Wanaweza Kuona Kwamba Sisi Ni Tofauti
1 Mwaka uliopita, zaidi ya watu wapya 300,000 walijiunga nasi wakabatizwa. Ni nini ambacho watu hawa wameona katika Mashahidi wa Yehova kinachowafanya watake kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu? Kwa nini sisi ni tofauti sana na dini nyinginezo? Hapa pana majibu yaliyo dhahiri:
—Sisi hushikilia Biblia badala ya maoni ya kibinafsi: Sisi humwabudu Yehova Mungu “kwa roho na kweli,” kama vile Yesu Kristo alivyosema tufanye. Hiyo imemaanisha kukinza mafundisho yasiyo ya kweli ya kidini na kujipatanisha na yale yaliyo katika Neno la Mungu lililoandikwa.—Yn. 4:23, 24; 2 Tim. 3:15-17.
—Sisi huenda kwa watu badala ya kuwangoja waje kwetu: Tumekubali utume wa Kristo wa kuhubiri na kufundisha, nasi twaiga kielelezo chake cha kutafuta watu wenye moyo wa haki. Twawatafuta nyumbani kwao, barabarani, au popote ambapo huenda wakapatikana.—Mt. 9:35; 10:11; 28:19, 20; Mdo. 10:42.
—Sisi huandaa mafundisho ya Biblia kwa kila mtu bila malipo: Sisi hutumia mali na nishati zetu bila malipo, tukitoa muda wa saa zaidi ya bilioni moja kila mwaka katika utumishi wa Mungu. Bila ubaguzi wowote, twajifunza Biblia na watu wa aina zote.—Mt. 10:8; Mdo. 10:34, 35; Ufu. 22:17.
—Tumezoezwa vema kusaidia watu kiroho: Kupitia funzo letu la kibinafsi la Biblia na mafundisho yanayoandaliwa kwenye mikutano ya kutaniko, makusanyiko, na mikusanyiko, sisi hupokea elimu ya kitheokrasi yenye thamani, yenye kuendelea ambayo hutuwezesha kuelimisha wengine kiroho.—Isa. 54:13; 2 Tim. 2:15; 1 Pet. 3:15.
—Sisi huchukua kweli kwa uzito, tukiitumia maishani mwetu kila siku: Kwa sababu ya upendo wetu kwa Mungu, sisi hufanya marekebisho, tukipatanisha maisha zetu na mapenzi yake. Utu wetu mpya ulio kama wa Kristo huvutia wengine waje kwenye kweli.—Kol. 3:9, 10; Yak. 1:22, 25; 1 Yh. 5:3.
—Sisi hujitahidi kuishi na kufanya kazi pamoja na wengine kwa amani: Kusitawisha sifa za kimungu hutusaidia kulinda vitendo vyetu na usemi wetu. Sisi ‘hutafuta sana amani na kuifuatia’ na watu wote.—1 Pet. 3:10, 11; Efe. 4:1-3.
2 Vielelezo vya maisha ya Kikristo ambavyo watu huona katika tengenezo la Yehova huchochea wengi waikubali kweli. Kielelezo chetu binafsi na kiwe na matokeo hayohayo kwa wale wanaotujua na kutuchunguza.