Tumia Matukio ya Sasa Kuamsha Upendezi
1 Je, ungependa kuwa na njia nyingi mbalimbali zitakazofanya huduma yako ivutie na kuamsha upendezi wa watu kwa ujumbe wa Biblia? Basi tumia matukio yanayotokea ulimwenguni na katika jumuiya yako ili kuanzisha mazungumzo. Unaweza kutaja matukio ya sasa ya kwenu na ya taifa au jambo lililotajwa katika habari za kimataifa. Matukio hayo hubadilika sikuzote. (1 Kor. 7:31) Angalia mifano ifuatayo.
2 Matatizo ya kiuchumi na gharama za juu za maisha ni mambo yanayohangaisha watu kwelikweli. Hivyo, unaweza kusema:
◼ “Je, ulisikia katika habari [taja jambo] vitu vimepanda bei tena?” Au unaweza kutaja juu ya kukosa kazi ya kuajiriwa ikiwa kampuni kubwa imefuta wafanyakazi wengi. Ikitegemea jinsi unavyotaka kuendeleza mazungumzo, unaweza kufuatia kwa kuuliza “Je, umepata kujiuliza kwa nini ni vigumu sana kutafuta riziki?” au “Je, wafikiri kwamba sikuzote itakuwa vigumu kuandaa riziki?”
3 Ripoti za jeuri, kama vile jambo la kuhuzunisha sana miongoni mwa familia au wanafunzi wa shule, huandaa msingi wa mazungumzo mengine. Waweza kuuliza:
◼ “Je, ulisoma katika gazeti kwamba [taja msiba uliotokea katika jumuiya]?” Kisha uliza “Unafikiri ni nini kinachosababisha jeuri nyingi hivyo ulimwenguni?” au “Je, wafikiri kutakuwa na wakati tutakapohisi tukiwa salama?”
4 Habari za mafuriko yenye kuangamiza, matetemeko ya dunia, au ghasia za kiraia katika sehemu mbalimbali za ulimwengu pia hutoa habari inayochochea kupendezwa. Kwa mfano, unaweza kuuliza:
◼ “Je, Mungu ndiye mwenye kusababisha [taja msiba wa asili]?” Au unaweza kutaja ghasia za kiraia za karibuni na kusema hivi: “Ikiwa kila mtu anataka amani, kwa nini ni vigumu kuipata?”
5 Kaa chonjo kwa matukio ya sasa ambayo unaweza kutumia katika utangulizi wako. Madokezo yanayoweza kusaidia yanapatikana chini ya “Matukio ya Sasa,” kwenye ukurasa wa 12 wa kitabu Kutoa Sababu. Hata hivyo, epuka kuunga mkono masuala ya kisiasa au ya kijamii. Badala yake, elekeza fikira kwenye Maandiko na Ufalme wa Mungu kuwa ndio suluhisho pekee la daima kwa matatizo ya wanadamu.