“Nifanyeje?”
1 Ukiwa kijana anayekaribia kufikia utu mzima, huenda ukauliza, ‘Nifanye nini na maisha yangu?’ Vijana Wakristo wanataka kupanua utumishi wao kwa Yehova katika huduma. Lakini unaweza kufanyaje hivyo unapokuwa na madaraka ya utu mzima, ambayo hutia ndani kujiandalia mahitaji yako mwenyewe ya kimwili? Huenda isiwe rahisi kupata jibu.
2 Vijana fulani huwa na wasiwasi wanapotazama hali ya kiuchumi ya ulimwengu na matabiri ya wakati ujao. Wao hujiuliza: ‘Je, nifuatie elimu ya kimwili ya ziada? Je, niingie katika utumishi wa wakati wote mara moja?’ Ili mtu afanye uamuzi mzuri, anahitaji kujibu swali hili kwa unyofu, ‘Ni jambo gani kuu linalonipendeza maishani?’ Lazima achunguze nia yake.
3 Ni nini ambacho umesitawisha kuwa hangaikio lako kuu katika ujana wako? Je, unapendezwa tu na kutafuta manufaa za kifedha, au kwa kweli unataka kutumia maisha yako kuendeleza masilahi ya Ufalme? Digrii ya chuo kikuu haitoi uhakikishio wa kufanikiwa kupata kazi ya kuajiriwa. Badala yake, wengi wamejipatia stadi za kazi zenye mafanikio kupitia programu za uanagenzi, elimu ya shule ya utaalamu au ufundi, au mitaala mifupi ya chuo ambayo huhitaji wakati mchache na kutojihusisha nayo sana.
4 Amini Ahadi ya Yehova: Jambo muhimu kufikiria ni uhakikisho kutoka kwa Yehova Mungu kwamba ataandalia wale wanaoweka masilahi ya Ufalme kwanza maishani. (Mt. 6:33) Hii si ahadi isiyo na msingi. Ndugu wengi wanaohudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma walipata digrii za chuo kabla ya kujifunza kweli. Lakini walikuwa wakifanya kazi gani ya kimwili? Ni wachache tu waliofuatia kazi waliyokuwa wamesomea. Wengi walikuwa wakifanya kazi za kurekebisha na kutunza vitu, wakishughulikia vizuri sana mahitaji yao ya kifedha huku wakipainia. Kwa kupanua utendaji wao katika huduma, wanapokea baraka nyingi zinazozidi fedha kwa mbali.
5 Unapoamua utakalofanya baada ya kumaliza shule ya sekondari, pima mambo yote na uchanganue nia yako kwa uangalifu. Ili upate maoni yanayosawazika ya uchaguzi wako, fikiria habari kama ile iliyokuwa katika Amkeni! la Machi 8, 1998, ukurasa wa 19-21. Zungumza na wazazi wako, wazee, mwangalizi wa mzunguko wenu, na mapainia wenye mafanikio katika eneo lenu. Kufanya hivyo kutakusaidia ufanye uamuzi wenye hekima kuhusu kile utakachofanya na maisha yako.—Mhu. 12:1, 13.