Iweke Vizuri
Madokezo ya Utoaji wa Utumishi wa Shambani
Jinsi ya Kutumia Nyongeza Hii
Baadhi ya utoaji mbalimbali ulio hapa ulikuwa katika matoleo ya zamani ya Huduma Yetu ya Ufalme. Jaribu kutumia utoaji mbalimbali katika utendaji wako, na uone utapata matokeo gani. Weka nyongeza hii vizuri, na uirejezee unapojitayarisha kwenda katika huduma.
Huenda ukamvutia mtu apendezwe na Neno la Mungu ukisema kifupi. Uliza swali fulani, kisha tumia Andiko kumjibu kifupi. Unaweza kujaribu madokezo haya:
“Unapofikiria kuhusu wakati ujao, je, una tumaini au shaka? [Ngoja ajibu.] Biblia ilitabiri matukio yenye kubabaisha tunayoona leo na pia matokeo yake.”—2 Tim. 3:1, 2, 5; Mit. 2:21, 22.
“Leo watu wanahangaikia sana mambo ya afya. Je, ulijua kwamba Mungu ameahidi kuondoa kabisa matatizo ya afya?” —Isa. 33:24; Ufu. 21:3, 4.
“Je, ulijua kuwa Biblia hutabiri kwamba hatimaye kutakuwa na serikali moja tu itakayotawala ulimwenguni pote?”—Dan. 2:44; Mt. 6:9, 10.
“Wafikiri hali zingekuwaje kama Yesu Kristo angetawala dunia?”—Zab. 72:7, 8.
“Watu wengi hubaguliwa kwa sababu ya jinsia yao, dini, na rangi ya ngozi yao. Wafikiri Mungu huonaje ubaguzi huo?”—Mdo. 10:34, 35.
“Twajua kuwa Yesu Kristo alifanya miujiza mingi katika siku yake. Ikiwa ungemwomba afanye mwujiza mwingine tena, ungetaka afanye mwujiza gani?”—Zab. 72:12-14, 16.
“Watu wengi wamechoka kusikia juu ya matatizo. Wanataka kusikia juu ya utatuzi. Lakini tutapata wapi utatuzi wa kweli wa matatizo yetu?”—2 Tim. 3:16, 17.
“Je, waweza kufafanua Ufalme ambao wewe huomba uje katika ile Sala ya Bwana (au, Baba Yetu)?”—Ufu. 11:15.
Vianzisha-Mazungumzo
Orodha ya maswali yaliyo chini, ambayo yamekusanywa kutoka katika kitabu Kutoa Sababu, yaonyesha ukurasa ambapo kila jibu lapatikana:
Kwa nini tunazeeka na kufa? (100)
Ni nini iliyo hali ya wafu? (101)
Je! kuna sababu timamu za kuitikadi kwamba kuna Mungu? (218)
Je! Mungu kweli anajali yanayotupata sisi wanadamu? (219)
Je! Mungu ni mtu halisi? (220)
Je! watu wema wote wanaenda mbinguni? (189)
Je! ni lazima mtu aende mbinguni ili awe na wakati ujao wenye furaha kwelikweli? (190)
Kwa nini ni jambo la maana kujua na kutumia jina la kibinafsi la Mungu? (425)
Je! Yesu Kristo ni Mungu? (430)
Ufalme wa Mungu utatimiza nini? (327)
Ni nini lililo kusudi la uhai wa kibinadamu? (341)
Ni nini kinachoweza kusaidia ndoa iwe bora? (246)
Je! dini zote zinakubaliwa na Mungu? (67)
Mtu awezaje kujua ni ipi iliyo dini ya kweli? (73)
Shetani ni mtu mwenye nguvu jinsi gani katika ulimwengu wa leo? (287)
Sababu gani Mungu anaruhusu kuteseka? (132)
Kwa nini kuna uovu mwingi sana? (369)
Ni nani anayetawala ulimwengu huu—Mungu au Shetani? (359)
Madokezo ya Namna ya Kutoa Broshua Anataka
“Labda utakubali kwamba watu wengi humwamini Mungu. Wote wanaomwamini hukubali kwamba Mungu hutaka tufanye jambo fulani. Lakini watu wana maoni tofauti kuhusu yale ambayo Mungu anataka tufanye.” Kisha mtolee broshua Anataka, fungua somo la 1, na mlizungumzie.
“Kwa kuwa familia zina matatizo mengi leo, je, umewahi kujiuliza ni nini siri ya kupata furaha ya familia?” Baada ya kumngoja ajibu, mweleze kwamba katika Biblia, Mungu anafunua siri ya kupata furaha ya familia. Soma Isaya 48:17. Kisha fungua broshua Anataka, kwenye somo la 8 na umwonyeshe baadhi ya mistari ya Biblia iliyotajwa inayotoa mwongozo wenye kutegemeka kwa kila mshiriki wa familia. Soma maswali yanayopatikana mwanzoni mwa somo hilo. Mwulize kama angependa kusoma majibu.
“Broshua hii ina mafunzo yenye kuhusisha mambo mengi, yanayoshughulikia mafundisho ya msingi ya Biblia. Katika kila ukurasa, utapata majibu ya maswali ambayo yamewatatiza watu kwa karne nyingi. Kwa mfano, Mungu ana kusudi gani kuhusu dunia?” Fungua broshua hiyo kwenye somo la 5, na usome maswali yaliyo mwanzoni mwa somo. Mwulize mwenye nyumba ni swali gani linalompendeza zaidi, kisha usome fungu au mafungu yanayohusiana na swali hilo, mkichunguza maandiko yaliyotajwa. Eleza kwamba majibu yenye kuridhisha ya maswali mengine yanaweza kupatikana kwa urahisi tu kama jibu hilo. Dokeza urudi tena ili mzungumzie swali jingine.
“Unafikiri ni nini kinachosababisha jeuri shuleni? Je, ni kwa sababu wazazi hawawafundishi watoto wao? Au je, inaweza kuwa ni kwa sababu nyingine, kama vile uvutano wa Ibilisi?” Mwache ajibu. Akisema ni kwa sababu ya uvutano wa Ibilisi, soma Ufunuo 12:9, 12. Mwonyeshe jinsi Ibilisi anavyochochea msukosuko ulimwenguni. Kisha fungua broshua Anataka kwenye somo la 4, na umwulize kama amewahi kujiuliza Ibilisi alitoka wapi. Soma na uzungumzie mafungu mawili ya kwanza. Akisema kuna jeuri shuleni “kwa sababu wazazi hawawafundishi watoto wao,” soma 2 Timotheo 3:1-3 na umweleze tabia ambazo huchochea tatizo hilo. Kisha fungua broshua Anataka kwenye somo la 8, soma fungu la 5, na uendelee na mazungumzo.
“Unafikiri ni jambo la akili kutazamia Muumba atupatie ujuzi tunaohitaji ili kufanikisha maisha ya familia?” Baada ya kumngoja ajibu, mwonyeshe broshua Anataka. Fungua somo la 8, na ueleze kwamba lina kanuni za Biblia zinazohusu kila mshiriki wa familia. Jitolee kumwonyesha jinsi ya kutumia broshua hiyo pamoja na Biblia ili apate manufaa zaidi.
“Kwa kuwa tunakabili matatizo mengi siku hizi, je, wafikiri sala yaweza kweli kutusaidia? [Ngoja ajibu.] Wengi husema kwamba sala huwapa nguvu. [Soma Wafilipi 4:6, 7.] Hata hivyo, huenda mtu akahisi kwamba sala zake hazijibiwi. [Fungua broshua Anataka kwenye somo la 7.] Broshua hii yaeleza jinsi sala yaweza kutufaidi sana.”
“Tumekuwa tukiongea na jirani zetu kuhusu sababu ya kuwapo kwa dini nyingi tofauti ulimwenguni ilhali kuna Biblia moja tu. Kwa maoni yako, kwa nini kuna mvurugo huo wa dini? [Ngoja ajibu. Fungua broshua Anataka kwenye somo la 13, na usome maswali ya kwanza.] Utapata majibu yenye kuridhisha kwa maswali hayo ukisoma somo hili.”
Baada ya kumwachia mtu magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, mwulize kama unaweza kumsomea fungu moja fupi. Akikubali, fungua broshua Anataka kwenye somo la 5. Mtajie maswali yaliyo mwanzoni mwa somo, na umwombe asikilize jibu wakati unaposoma fungu la kwanza. Baada ya kusoma fungu, mwulize swali hilo, na usikie jibu lake. Mtolee broshua, akiikubali, panga umrudie ili upate majibu yake kwa maswali mawili yanayofuata.
Madokezo ya Kutoa Kitabu Ujuzi
Ukiwa umeshika Biblia, anza kwa kusema: “Tunamsomea kila mtu andiko moja hapa kwenu leo. Lasema hivi . . .” Soma Yohana 17:3, kisha uulize: “Je, umeona tunaahidiwa nini tukiwa na ujuzi unaofaa? [Ngoja ajibu.] Mtu anaweza kupata wapi ujuzi huo?” Akijibu, mwonyeshe kitabu Ujuzi, na umwambie: “Kitabu hiki kinazungumzia ujuzi unaoongoza kwenye uhai wa milele. Kinajibu maswali ya kawaida ambayo watu wanauliza kuhusu Biblia.” Mwonyeshe ukurasa wa yaliyomo, na umwulize kama amejiuliza yoyote ya maswali hayo.
“Je, umewahi kujiuliza kama kweli Mungu anajali kuhusu ukosefu wa haki na mateso tunayoona au tunayopata sisi wenyewe? [Ngoja ajibu.] Biblia hutuhakikishia kwamba Mungu anatupenda na kwamba atatusaidia nyakati za taabu.” Soma Zaburi 72:12-17. Fungua kitabu Ujuzi sura ya 8, na ueleze kwamba kinatoa jibu lenye kutia moyo kwa swali ambalo mamilioni ya watu wameuliza, Sababu gani Mungu huruhusu kuteseka? Ikiwezekana, zungumzieni baadhi ya Maandiko yaliyo kwenye fungu la 3 hadi 5, au ufanye hivyo unapomrudia.
“Wengi wetu tumefiwa. Je, umewahi kujiuliza kama tutawaona wapendwa wetu tena? [Ngoja ajibu.] Yesu alionyesha kwamba wapendwa wetu wanaweza kukombolewa kutoka katika kifo. [Soma Yohana 11:11, 25, 44.] Hata ingawa alisema hivyo karne nyingi zilizopita, hiyo yaonyesha yale ambayo Mungu ameahidi kutufanyia.” Fungua kitabu Ujuzi kwenye picha iliyo katika ukurasa wa 85, na usome maelezo yaliyo juu ya picha. Kisha mwonyeshe picha iliyo kwenye ukurasa wa 86, na utoe maelezo. Weka msingi wa mazungumzo ya ziara ijayo kwa kuuliza: “Ungependa kujua sababu gani wanadamu wanazeeka na kufa?” Rudi ili mzungumzie sura ya 6.
“Je, umewahi kufikiri ni kwa nini wanadamu wanatamani kuishi muda mrefu zaidi?” Baada ya jibu lake, fungua kitabu Ujuzi sura ya 6, na usome fungu la 3. Zungumzia maandiko yaliyotajwa. Soma yale maswali mawili mwishoni mwa fungu, kisha umwulize kama angependa kujua majibu. Akikubali, zungumzieni mafungu machache yafuatayo.
“Tunawauliza watu kama wanaamini jambo hili . . .” Soma Mwanzo 1:1, kisha uulize: “Je, wakubaliana na maneno hayo?” Mwenye nyumba akikubali, mwambie: “Mimi pia nakubaliana nayo. Hata hivyo, je, wafikiri kwamba kwa kuwa Mungu ndiye aliyeumba vitu vyote, yeye ndiye wa kulaumiwa kwa sababu ya uovu uliopo?” Baada ya kumshukuru kwa jibu lake, soma Mhubiri 7:29. Fungua kitabu Ujuzi sura ya 8, na usome fungu la 2. Ikiwa hakubaliani na Mwanzo 1:1, mwombe achunguze uthibitisho unaoonyesha kwamba kuna Muumba.—Ona kitabu Kutoa Sababu, ukurasa wa 397-399.
“Je, hukubali kwamba kwa kuwa leo maadili yanaendelea kubadilika haraka, twahitaji mwongozo unaotegemeka maishani? [Ngoja ajibu.] Ijapokuwa Biblia ni kitabu cha kale zaidi ya vitabu vyote, hiyo hutupatia ushauri kuhusu maisha ya siku hizi na vilevile jinsi ya kuwa na maisha ya familia yenye furaha.” Fungua kitabu Ujuzi sura ya 2, na usome fungu la 10 na sentensi ya kwanza ya fungu la 11, kutia ndani 2 Timotheo 3:16, 17.
“Je, ungetaka kujua wakati ujao utakuwaje kwetu na kwa dunia hii? [Ngoja ajibu.] Biblia huonyesha kwamba kutakuwa na Paradiso wakati ujao! Hapo ndipo Mungu aliwaweka wenzi wa kwanza alipowaumba. Ona jinsi ilivyokuwa.” Fungua kitabu Ujuzi kwenye ukurasa wa 8, na usome fungu la 9, chini ya kichwa kidogo “Uhai Katika Paradiso.” Kisha zungumzia mambo yaliyo katika fungu la 10, na usome andiko lililotajwa hapo, Isaya 55:10, 11. Endeleza mazungumzo kuhusu jinsi maisha yatakavyokuwa katika Paradiso, mkisoma fungu la 11-16.
Unapowarudia wale ambao uliwaachia magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! waweza kusema hivi:
“Nilipokuwa hapa mara ya mwisho, nilikuachia gazeti la Mnara wa Mlinzi. Labda uligundua kwamba kichwa chote cha gazeti hilo ni Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Leo ningetaka kukueleza kuhusu Ufalme wenyewe na kile ambacho Ufalme huo unaweza kukufanyia wewe na familia yako.” Kisha fungua broshua Anataka kwenye somo la 6, usome na kulizungumzia kulingana na nafasi ya mtu huyo.
“Hivi majuzi nilipokutembelea, nilikuachia magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Magazeti hayo yanatia watu moyo waheshimu Biblia na mwongozo wake wa maadili. Kwa kuwa naona ni muhimu kila mtu aelewe Neno la Mungu, nimerudi ili nikuonyeshe jambo fulani litakalokusaidia ufanye hivyo.” Toa broshua Anataka au kitabu Ujuzi, na umweleze juu ya funzo la Biblia.
Unapotoa kitabu chochote cha zamani chenye kurasa 192, unaweza kujaribu kusema hivi:
“Watu wamekazia sana uhitaji wa elimu bora. Kwa maoni yako, ni elimu ya aina gani ambayo mtu anapaswa kufuatia ili ahakikishe kwamba atapata furaha na mafanikio mengi maishani? [Ngoja ajibu. Kisha soma Mithali 9:10, 11.] Kitabu hiki [taja kichwa cha kitabu unachotoa] kinazungumzia habari ya Biblia. Kinaonyesha aina moja tu ya ujuzi ambao unaweza kuongoza kwenye uhai udumuo milele.” Mwonyeshe picha fulani katika kitabu, na umtie moyo akisome.
Vichapo Vingine
Madokezo ya namna ya kutoa vitabu na broshua nyingine yanaweza kupatikana katika kitabu Watch Tower Publications Index chini ya:
Presentations
List by Publication
Njia ya Moja kwa Moja
Ili kuanzisha funzo la Biblia, jaribu kutumia mojawapo ya njia hizi za moja kwa moja:
“Je, ulijua kwamba kwa dakika chache tu, unaweza kupata jibu la swali muhimu katika Biblia? Kwa mfano, . . .” Kisha uliza swali linalopatikana mwanzoni mwa mojawapo ya masomo katika broshua Anataka unalofikiri kwamba litampendeza.
“Nimerudi ili nikuonyeshe utaratibu wetu wa funzo la Biblia bila malipo. Itachukua muda wa dakika tano tu kukuonyesha. Unaweza kupata dakika tano?” Akikubali, tumia somo la 1 katika broshua Anataka umwonyeshe jinsi ya kujifunza, ukisoma andiko moja au mawili tu uliyochagua. Baadaye, mwulize hivi: “Ni lini utakapokuwa na nafasi ya dakika 15 hivi ili tujifunze somo lifuatalo?”
“Watu wengi wana Biblia, lakini hawatambui kwamba ina majibu ya maswali yetu muhimu kuhusu wakati wetu ujao. Ukijifunza kichapo hiki [broshua Anataka au kitabu Ujuzi] kwa muda wa saa nzima kila juma, unaweza kuelewa mambo ya msingi ya Biblia kwa miezi michache tu. Ningependa kukuonyesha jinsi ya kufanya hivyo.”
“Nimekutembelea ili nikupe fursa ya kuwa na funzo la Biblia nyumbani bila malipo. Ukiniruhusu, ningependa kutumia dakika chache tu kukuonyesha jinsi watu katika nchi 200 hivi wanavyojifunza Biblia nyumbani mwao wakiwa familia. Twaweza kutumia habari zozote zilizopo katika kichapo hiki kama msingi wa mazungumzo yetu. [Mwonyeshe ukurasa wa yaliyomo katika kitabu Ujuzi.] Ni habari gani hasa unayopendezwa nayo?” Ngoja achague. Fungua sura aliyochagua, na mwanze kujifunza fungu la kwanza.
“Mimi hufunza watu Biblia bila kulipisha chochote na nina nafasi nyingine ya wanafunzi wa ziada. Kichapo hiki ndicho tunachotumia kujifunza Biblia. [Mwonyeshe kitabu Ujuzi.] Masomo hayo huchukua miezi michache tu na hutoa majibu ya maswali kama: Sababu gani Mungu huruhusu kuteseka? Sababu gani tunazeeka na kufa? Inakuwaje kwa wapendwa wetu waliokufa? Na twawezaje kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu? Nikuonyeshe jinsi tunavyojifunza?”
Ukipata utoaji wenye mafanikio ambao unaamsha kupendezwa, endelea kuutumia! Upatanishe tu na toleo la kichapo cha mwezi huo.