Mlango Mkubwa Uongozao Kwenye Utendaji Umefunguliwa
1 Akiwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii, Paulo alitafuta kabisa kwa hamu maeneo yaliyokuwa na uhitaji mkubwa zaidi, moja ya hayo lilikuwa jiji la Efeso. Alikuwa na mafanikio mazuri akihubiri huko hivi kwamba aliandikia Wakristo wenzake hivi: “Nimefunguliwa mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji.” (1 Kor. 16:9) Paulo aliendelea kutumikia akiwa katika eneo hilo naye akasaidia Waefeso wengi kuwa waamini.—Mdo. 19:1-20, 26.
2 Leo tumefunguliwa mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji. Tuna mwaliko wa kusaidia makutaniko ambayo hayawezi kuhubiri eneo lao lote kikamili kila mwaka. Hivyo jitihada zetu zaweza kusawazisha uhitaji uliopo katika maeneo mengine.—Linganisha 2 Wakorintho 8:13-15.
3 Je, Waweza Kutumikia Mahali Palipo na Uhitaji Mkubwa Zaidi? Je, umefikiria kwa njia ya sala uwezekano wa kutumikia mahali penginepo? Huenda ukaweza kusaidia kutaniko fulani mjini mwako mwenyewe. Kwa nini usiongee na mwangalizi wa mzunguko kuhusu jambo hilo na uone atakayodokeza? Au huenda ikawa kwamba katika eneo la kutaniko lako mwenyewe, kuna idadi ya watu iliyo kubwa ya viziwi au watu wenye kuongea lugha ya kigeni ambayo hakuna mtu ambaye ameweza kuishughulikia. Ili kutimiza uhitaji huu, je, waweza kujikakamua ujifunze lugha yao? Kisha tena, labda tayari kuna kikundi cha lugha nyingine au kutaniko lililo karibu ambalo limekuwa ‘likimwomba Bwana-Mkubwa wa mavuno lipate wafanyakazi zaidi wa Ufalme.’ (Mt. 9:37, 38) Ikiwa ni hivyo, je, waweza kusaidia?
4 Miongo ya hivi majuzi, maelfu ya familia za Kikristo yamehamia nchi nyingine ili yashiriki kikamili zaidi katika kazi ya mavuno. Wenzi wa ndoa waliofanya hivi walisema: “Tulitaka kumtumikia Yehova mahali ambapo tungesaidia zaidi.” Ukiwa na tamaa hii na ukiona inawezekana kuhamia penginepo katika nchi yako au ukiwa na sifa ya ustahili kutumika katika nchi nyingine, kwanza zungumza matazamio yako na wazee wa kutaniko lako.
5 Ukitaka kuulizia habari kutoka kwa Sosaiti kuhusu mahali palipo na uhitaji, andalia Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko barua inayoonyesha tamaa yako mahususi. Wataambatisha maelezo yao na kuipelekea Sosaiti. Kwa vyovyote vile, maadamu mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji unaendelea kuwa umefunguliwa, sisi sote na tuendelee kuwa wenye shughuli nyingi katika utumishi wa Yehova.—1 Kor. 15:58.