“Imani Katika Neno la Mungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1997
1 Mtume Paulo alikumbusha Timotheo kwamba “Andiko lote limepuliziwa na Mungu.” (2 Tim. 3:16) Kwa kuwa Neno la Mungu limepuliziwa, tuna kila sababu ya kudhihirisha imani katika hilo. Kichwa cha mkusanyiko wa wilaya wa mwaka huu ni “Imani Katika Neno la Mungu.” Programu hiyo itaimarisha imani yetu katika Biblia, iwe tumejua kweli kwa miaka mingi au tumeshirikiana na tengenezo la Yehova hivi majuzi. Sisi sote twapaswa kupanga kuhudhuria programu nzima. Itakuwa yenye kujenga jinsi gani ikiwa watu wenye kupendezwa, hasa wale tunaojifunza Biblia nao, watahudhuria!
2 Mkusanyiko wa Siku Tatu: Mwaka huu mkusanyiko wa wilaya wa siku tatu umepangwa kwa manufaa yetu. Kufikia sasa umejulishwa kuhusu mkusanyiko ambao kutaniko lako limegawiwa, na unapaswa kuwa umefanya mipango hususa kuhudhuria siku zote tatu za hiyo programu. Je, umemfikia mwajiri wako ili upate ruhusa ya wakati unaohitajiwa? Ikiwa una watoto wenye umri wa kwenda shuleni na mkusanyiko wenu unakuwa wakati wa muhula wa shule, je, umewajulisha walimu wao kwa njia ya fadhili kwamba watoto wako hawatakuwapo Ijumaa kwa sababu ya sehemu ya maana ya mafundisho yao ya kidini?—Kum. 31:12.
3 Kutakuwa na uandalizi wa Lugha ya Ishara ya Kimarekani katika mikusanyiko ya Kiingereza inayofuata: Nairobi, Mombasa, na Kampala. Ndugu zetu viziwi na wenye kupendezwa wapaswa kuelekezwa kwenye mmojawapo wa mikusanyiko hii mitatu.
4 Programu itaanza kila siku saa 3:30 asubuhi. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Wale tu ambao wataruhusiwa kuingia kabla ya wakati huo watakuwa wale walio na migawo ya kazi, lakini hawataruhusiwa kuhifadhi viti hadi jengo lifunguliwe kwa ajili ya kila mtu.—Flp. 2:4.
5 Wapaswa Kukazia Uangalifu: Mtume Petro alikumbusha Wakristo wa karne ya kwanza kwamba wanapaswa kulikazia uangalifu neno la kiunabii kama kwamba ni taa ing’aayo mahali penye giza. (2 Pet. 1:19) Ndivyo ilivyo kwetu leo. Kuishi katika ulimwengu huu wa kale unaoongozwa na Shetani ni kama kuwa mahali penye giza. Tunashukuru kuwa tumeitwa kutoka katika giza la kiroho. (Kol. 1:13; 1 Pet. 2:9; 1 Yoh. 5:19) Ili kudumu katika nuru, twahitaji kuendelea kuimarisha imani yetu kwa kulikazia uangalifu Neno la Yehova lililopuliziwa. Mkusanyiko wetu wa wilaya utatutia moyo kufanya hivyo.
6 Jitihada huenda ikahitajiwa upande wetu ikiwa tutakaza fikira kwenye programu, lakini bila shaka tutabarikiwa tukifanya hivyo. Twapaswa kujitahidi kuja mkusanyikoni tukiwa tumepumzika vizuri ili tuwe chonjo wakati wa vipindi. Ruhusu wakati wa kutosha wa kufika kwenye mkusanyiko kila siku, ili uweze kuwa kwenye kiti chako kabla ya programu kuanza. Kisha jiunge katika kuimba wimbo wa kufungua na sala mwanzoni mwa kila siku ya programu. Watu wazima wapaswa kuweka kielelezo, nao wazazi wapaswa kuwazoeza watoto wao.—Efe. 6:4.
7 Tukitazama vichwa vya sehemu kabla ya programu ya siku kuanza, twaweza kujaribu kutazamia mbele mambo yatakayotokezwa kwenye kipindi hicho. Hili litaongeza upendezi wetu katika habari inapotolewa. Tunaweza kutafuta mambo ya kutusaidia tueleze wengine kwa nini twaamini Mungu na ahadi yake ya hakika ya kuthawabisha wale wanaomtafuta kwa bidii. (Ebr. 11:1, 6) Imependekezwa kwamba tuandike maandishi mafupi ya kutusaidia kukumbuka mambo makuu katika programu. Tukiandika maandishi mengi sana, huenda tukakosa mambo fulani ya msingi kwa sababu tunashughulika sana na kuandika.
8 Mwaka uliopita tena watu fulani wazima na vijana walionwa wakitembea bila kusudi kwenye vijia, kuzunguka-zunguka nje, na kuwatembelea wengine programu ilipokuwa ikiendelea, badala ya kusikiliza yale ambayo “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alikuwa ameandaa kwa manufaa yetu. Yesu aliahidi kutupatia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45-47) Kwa hiyo, twapaswa kuwapo ili tunufaike na chakula hicho na tusionyeshe ukosefu wa uthamini. (2 Kor. 6:1) Pia yaonekana kwamba watoto wengine wanapokosa kutulia, mara nyingi wao huomba kwenda msalani ukiwa udhuru wa kuondoka na kwenda kuzurura. Mazoezi yafaayo nyumbani yatahakikisha kwamba safari za kwenda msalani si za lazima. Nyakati nyingine, vijana wakubwa hukaa pamoja mahali palipojitenga, wakiongea, kunong’onezana, na kupitishiana maandishi. Vijana wetu, ambao hukabili msongo mwingi leo, wahitaji kuikazia fikira habari inayotolewa, si kufanya mambo mengine wakati wa programu. Tamaa za ujana ambazo hazipatani na kanuni za Biblia zapasa kuepukwa. (Linganisha 2 Timotheo 2:22.) Usikivu wa wote, watu wazima kwa vijana, utamheshimu Yehova na kumletea shangwe.
9 Ikiwa lazima kwa mmoja wa wakaribishaji kumpa yeyote shauri kuhusu mambo haya, lapaswa kupokewa likiwa uandalizi wa upendo kutoka kwa Yehova. (Gal. 6:1) Wote wanahitaji kukumbuka kwamba sababu ya kuweka jitihada za kuhudhuria mkusanyiko ni kwamba tuweze ‘kusikiliza na kujifunza.’ (Kum. 31:12) Pia, “mwenye hekima asikie na kuongezewa elimu.” (Mit. 1:5) Wakati unaobaki kabla hujahudhuria mkusanyiko, zungumza na familia yako uhitaji wa kuketi pamoja na wasikilizaji, mbaki mkiwa mmekaa wakati wa programu, na msikilize kwa makini, ili mpate manufaa kamili ya programu.
10 Mapambo Yampendezayo Yehova: Watu wa Yehova wako wazi waonwe na ulimwengu wote. (1 Kor. 4:9) Kwa ujumla sisi hutambuliwa kwa kiwango chetu kizuri cha mavazi na mapambo. Kutumia kanuni za Kimaandiko zinazopatikana kwenye 1 Timotheo 2:9, 10 na kwenye 1 Petro 3:3, 4 kumetokeza mabadiliko makubwa zaidi katika sura ya wengi wakilinganishwa na jinsi walivyoonekana walipoanza kushirikiana na kutaniko la Kikristo. Ni tofauti sana na viwango vyenye kushuka zaidi vya mavazi na mapambo ambavyo twaona katika ulimwengu. Twataka kujihadhari tusije tukawa kama ulimwengu kuhusu sura—tukivaa mavazi ya kupita kiasi, yanayochochea mitindo ya muda tu ya kilimwengu katika mitindo ya nywele, au kuvalia kwa njia isiyo ya adabu. Mavazi yetu na mambo yetu yenye kutoa kielelezo kizuri yapaswa kusaidia wapya wanaohudhuria mkusanyiko waone jinsi Wakristo wanavyopaswa kujipamba wenyewe.
11 Ingawa wazo lililoachwa likiwa tokeo la mkusanyiko wa mwaka uliopita lilikuwa lenye kupendeza, mavazi na mapambo ya kilimwengu yanaendelea kuwa tatizo kwa baadhi ya ndugu na dada, hasa baada ya vipindi vya siku. Tunapofanya mipango yetu ya kuhudhuria mkusanyiko, twapaswa kujichunguza wenyewe kuhusu mavazi na mapambo yetu. Wazazi, kwa hekima angalieni kile ambacho watoto wenu wachanga na matineja wetu watakachovaa. Hakikisheni kwamba hatuachi mitindo ya kilimwengu na mitindo ya muda tu iathiri vibaya sura yetu ya Kikristo.
12 Dumisha Mwenendo Mzuri: Mwenendo mzuri ni ishara ya Wakristo wa kweli. (1 Pet. 2:12) Tabia yetu popote pale ambapo huenda tukawa—kwenye mkusanyiko, kwenye mikahawa, na katika mahoteli, na vilevile tunaposafiri—yaweza kutoa ushahidi mzuri na kusaidia wengine waone kile ambacho imani katika Mungu na Neno lake yaweza kufanyia watu. Huenda hiyo ikasaidia wengine wapate kumjua Yehova. (Linganisha 1 Petro 3:1, 2.) Tuna pendeleo la kumtukuza Mungu kwa mwenendo wetu. Wasimamizi wa hoteli moja walisema kwamba wajumbe wetu ni “kikundi kizuri zaidi na kilicho na mwenendo bora zaidi walichokaribisha.” Waliongezea hivi: “Litakuwa pendeleo kuwa nanyi tena wakati ujao.” Ofisi moja inayoshughulika na mambo ya mikusanyiko na ya kitalii katika upande wa kaskazini-magharibi mwa Marekani iliandika hivi: “Kila mwaka mkutano wa Watchtower Society hungojwa kwa hamu na jumuiya yetu yote. Washiriki wenu wapendeza kikweli; wakijiendesha wenyewe kwa hisani na staha ya hali ya juu. Biashara zetu hutambua jambo hili nazo huthamini kurudi kwa ‘familia’ yao ya wageni-waalikwa kila mwaka.” Ripoti kama hizi zapendeza kuzisoma, sivyo? Hata hivyo, kuna uhitaji wa kudumu waangalifu, ili tudumishe sifa nzuri ya watu wa Yehova.
13 Tafadhali kumbukeni kwamba kupika hakufanywi katika vyumba vya mahali pa mkusanyiko. Kukiruhusiwa, sehemu inayofaa itaonyeshwa na halmashauri ya mkusanyiko. Jambo hilohilo litahusu vyumba vya hoteli, isipokuwa viwe na mahali pa kupikia kwa kusudi hilo.
14 Hudhurio la kusanyiko limeendelea kukua katika shamba letu ijapokuwa ndugu wengi wanakabili magumu ya kiuchumi. Twawapongeza nyinyi akina ndugu kwa kuonyesha uthamini kwa chakula cha kiroho tunachoendelea kupokea kupitia programu za mkusanyiko. Hapana shaka kwamba mmeanza kuweka akiba ya fedha ili muwe na nauli yenu ya kutosha ya kusafiri ya na familia zenu. Twatumaini kupata kitabu Proclaimers katika Kiswahili katika mikusanyiko. Kwa kuwa kichapo hiki kitatumiwa baadaye katika “Ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 1998,” akina ndugu hasa katika makutaniko ya Kiswahili wapaswa kujitayarisha wawe na nakala ya kichapo hiki.
15 Kumbuka kwamba kutoa bakshishi kunafaa unapopokea utumishi wa kibinafsi, hasa kwa kuwa wengi wanaotumika kwenye umma, kama vile wahudumu wa kiume na wa kike, watumishi wanawake, na wenye kuelekeza wageni kwenye vyumba, hutazamia bakshishi. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, twataka kuonyesha tabia nzuri kwa habari hii pia.—Ona Amkeni! la Aprili 8, 1987, ukurasa wa 25-28.
16 Kulipia Gharama za Mkusanyiko: Sisi sote tutakuwa na gharama kuhusiana na kuhudhuria mikusanyiko. Kuna gharama nyingine ambayo twapaswa kufikiria. Majengo yanayotumiwa kwa ajili ya mikusanyiko ni ghali. Pia kuna gharama nyingine ambazo lazima zilipiwe. Michango yetu yenye ukarimu na ya kujitolea yathaminiwa sana.—Mdo. 20:35; 2 Kor. 9:7, 11, 13.
17 Viti: Mwelekezo ambao umetolewa kwa miaka kadhaa utaendelea kutumika, yaani, VITI VYAWEZA KUHIFADHIWA TU KWA AJILI YA WASHIRIKI WA KARIBU WA FAMILIA YAKO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE KATIKA GARI LAKO. Inapendeza kuona kwamba katika miaka ya juzijuzi wengi zaidi wanatii mielekeo hii, na hili limeongeza hali ya upendo inayoonyeshwa kwenye mikusanyiko. Mahali kwingine viti hupatikana kwa urahisi kuliko kwingine. Tafadhali onyesha ufikirio, na uachie wale ambao hali zao zataka viti vifaavyo zaidi.
18 Kamera, Vidiokamera, na Virekodio vya Kaseti: Kamera na vifaa vya kurekodia vyaruhusiwa kutumiwa mikusanyikoni. Hata hivyo, kuvitumia kwetu hakupaswi kuwakengeusha fikira wengine katika hudhurio. Hatupaswi kutembea-tembea tukipiga picha, kwa kuwa hilo lingesumbua wengine wanaojaribu kuikazia fikira programu. Vifaa vya aina yoyote vya kurekodia havipaswi kuunganishwa kwenye mifumo ya umeme au ya sauti, wala vifaa hivi havipaswi kufunga vijia vya kupitia, au kuzuia wengine kuona.
19 Msaada wa Kwanza: Idara ya Msaada wa Kwanza ni ya dharura tu. Haiwezi kushughulikia walio na magonjwa ya kudumu. Hiyo ndiyo sababu wapaswa kufikiria mahitaji ya afya yako na ya familia yako mapema. Tafadhali lete aspirini, visaidizi vya umeng’enyaji, bendeji, pini, na vifaa vifananavyo na hivyo, kwa kuwa vitu hivyo havitapatikana kwenye mkusanyiko. Wowote walio hatarini mwa kifafa, mshtuko, matatizo ya moyo, na kadhalika, wapaswa watazamie kimbele mahitaji yao kadiri iwezekanavyo. Wanapaswa kuwa na dawa wanazohitaji, na mshiriki wa familia au wa kutaniko anayeelewa hali yao apaswa kuwa pamoja nao nyakati zote ili kuandaa usaidizi unaohitajiwa. Matatizo yametokea kwenye mikusanyiko mtu mmoja-mmoja aliye na matatizo ya kudumu ya afya alipoachwa peke yake, akawa mgonjwa. Uhudumiaji wa mkusanyiko umelazimika kuwasiliana na idara za tiba ya dharura ili wapelekwe hospitali. Yeyote aliye na washiriki wa familia ambao wana ugonjwa wa kudumu watataka kuhakikisha kwamba hawa hawaachwi bila mtu wa kuwaangalia. Ikiwa wengine wenye mahitaji ya pekee ya afya hawana washiriki wa familia wanaoweza kuwasaidia, wazee wa kutaniko lao watahitaji kujulishwa kuhusu hali hiyo na kufanya mipango ya lazima ili kusaidia. Hakuna uandalizi utakaofanywa kwenye mikusanyiko kwa ajili ya kupatia wenye mizio vyumba vya pekee.
20 Chakula Kwenye Mkusanyiko: Kuwa bila utumishi wa chakula mikusanyikoni kumetokezea wengi uhuru zaidi wa kutofanya kazi wakati wa vipindi ili wakaze fikira kwenye chakula cha kiroho. Maelezo kadhaa ya shukrani kwa usahilishaji huu yamepokewa tangu mpango huo uanzishwe. Wote wanapaswa kupanga ili walete vyakula vyao wenyewe vyenye kufaa, vijengavyo mwili kwa mapumziko ya mchana, kama vile vilivyodokezwa katika nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Mei 1995, fungu la 12 na 13. Vyombo vya gilasi na vinywaji vyenye alkoholi havipaswi kuletwa mahali pa kufanyia mkusanyiko. Vyombo vya kuwekea chakula vyapaswa kuwa vyenye udogo wa kutosha kuwekwa chini ya kiti chako. Wengine kati ya wasikilizaji wameonwa wakila na kunywa wakati wa programu. Kufanya hivi ni kukosa staha. Mahali ambapo kuna kioski mahali pa kufanyia mkusanyiko au kuna wachuuzi nje, ndugu wengine wameonwa wakinunua vyakula wakati wa programu. Zoea hilo halifai.
21 Kwa kweli twathamini karamu yetu ya kiroho na mazingira yenye kupumzisha, yenye amani ya ushirika wakati wa mapumziko mafupi ya mchana. Ili kushikamana na kusudi la mpango huu, badala ya kuacha mahali pa kufanyia mkusanyiko wakati wa pumziko la mchana ili kwenda kununua chakula, tafadhali uje na chakula. Hivyo, utakuwa na wakati mwingi zaidi wa kufurahia ushirika wa ndugu na dada zako.
22 Twafurahi kama nini kwamba “Imani Katika Neno la Mungu” Mikusanyiko ya Wilaya itaanza karibuni! Sisi sote twataka kuhakikisha kwamba matayarisho yetu yamefanywa ili kuhudhuria programu yote, ili tuweze kufurahia kikamili karamu nzuri ya kiroho ambayo Yehova ametutayarishia kupitia tengenezo lake. Kwa njia hiyo tutakuwa “[tuli]oandaliwa vifaa kikamili kwa ajili ya kila kazi njema.”—2 Tim. 3:17.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Vikumbusha vya Mkusanyiko wa Wilaya
Ubatizo: Wataka kubatizwa wapaswa kuwa vitini mwao katika mahali palipoteuliwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Akina dada hasa watataka kuangalia mapema kuona kama mavazi wanayopanga kuvaa yanabaki yakiwa yenye staha hata yanapokuwa yamelowa maji. Vazi la kuogelea lenye staha au vazi jingine lifaalo na taulo vyapasa kuletwa na kila mmoja anayepanga kubatizwa. Wakati uliopita wengine wamevalia vazi ambalo halikufaa na lililokengeusha fikira juu ya hiyo pindi. Wazee wanaopitia maswali katika kitabu Huduma Yetu pamoja na wataka kubatizwa wanapaswa kuhakikisha kwamba kila mtu anaelewa mambo haya. Baada ya hotuba ya ubatizo na sala itakayotolewa na msemaji, mwenyekiti wa kipindi atataja wimbo. Baada ya ubeti wa mwisho, wakaribishaji watawaelekeza wataka kubatizwa hadi kwenye mahali pa uzamisho. Ubatizo katika mfano wa wakfu wa mtu ni jambo la uhusiano wa karibu na la kibinafsi kati ya mtu huyo na Yehova. Hivyo, haifai wataka kubatizwa kukumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.
Kadi za Beji: Tafadhali vaa kadi ya beji ya 1997 nyakati zote mnapokuwa katika jiji la mkusanyiko na mnaposafiri kwenda na kutoka huko. Mara nyingi hili hutokeza fursa kwetu kutoa ushahidi mzuri. Kadi na vifuko vya beji vyapasa kununuliwa kupitia kutaniko, kwa kuwa havitapatikana mkusanyikoni. Usingoje hadi siku chache kabla ya mkusanyiko kuuliza juu ya kadi zako na za familia yako. Kumbuka kubeba kadi yako ya wakati huu ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia.
Mahali pa Kulala: Wale wanaohitaji mahali pa kulala katika madarasa au vyumba vya shule katika majengo mengine ambamo hakuna vitanda wala matandiko yawapasa wakumbuke kuleta matandiko yao wenyewe. Mahali pengine, usiku waweza kuwa wenye baridi sana. Katika maeneo mengine, akina ndugu wameliona likiwa jambo lenye hekima kuwa na aina fulani ya kujilinda na mbu. Tafadhali iweni waangalifu mnapokunywa maji na hasa mwangalie watoto wanywe maji safi.
Nyimbo: Nyimbo zifuatazo zimeteuliwa kwa ajili ya programu ya mwaka huu: 4, 10, 13, 43, 46, 77, 98, 130, 138, 144, 155, 156, 160, 164, 180, 183, 191, na 195. Watu mmoja-mmoja na vikundi vya familia huenda wakataka kupanga vipindi vya mazoezi ili waweze kushiriki kikamili katika kuimba nyimbo zote wakati wa programu ya mkusanyiko.
Utumishi wa Kujitolea: Je, waweza kutenga kando wakati kwenye mkusanyiko ili usaidie katika mojawapo ya idara? Kutumikia ndugu zetu, japo kwa saa chache tu, kutasaidia sana nako huleta uradhi mwingi sana wa kibinafsi. Ikiwa waweza kusaidia, tafadhali ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kwenye mkusanyiko. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kutoa usaidizi mzuri kwa kufanya kazi chini ya mwelekezo wa mzazi au mtu mzima mwingine mwenye daraka.
Maneno ya Tahadhari: Angalia matatizo yawezayo kutokea ili kuepuka magumu yasiyo ya lazima. Mara nyingi wezi na watu wengine walaghai huibia watu ambao ni wageni kutoka sehemu nyingine. Hakikisha gari lako limefungwa nyakati zote, na usiache kamwe garini chochote chenye kuonekana kiwezacho kumfanya mtu alivunje ili kuiba. Wezi na wenye kuibia watu mifukoni hukazia fikira vikusanyiko vikubwa. Halingekuwa jambo la hekima kuacha vitu vyovyote vyenye thamani kitini mwako. Huwezi kuwa na hakika kwamba kila mtu anayekuzunguka ni Mkristo. Kwa nini ukaribishe vishawishi? Ripoti zimepatikana za majaribio yaliyofanywa na watu fulani wa nje ili kudanganya watoto na kuwatorosha. ANGALIA WATOTO WAKO NYAKATI ZOTE.
Uangalifu wapaswa kutolewa pia ili kuepuka kujaza kupita kiasi magari yaliyokodiwa na kutaniko kwa ajili ya safari ya mkusanyiko. Ni afadhali kutumia fedha za ziada kwa gharama za usafiri kuliko kuvunja sheria za Kaisari au vibaya hata zaidi kuweka akina ndugu katika hatari za aksidenti na upotezo uwezekanao wa uhai kwa sababu ya kujaza gari kupita kiasi au kumtia moyo dereva aendeshe kasi zaidi ili mfike mnakoenda mapema. (Rom. 13:1-7; Kum. 21:1-9) Akina ndugu wenye daraka wanaosafiri kwenye magari hayo wanapaswa kujihisi huru kutoa shauri lenye upendo kuhusiana na jambo hili ikihitajika.