Baraka ya Yehova Hututajirisha
1 Mara nyingi, mafanikio ya mtu hupimwa kwa mshahara wake. Ndiyo sababu watu wengi huona wale walio na pesa kuwa watu wenye furaha zaidi na wenye kuridhika zaidi. Hata hivyo, watu ambao huhisi kwamba pesa zaweza kununua furaha wamekosea sana. (Mhu. 5:12) Hakuna shangwe yenye kudumu kwa wale “waazimiao kuwa matajiri” kimwili. (1 Tim. 6:9) Kinyume cha hilo, watumishi wa Yehova wana shangwe kwelikweli na ni watu matajiri zaidi ulimwenguni. (Mit. 10:22; Ufu. 2:9) Jinsi gani?
2 Uthibitisho wa Utajiri Wetu: Sisi tuna ufahamu wa kiroho wenye kina na uelewevu wa Neno la Mungu, Biblia. Kupitia tengenezo lake la kidunia, Yehova huendelea kutufundisha juu yake mwenyewe na Mwanaye, ili tunufaike kabisa. Uelewevu sahihi hutuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova. (Yak. 4:8) Kutambua lililo jema na lililo baya na kufuata sheria za Mungu hutulinda na maradhi na hatari fulani-fulani. Tuna uhakika kwamba Yehova atatuandalia, tupate uradhi wa kimungu na amani ya akili.—Mt. 6:33.
3 Twafurahia amani na umoja miongoni mwa udugu wetu wa kiroho kwa sababu ya kusitawisha matunda ya roho ya Mungu. Tukiwa tumeunganishwa na kifungo chenye nguvu cha upendo, hatuhitaji kuhisi tumeachwa na Mungu au na ndugu zetu maafa yanapotupata.—Gal. 6:10.
4 Maisha yetu yana maana na kusudi halisi. Twaliona kuwa pendeleo kubwa ajabu kushiriki katika kuhubiri habari njema ulimwenguni pote. Hiyo hutuletea shangwe tunaposaidia watu wengine wawe na uhusiano mzuri pamoja na Mungu na kutumikia kwa umoja pamoja nasi katika ibada safi. Hazina yetu yenye thamani ya huduma humletea Yehova heshima na kutupa uradhi wa kuchangia kulitakasa jina lake. Twadumisha mtazamo ufaao wa akilini, tukijua kwamba tumaini letu la wakati ujao litatimizwa hivi karibuni.
5 Kuonyesha Uthamini Wetu: Sikuzote na tuthamini baraka za Yehova, ambazo hutufanya tuwe watu matajiri zaidi ulimwenguni. (Mit. 22:4) Kwa kutafakari kila siku yale tuliyo nayo sisi huchochewa kumshukuru Yehova kwa upendo wake mkarimu na kuendelea kumpa ujitoaji wetu usiohusisha mwingine.