Ni Nani Ambaye Huenda Akakubali Funzo la Biblia?
1 Nabii Amosi alitangaza kwamba kungekuwa na njaa katika nchi ya Israeli, “njaa . . . si njaa ya kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya kukosa kuyasikia maneno ya BWANA.” (Amo. 8:11) Kwa manufaa ya wale wenye njaa na kiu ya kiroho, tengenezo la Yehova linagawanya fasihi nyingi sana za Biblia ulimwenguni pote.
2 Kufikia sasa, tumechapisha nakala milioni 70 za kitabu Ujuzi na nakala milioni 91 za broshua Anataka. Twathamini usahili na uwezo wa vichapo hivi katika kufundisha kweli. Hata hivyo, kwa hakika, umati wa watu ambao wamepokea fasihi zetu hawajapata kujifunza Biblia nasi. Twaweza kufanya nini kuhusu jambo hilo?
3 Kila Kichapo Unachoangusha Chaweza Kuongoza Kwenye Funzo! Ebu fikiria jambo lililoonwa la mhubiri mmoja aliyejitolea kujifunza na mwanamke fulani mara ya kwanza alipoongea naye mlangoni pake. Alikubali mara moja. Baadaye alimwambia hivi, “Wewe ndiwe mtu wa kwanza kujitolea kujifunza Biblia nami.” Katika eneo lako, ni watu wangapi ambao tayari wana fasihi zetu na ambao huenda wakasema vivyo hivyo? Kila kichapo unachoangusha chaweza kutokeza fursa ya ziara za kurudia na funzo la Biblia la nyumbani.
4 Kwa kuwa mara nyingi sisi hukutana na watu ambao tayari wana vichapo vyetu, twaweza kuchocheaje kupendezwa kwao kujifunza yale ambayo yamo katika fasihi zetu? Shahidi mmoja alimwuliza mwenye nyumba moja kwa moja kama alikuwa na maswali yoyote ya Biblia, lakini akasema, “La.” Dada huyo alisisitiza, “Hapana shaka una maswali.” Mwanamke huyo alikuwa na maswali, na funzo likaanzishwa. Kwa nini usimwulize mwenye nyumba kama angependa kujifunza maoni ya Biblia juu ya swali au jambo linalomhangaisha? Jitayarishe kuuliza swali lenye kupendeza kama hawezi kufikiri juu ya jambo fulani. Mazungumzo kama hayo yaweza kuandaa njia ya funzo la kawaida la kweli za msingi za Biblia.
5 Kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia ndiyo kiini cha huduma yetu. Kwa kuwa hatujui kamwe ni nani anayeweza kukubali funzo, usisite kutoa fursa ya funzo kwa yeyote unayekutana naye. Sali kwa Yehova kuhusu jambo hilo, nawe utende kulingana na sala zako. Huenda karibuni mtu fulani utakayejitolea kujifunza naye akakubali funzo!—1 Yoh. 5:14, 15.