Mafunzo ya Biblia Yanayotokeza Wanafunzi
1 “Ni nini chenye kunizuia nisibatizwe?” akauliza towashi Mwethiopia baada ya Filipo “[ku]mtangazia habari njema juu ya Yesu.” (Mdo. 8:27-39) Katika kisa cha towashi, yeye tayari alikuwa ameyapenda maandishi ya Mungu yaliyopuliziwa, na baada ya kupokea msaada wa kiroho kutoka kwa Filipo, alikuwa tayari kuwa mwanafunzi. Lakini si watu wote wanaosadikishwa kwamba wanahitaji wenyewe kuyachunguza Maandiko.
2 Kwa shukrani, tengenezo la Yehova limeandaa broshua, Mungu Anataka Tufanye Nini?, ili kutia watu moyo wajichunguzie wenyewe matakwa ya Mungu. Habari iliyo katika broshua hiyo yapasa kuvutia watu wenye moyo mweupe ambao huenda wakawa na elimu lakini hawajui mengi juu ya Biblia. Chombo hiki kizuri kimekusudiwa kuchochea watu watake kuichunguza Biblia.
3 Unapoanzisha funzo la Biblia, ingesaidia kupitia madokezo bora zaidi yaliyochapishwa katika nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Juni 1996 juu ya jinsi funzo lenye matokeo liwezavyo kuongozwa katika kitabu Ujuzi. Wakati wa mtaala wa funzo, chunguza maendeleo yanayofanywa na mwanafunzi ili uweze kuamua ni sehemu zipi zinazohitaji uangalifu zaidi. Tia moyo mwanafunzi atayarishe masomo yake mapema, akiyasoma maandiko yaliyotajwa. Maelezo yanayotolewa kwa maneno yake mwenyewe yanaweza kuonyesha uthamini wake wa moyoni kwa ajili ya kweli. Maendeleo ya haraka mara nyingi yanafanywa na wale ambao wanasoma zaidi vichapo vya Sosaiti na wanaohudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida. Mtie moyo azungumze kivivi hivi na wengine juu ya yale anayojifunza. Mwonyeshe kwa fadhili analohitaji kufanya ili afanye maendeleo ya kiroho. Hatupaswi kuongoza mafunzo kwa wakati usio dhahiri na watu wenye kusitasita kuamua. Wanafunzi wanapaswa kuchukua hatua ya kwanza ya kujifunza, wachukue msimamo imara kwa ajili ya kweli, na kusonga mbele kuelekea wakfu na ubatizo.
4 Katika nyumba fulani-fulani, mafunzo zaidi ya moja huongozwa, kwa kuwa washiriki tofauti-tofauti wa familia wana mafunzo yao mbalimbali. Hata hivyo, kuwa na funzo la familia lililounganishwa kwaweza kuwa bora katika visa vilivyo vingi, kwa kuwa kutasaidia kuvuta familia pamoja kiroho.
5 Amri ya Yesu ni kwamba twende tukafanye wanafunzi. (Mt. 28:19) Ili kufanya hivyo, lazima tuongoze mafunzo ya Biblia yanayosaidia wanafunzi wafanye maendeleo kufikia hatua ya kwamba waweza kuuliza, “Ni nini chenye kunizuia nisibatizwe?”