Kuhubiri Hutufanya Tuwe Tofauti
1 Watu wengi huuliza, “Ni nini ambacho huwatofautisha Mashahidi wa Yehova na dini zile nyingine?” Ungejibuje? Unaweza kueleza baadhi ya itikadi zetu zenye kutegemea Biblia. Lakini je, umefikiria pia kutaja jinsi ambavyo huduma yetu ya hadharani hututofautisha sana na dini zile nyingine?—Mt. 24:14; 28:19, 20.
2 Leo, ni watu wachache wa kidini ambao huchochewa kushiriki itikadi zao na wengine. Huenda wakafikiri kwamba yatosha tu kutii sheria za Kaisari, kuishi maisha ya adili, au kufanyia wengine vitendo vya fadhili. Hata hivyo, wao hawahisi wakiwajibika kusaidia wengine wajifunze kile ambacho Biblia husema juu ya kupata wokovu. Sisi tuko tofauti jinsi gani?
3 Huduma yetu ya bidii huwa tofauti kabisa na utendaji mbalimbali wa dini zile nyingine. Kwa zaidi ya miaka 100, Mashahidi wa siku ya kisasa wamehubiri habari njema kwa bidii hadi miisho ya dunia, wakiwaiga Wakristo wa mapema. Lengo letu la kufanya hivyo ni kuwasaidia watu wengi iwezekanavyo waishi kupatana na mapenzi ya Mungu.—1 Tim. 2:4; 2 Pet. 3:9.
4 Una Sifa Gani? Je, wajulikana kuwa mhubiri mwenye bidii wa Neno la Mungu? (Mdo. 17:2, 3; 18:25) Kwa sababu ya kuhubiri kwako, je, jirani zako huona mara moja tofauti kati ya dini yao na dini yako? Je, wajulikana kuwa mtu apendaye kushiriki tumaini lako na wengine? Je, wewe hushiriki katika huduma kwa ukawaida? Kumbuka kwamba sisi hujitofautisha kwa jina letu na vilevile kwa kufanya yale ambayo jina hilo hufafanua—kutoa ushahidi juu ya Yehova.—Isa. 43:10.
5 Upendo kwa Mungu na kwa jirani zetu hutuchochea tuhubiri. (Mt. 22:37-39) Ndiyo sababu, kama vile Yesu na mitume, twataka kutumia ifaavyo kila fursa ya kushiriki ujumbe wa Ufalme na wengine. Na tuendelee kwa bidii kuhubiria wale walio tayari kusikiliza habari njema. Kufanya hivyo kutasaidia watu wenye mioyo minyofu ‘waone tofauti kati ya . . . yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.’—Mal. 3:18.