Muumba Wetu Mtukufu Hutujali!
1 Katika jitihada zake za kusababu na Waisraeli wasio watiifu, Yehova aliuliza: “Je! wewe hukujua? hukusikia? Yeye Mungu wa milele, BWANA, Muumba miisho ya dunia.” (Isa. 40:28) Twamjua Muumba wetu Mtukufu, na twaona utunzaji wake wenye upendo kwetu. Hata hivyo, mamilioni ya watu hushuku kuwapo kwake au humdhania Mungu kwa njia isiyopatana na yale yanayopatikana katika Biblia. Twaweza kuwasaidiaje?
2 Kitabu kipya Je, Kuna Muumba Anayekujali? kimekusudiwa kusaidia watu wa aina hiyo. Hualika watu wenye kufikiri wasababu juu ya mambo ya hakika. Habari yenye kuvuta uangalifu na yenye hoja zenye kusadikisha katika kitabu hiki yapaswa kuwapendeza wale wanaokisoma.
3 Fahamu Kitabu Muumba: Weka akilini jambo la msingi la yaliyomo. Sura ya 2 hadi ya 5 hukazia jinsi ulimwengu, uhai, na mwanadamu alivyopata kuwapo na yule aliyeumba vyote hivyo. Sura ya 6 hadi ya 9 huchunguza Biblia na Mtungaji wake, hasa, kama simulizi la Mwanzo la uumbaji lapasa kutumainiwa. Sura ya 10 hutoa jibu lenye kuridhisha la mojawapo ya maswali magumu zaidi ambayo mwanadamu huuliza: “Ikiwa Muumba anajali, mbona wanadamu wanateseka sana?”
4 Jaribu Kusababu na Wale Wenye Shaka: Ukurasa wa 78-79 katika kitabu Muumba huonyesha hoja unayoweza kutumia kuwasaidia wengine wafikie mkataa sahihi kuhusu Mungu. Waulize: “Je, ulimwengu ulipata kuwa na mwanzo?” Wengi watakubali jambo hilo. Ikiwa ndivyo, uliza: “Mwanzo ulisababishwa au haukusababishwa?” Wengi hutambua kwamba ulisababishwa. Hilo laongoza kwenye swali la mwisho: “Je, mwanzo wa ulimwengu ulisababishwa na kitu fulani au na Mtu fulani wa umilele?” Mfikio huu waweza kufanya wengi waone kwamba lazima kuwe na Muumba.
5 Kitabu Muumba ni kitu ambacho watu wengi wanahitaji hasa. Kishiriki pamoja na watu wa jamaa, wafanyakazi wenzako, wanashule wenzako, na marafiki wengineo. Kibebe hudumani ili uweze kukiangushia wale unaowapata ambao wana mashaka kuhusu kuwapo kwa Mungu. Kadiri tunavyokifahamu kitabu hiki, ndivyo upendo wetu kwa Muumba utakavyoongezeka, ukituchochea twendelee kutembea kupatana na viwango vyake vya juu.—Efe. 5:1; Ufu. 4:11.