Kabla ya Kuhubiri, Huenda Ukahitaji Kutafuta Kwanza
1. Katika mahali ambako watu huzungumza lugha mbalimbali, kwa nini maeneo ya makutaniko hupangwa kulingana na lugha?
1 Katika Pentekoste ya 33 W.K., baada ya kupokea roho takatifu, wanafunzi wa Yesu ‘walianza kusema katika lugha tofauti’ kwa watu waliokuwepo kutoka sehemu nyingine za dunia. (Mdo. 2:4) Matokeo yakawa kwamba watu 3,000 hivi walibatizwa. Inaonekana kuwa wengi wa wageni hao pia walizungumza lugha fulani kuu ya wakati huo, labda Kiebrania au Kigiriki. Na bado Yehova aliamua kwamba wanapaswa kuhubiriwa ujumbe wa Ufalme katika lugha yao ya asili. Bila shaka sababu moja ya kufanya hivyo ni kwamba kwa kawaida watu hukubali habari njema kwa utayari zaidi wanapoisikia katika lugha yao. Hivyo basi, leo, katika mahali ambapo watu huzungumza lugha mbalimbali, maeneo ya makutaniko hupangwa kulingana na lugha. (Tengenezo uku. 107, fu. 2-3) Wahubiri wa vikundi vya lugha ya kigeni hawapewi eneo hususa, bali huwahubiria watu wanaozungumza lugha yao katika eneo la kutaniko linalowasimamia au maeneo ya makutaniko mengine yaliyo karibu.
2. (a) Kazi ya kutafuta ni nini, na huenda ikahitajika kufanywa wapi? (b) Makutaniko yanaweza kusaidianaje kuhubiri katika maeneo yenye watu wanaozungumza lugha mbalimbali? (c) Tunapaswa kufanya nini iwapo tutampata mtu anayependezwa ambaye anazungumza lugha nyingine?
2 Ikiwa unaishi katika mahali ambako watu huzungumza lugha ileile, ni rahisi kuhubiri kutoka nyumba moja hadi nyingine. Hata hivyo, huenda hali ikawa tofauti ikiwa unaishi katika mji au jiji ambako lugha mbalimbali huzungumzwa. Makutaniko ya lugha nyingine yanaweza kuwa yakihubiri katika maeneo yaleyale. Ijapokuwa makutaniko hayo yanaweza kuwapa habari kuhusu watu ambao wanazungumza lugha ya kutaniko lenu, jukumu la kutafuta watu mnaopaswa kuhubiria ni la kutaniko au kikundi chenu. (Ona sanduku “Saidianeni.”) Hivyo basi, huenda mkalazimika kufanya kazi ya kutafuta watu ambayo itahusisha kuulizia watu wanaozungumza lugha yenu. Kazi ya kutafuta inaweza kufanywaje?
3. Ni nini kinachoamua mahali ambapo kutaniko au kikundi kitafanya kazi ya kutafuta na wakati ambao utatumiwa kwa ajili ya kazi hiyo?
3 Kupanga Kazi ya Kutafuta: Kiasi cha wakati mtakachotumia mnapofanya kazi ya kutafuta watu katika maeneo yenye lugha mbalimbali kinategemea hali za kwenu. Kwa mfano, ni watu wangapi katika jamii huzungumza lugha hiyo? Kuna wahubiri wangapi? Kufikia sasa, kutaniko au kikundi kina anwani za watu wangapi wanaozungumza lugha hiyo? Kutaniko halihitajiwi kufanya kila sehemu kwa kiwango kilekile, lakini huenda likaamua kukazia zaidi sehemu zenye watu wengi katika eneo lao au kwenye maeneo ambayo hayako mbali sana. Hata hivyo, ni muhimu kuwa na mpango mzuri wa kutafuta ili watu wengi iwezekanavyo wapate fursa ya kuliitia jina la Yehova.—Rom. 10:13, 14.
4. (a) Kazi ya kutafuta inapaswa kupangwaje? (b) Ni zipi baadhi ya njia za kutafuta watu wanaozungumza lugha yenu?
4 Ili kuepuka kufanya kazi maradufu katika sehemu ambayo kazi ya kutafuta inafanywa, baraza la wazee, na hasa mwangalizi wa utumishi, linapaswa kupanga na kusimamia kazi ya kutafuta. (1 Kor. 9:26) Katika vikundi vya lugha ya kigeni, ndugu anayestahili, hasa mzee au mtumishi wa huduma aliyechaguliwa na baraza la wazee la kutaniko linalosimamia kikundi hicho, anaweza kuongoza katika kazi hiyo. Makutaniko na vikundi vingi vina mpango mzuri wa kufanya utafiti kabla ya kuanza kutafuta, labda kwa kutumia kitabu cha orodha ya majina ya watu au Intaneti ili kukusanya majina ambayo kwa kawaida hupewa watu ambao huzungumza lugha hiyo. Kisha kazi ya kutafuta hufanywa kupitia simu au kuwatembelea watu ili kujua kama anwani zao zinapaswa kuhifadhiwa. Ikiwa inafaa, baraza la wazee wa kutaniko linalosimamia kikundi linaweza kufanya mipango ili mara kwa mara kutaniko lote lishiriki katika kazi ya kutafuta.—Ona sanduku “Jinsi ya Kuwatafuta Watu Wanaozungumza Lugha Yenu.”
5. (a) Taja baadhi ya mapendekezo ambayo wahubiri wanaofanya kazi ya kutafuta wanaweza kutumia. (b) Tunaweza kuwaambia watu nini tunapofanya kazi ya kutafuta?
5 Tunapaswa kuwa na lengo hususa kila wakati tunaposhiriki kibinafsi katika kazi ya kutafuta. Kwa kuwa hii ni sehemu ya huduma yetu, tunapaswa kuvaa mavazi yanayofaa kama tunavyofanya tunapokuwa katika utumishi wa shambani. Wengi wameona kwamba kujizoeza mambo watakayosema na kuzungumza lugha hiyo wanapofanya kazi ya kutafuta huwasaidia kudumisha shauku na pia huboresha uwezo wao wa kuzungumza na kuielewa lugha hiyo. Katika ripoti yetu ya utumishi wa shambani, tunaweza kuripoti wakati tunaotumia katika kazi ya kutafuta lakini tusiripoti wakati ambao tumetumia kutayarisha orodha na ramani za maeneo. Tunapompata mtu ambaye anazungumza lugha yetu, tunapaswa kujitahidi kumhubiria habari njema na bila kukawia tumfahamishe mwangalizi wa utumishi au mtu mwingine aliyeteuliwa na mwangalizi huyo ili rekodi za maeneo zijazwe habari za karibuni zaidi. Tunapaswa kufanya hivyo iwe mtu huyo alipendezwa au la. Ingawa kazi ya kutafuta ni muhimu, tunapaswa kuwa na usawaziko na kushiriki katika sehemu zote za huduma.—Ona sanduku “Mambo ya Kusema Tunapofanya Kazi ya Kutafuta.”
6. Kutafuta viziwi hutokeza hali gani za pekee?
6 Kuwatafuta Watu Ambao Ni Viziwi: Kazi ya kuwatafuta viziwi hutokeza hali za pekee na inahitaji jitihada na bidii nyingi. Kiziwi hawezi kutambuliwa kwa kutaja tu majina, umbo, au vazi lake. Isitoshe, huenda watu wa familia na marafiki wakahofia usalama wa mtu huyo na hivyo wakasita kuwapa wahubiri habari kumhusu. Mapendekezo yafuatayo kuhusu kuwatafuta viziwi yanaweza pia kutusaidia tunapotafuta watu wanaozungumza lugha nyingine.
7. (a) Ni habari gani tunazoweza kuulizia katika maeneo ya makazi ili kuwapata viziwi? (b) Tunaweza kufanya nini ili kuondoa wasiwasi wa mwenye nyumba?
7 Wahubiri katika makutaniko na vikundi vya lugha ya ishara wamepata mafanikio wanapotafuta viziwi katika nyumba za makazi. Labda mwenye nyumba amemwona jirani, mfanyakazi, au mwanashule mwenzake akitumia lugha ya ishara. Huenda ameona kibao barabarani kinachoonyesha kwamba kuna watoto viziwi. Labda ana mtu wa ukoo ambaye ni kiziwi. Kumbuka kwamba huenda watu wakashuku nia yako ya kuwatembelea. Hata hivyo, unaweza kuondoa wasiwasi wao kwa kupendezwa nao kikweli na kuwaeleza kifupi, kwa unyoofu, na kwa heshima, kusudi lako la kuwatembelea. Wengine wanapomuuliza mwenye nyumba kama anajua kuhusu mtu yeyote kiziwi, wao humwonyesha Biblia au DVD za lugha ya ishara na hivyo wamepata matokeo mazuri. Kisha wanataja kwamba wangependa kuzungumza na mtu huyo kuhusu tumaini la Biblia. Ikiwa mwenye nyumba anasita kutoa habari, huenda akakubali kuchukua kadi yako ya anwani au mwaliko wa kuhudhuria mkutano ili ampe mtu wa ukoo au rafiki yake ambaye ni kiziwi.
8. Kutaniko la karibu linaweza kusaidiaje kutaniko la lugha ya ishara?
8 Siku moja au mbili kwa mwaka, kutaniko la lugha ya ishara linaweza kualika kutaniko la karibu linalotumia lugha tofauti ili wasaidiwe kazi ya kutafuta katika sehemu fulani ya mji katika eneo lao. Mkutano wa utumishi wa shambani unaoongozwa na kutaniko la lugha ya ishara unaweza kutia ndani maagizo ya kazi hiyo na pia onyesho. Kila kikundi kinaweza kugawiwa angalau mhubiri mmoja kutoka kutaniko la lugha ya ishara na kipewe ramani inayoonyesha eneo hususa ambako watatafuta.
9. Kazi ya kutafuta inaweza kufanywaje mahali ambako viziwi hukutanika ili kuonana na wenzao, kwa ajili ya tafrija au kupata huduma muhimu?
9 Kazi ya kutafuta inaweza pia kufanywa katika maeneo ambako viziwi hukusanyika ili kuonana na wenzao na kwa ajili ya tafrija au kupata huduma muhimu ambazo hutolewa katika jamii. Wahubiri wanapaswa kuvaa kulingana na hali hususa. Huenda likawa jambo la busara zaidi kuzungumza na mtu mmoja au wawili waliopo badala ya kuzungumza na watu wote wakiwa kikundi. Ikiwa mazungumzo ni yenye matokeo, huenda mhubiri akabadilishana anwani na mtu huyo.
10. Wahubiri wanawezaje kufanya kazi ya kutafuta katika aina mbalimbali za biashara?
10 Njia nyingine ni kutayarisha ramani zinazoonyesha biashara mbalimbali na kisha kwenda huko wakati unaofaa. Ramani moja inaweza kutia ndani vituo kadhaa vya mafuta. Nyingine inaweza kutia ndani mikahawa, dobi, hoteli, au aina nyingine za biashara. Ikiwa kila ramani ina aina ileile ya biashara, wahubiri wanaweza kutumia njia ileile ya kuwafikia watu na hivyo kupata uzoefu na ustadi. Kwa mfano, kwa kuwa hoteli huwahudumia wateja viziwi, tunaweza kumweleza kifupi mpokezi wa wageni hotelini kuhusu kazi yetu na tumpe kifurushi kidogo chenye DVD fulani na mwaliko wa mikutano ili awape wateja viziwi. Katika biashara nyingine, tunaweza tu kuuliza kama kuna wafanyakazi au wateja wanaohudumiwa kwa ukawaida ambao hutumia lugha ya ishara. Iwapo kuna shule ya viziwi katika eneo, tunaweza kuwapa baadhi ya DVD zetu kwa ajili ya maktaba yao.
11. Kwa nini kazi ya kutafuta ni sehemu muhimu ya huduma?
11 Kazi Muhimu: Kazi ya kutafuta wenye nyumba wanaozungumza lugha fulani inaweza kuchosha. Kwa kuongezea, watu katika maeneo mengine huhamahama na hivyo huwa vigumu kudumisha rekodi za karibuni zaidi za maeneo hayo. Hata hivyo, katika maeneo mengi, kazi ya kutafuta ni sehemu muhimu ya huduma. Yehova, ambaye ametupa kazi ya kuhubiri, hana ubaguzi. (Mdo. 10:34) “Mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Kwa hiyo, acheni tushirikiane na Yehova na wahubiri wenzetu ili kuwatafuta watu wa lugha zote ambao wana “moyo mzuri na mwema.”—Luka 8:15.
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Saidianeni
Ikiwa kutaniko au kikundi kingependa kupata msaada wa kuwatafuta wale wanaozungumza lugha yao, mwangalizi wa utumishi anaweza kuwasiliana na wazee wa makutaniko ya lugha nyingine yaliyo karibu. Huenda likawa jambo zuri kuwasiliana tu na makutaniko yasiyo mbali sana au yaliyo na idadi kubwa ya watu katika eneo lao ambao huzungumza lugha hiyo. Makutaniko yaliyoulizwa kuhusu watu wanaozungumza lugha fulani yanaweza kuwajulisha wahubiri wa kutaniko lao kwamba ikiwa watampata mtu yeyote anayezungumza lugha hiyo, wanapaswa kuandika anwani yake na kumpa mwangalizi wa utumishi ili aiwasilishe kwa kutaniko au kikundi kinachoomba msaada. Waangalizi wa utumishi wa makutaniko yanayohusika wanaweza kufanyiza utaratibu unaoweza kutumiwa na makutaniko na vikundi hivyo ili wote waweze kufanya kazi katika maeneo yenye lugha mbalimbali na kuwaelekeza wenye kupendezwa kwenye kutaniko au kikundi kinachowafaa.
Ikiwa wahubiri watampata mtu wa lugha nyingine ambaye inaonekana wazi kuwa anapendezwa (au mtu aliye kiziwi), wanapaswa kujaza bila kukawia fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43) na wampe mwandishi wa kutaniko. Hilo litamwezesha mtu huyo kupata msaada wa kiroho haraka.—Ona km 5/11 uku. 3.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Jinsi ya Kuwatafuta Watu Wanaozungumza Lugha Yenu
• Uliza watu wengine—wanafunzi wa Biblia, watu wao wa familia, wafanyakazi wenzako, na wengineo.
• Tumia kitabu cha orodha ya nambari za simu ili kukusanya majina ambayo kwa kawaida hupewa watu ambao huzungumza lugha hiyo. Huenda kitabu cha majina ambayo yameorodheshwa kulingana na anwani kinaweza kupatikana kupitia Intaneti au kampuni ya simu.
• Ukitumia busara, ulizia katika sehemu zinazotoa huduma kwa umma kama vile maktaba, ofisi za serikali, na vyuo.
• Kwenye magazeti ya habari, tafuta matangazo kuhusu utendaji wa umma unaopangwa na jamii inayozungumza lugha hiyo ya kigeni.
• Tembelea maduka au biashara zinazohudumia jamii inayozungumza lugha hiyo.
• Ukiruhusiwa na wenye mamlaka, panga meza ya machapisho katika eneo fulani la biashara, kituo cha wanafunzi wa chuo, au kituo cha usafiri ambacho hutumiwa na watu wanaozungumza lugha hiyo.
• Ikiwa sheria ya nchi yenu inaruhusu, nunua kitabu cha nambari za simu za maeneo ya biashara au programu ya kompyuta ambayo unaweza kutumia kutafuta watu kwenye Intaneti wanaozungumza lugha hiyo.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
Mambo ya Kusema Tunapofanya Kazi ya Kutafuta
Tutamwondolea mtu wasiwasi ikiwa tutamfikia kwa njia ya kirafiki, na kuzungumza naye waziwazi na kwa unyoofu. Mara nyingi, ni vizuri kwanza kumwonyesha machapisho katika lugha yake.
Baada ya kumsalimu, unaweza kusema: “Tunawatafuta watu wanaozungumza ______ ili tuwaeleze kuhusu tumaini la Biblia. Unamfahamu mtu yeyote tunayeweza kuzungumza naye?”
Unapowatafuta viziwi, unaweza kusema: “Hujambo. Ungependa nikuonyeshe kitu fulani? [Ukitumia mashine ya mkononi inayoweza kucheza DVD, mwonyeshe andiko moja kutoka New World Translation katika DVD.] Hii ni sehemu ya Biblia katika Lugha ya Ishara ya Marekani. Mbali na Biblia, tuna video kadhaa zinazopatikana bila malipo ambazo zimekusudiwa kutosheleza mahitaji ya kiroho ya watu ambao ni viziwi. Unamfahamu mtu yeyote ambaye ni kiziwi au mwenye tatizo la kusikia na hutumia lugha ya ishara?” Ikiwa mwenye nyumba hawezi kukumbuka mtu yeyote, ni vizuri kumtajia mahali ambapo huenda akawa ameona viziwi, kama vile kazini, shuleni, au katika ujirani.