Je, Wewe Huitikiaje Ubaridi?
1 Ubaridi ni ukosefu wa hisia au hisia-moyo, kukosa upendezi au hangaikio. Ni mojawapo ya mitazamo ya kawaida na migumu sana tunayokabili katika huduma. Wewe huuitikiaje? Umekusababisha upunguze huduma yako? Waweza kuushindaje ili kufikia watu kwa ujumbe wa Ufalme?
2 Kwanza, chunguza ujue ni kwa nini watu katika eneo lako wana ubaridi. Je, ni kwa sababu wametamaushwa na viongozi wao wa kisiasa na wa kidini? Je, wanahisi kwamba hakuna utatuzi wa matatizo wanayokabili? Je, ni wenye kutazamia mema juu ya ahadi za jambo bora zaidi? Je, wao hawataki kufikiria mambo ya kiroho isipokuwa waone manufaa halisi za mara moja?
3 Kazia Tumaini la Ufalme: Hakuna tatizo ambalo Ufalme hautalitatua. Kwa hiyo tukiweza, twapaswa kusema na watu juu ya ahadi za Ufalme, tukitaja maelezo makuu ya Kimaandiko, hata kama haiwezekani au si jambo lenye kutumika kuonyesha andiko la Biblia. (Ebr. 4:12) Hata hivyo, twaweza kuendelezaje mazungumzo kufikia hapo?
4 Watu wanahitaji kuelezwa kusudi la kuzuru kwetu. Wanahitaji kutambua kwamba tuko hapo kwa sababu ya upendo kwa jirani na hangaikio la jamii. Twaweza kuuliza swali lililofikiriwa vizuri kama vile, “Unafikiri suluhisho la [tatizo linaloathiri jamii] ni nini?” Mfikio mmoja usipofaulu, jaribu mwingine.
5 Katika eneo moja lililo na ukwasi mwingi ambalo wenye nyumba walikuwa na ubaridi kuelekea ujumbe wa Ufalme, wahubiri walijitahidi sana kutafuta utangulizi utakaoamsha kupendezwa. Walipokuwa wakitoa kitabu Ujuzi, wenzi fulani walijaribu utangulizi huu: “Je, wafikiri elimu bora ni ya maana ili kufanikiwa ulimwenguni leo? Je, wakubali kwamba elimu iliyo pana ingetia ndani ujuzi wa Biblia?” Katika alasiri moja waliangusha vitabu vitatu, kimoja ambacho walimwangushia mwanamke ambaye baadaye alisema alisoma kitabu Ujuzi kizima na alikubali funzo la Biblia.
6 Unapokabili ubaridi, jaribu mifikio mbalimbali, uliza maswali yenye kuamsha fikira, na tumia nguvu ya Neno la Mungu. Huenda kwa njia hiyo ukaweza kusaidia wengine wakubali tumaini letu la ajabu la Ufalme.