kwa kutumia msemo “ndugu” au “dada” ukifuatiwa na jina la mwisho la mtu anayetajwa.
Vipi ikiwa mtu asiyebatizwa anataka kushiriki katika mikutano? Ikiwa mtu ameshiriki na watu wa Yehova kwa muda fulani naye anaelekea kufikia wakfu, akijiona kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, hakutakuwa na upingamizi kumtaja kwa jina la mwisho likitanguliwa na “Ndugu” au “Dada.” Itakuwa hivyo hasa ikiwa mtu huyo amekuwa mtangazaji asiyebatizwa.
Kwa upande mwingine, watu wenye kupendezwa ambao wameanza tu kuhudhuria mikutano yetu bado hawajachukua hatua ambazo zinawatambulisha kuwa sehemu ya nyumba ya Mungu. Watu hawa hawataitwa “Ndugu” au “Dada,” kwa kuwa hawana uhusiano wa kiroho pamoja na familia ya Mungu. Kwa hiyo wakati wa mikutano, tutawaita kikawaida, tukitumia cheo kifaacho kama vile “Bwana” na jina lao la mwisho.
Kutumia misemo “ndugu” na “dada” kwenye mikutano yetu ya kutaniko huonyesha muungano ulio wa karibu sana na wenye thamani kuliko wowote unaoonyeshwa na majina ya kwanza. Hutukumbusha uhusiano wenye baraka sana tunaofurahia tukiwa familia ya kiroho chini ya Baba mmoja, Yehova Mungu. Pia hutukumbusha upendo wenye kina kirefu na shauku tuliyo nayo kwa mmoja na mwenzake.—Efe. 2:19; 1 Pet. 3:8.