Mavazi Yenye Mpangilio Mzuri Humstahi Mungu
1 Hivi karibuni tutakuwa na pendeleo la kuwa wageni wa Yehova kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Mtukuzeni Mungu” la mwaka wa 2003. Tunamshukuru Yehova kama nini kwa sababu ya kutualika kwenye karamu hiyo nono ya kiroho! Twaweza kuonyesha kwa mavazi na mapambo yetu kwamba tunamstahi yeye na tunathamini maandalizi yake ya kiroho.—Zab. 116:12, 17.
2 Safi na Nadhifu: Sura yetu inapasa kuonyesha kwamba tunatii kanuni za Mungu wetu, ambaye ni safi na mwenye utaratibu. (1 Kor. 14:33; 2 Kor. 7:1) Mwili wetu, nywele, na kucha zapasa kuwa safi, nasi twapaswa kuwa nadhifu. Watu wengi huvalia kizembe siku hizi. Hata hivyo, Mkristo hapaswi kuvalia kizembe eti kwa sababu tu mwigizaji mashuhuri wa sinema au bingwa wa michezo anavalia kizembe. Tukiiga mitindo inayopendwa na wengi, huenda watu wasione tofauti kati ya wale wanaomtumikia Mungu na wale wasiomtumikia.—Mal. 3:18.
3 Mavazi Yanayowafaa Wahudumu Wakristo: Mtume Paulo alipomwandikia mwangalizi Mkristo Timotheo, aliwatia moyo “wanawake wajirembe wenyewe katika mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, . . . katika njia inayofaa wanawake wanaodai kumstahi Mungu, yaani, kupitia kazi zilizo njema.” (1 Tim. 2:9, 10) Twahitaji kufikiria kwa makini ili kuhakikisha kwamba mavazi yetu yana mpangilio mzuri. Mavazi yetu yapaswa kuwa nadhifu, safi na yenye kiasi, wala si yenye kupita kiasi, yenye kuamsha ashiki, au yenye kuudhi.—1 Pet. 3:3.
4 Paulo alionya pia juu ya kupita kiasi katika “mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mvao ulio ghali sana.” (1 Tim. 2:9) Ni jambo la hekima kwa wanawake Wakristo kuwa na kiasi wanapotumia vito, virembeshi na mapambo mengine.—Mit. 11:2.
5 Kanuni za shauri ambalo Paulo aliwapa wanawake Wakristo zinawahusu pia wanaume Wakristo. Akina ndugu wanapaswa kuepuka mitindo ya ulimwengu. (1 Yoh. 2:16) Kwa mfano, katika nchi fulani, mavazi makubwa-makubwa (baggy) yanapendwa sana, lakini mtindo huo haumfai mhudumu wa Mungu.
6 Wakati wa Starehe: Ndugu na dada wengi huweka kielelezo chema kuhusiana na mavazi na mapambo wanapohudhuria kusanyiko. Hata hivyo, ripoti zinaonyesha kwamba wengine huvalia kiholela-holela wanaposafiri kuelekea na kutoka kusanyikoni au wanapostarehe baada ya kusanyiko. Kwa kweli, mavazi na mapambo yetu—iwe ni wakati wa kusanyiko au wakati mwingine—huathiri jinsi wengine wanavyowaona watu wa Mungu. Kwa kuwa sisi huvaa beji za kusanyiko, sikuzote twapaswa kuvalia kwa njia inayowafaa wahudumu Wakristo. Mara nyingi hilo huwafanya wengine watusifu na hutokeza nafasi ya kuhubiri.—1 Kor. 10:31-33.
7 Kama vile tu tabasamu ya kirafiki inavyofanya uso wetu uvutie, ndivyo na mavazi na mapambo yenye mpangilio mzuri yanavyofanya ujumbe wetu na tengenezo letu liheshimiwe. Baadhi ya watu watakaotuona wakati wa Makusanyiko ya Wilaya ya “Mtukuzeni Mungu” mwaka huu, huenda wakataka kujua ni kwa nini sisi tuko tofauti na huenda wakasema hivi hatimaye: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia [na kuona] kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” (Zek. 8:23) Kila mmoja wetu na amstahi Yehova kwa mavazi na mapambo yake.
[Maswali ya Funzo]
1. Twawezaje kuonyesha kwamba tunathamini kusanyiko letu la wilaya linalokuja?
2. Kwa nini ni muhimu tuwe safi na nadhifu?
3. Tunawezaje kuhakikisha kwamba sura yetu inapatana na shauri la 1 Timotheo 2:9, 10?
4, 5. Wanaume na wanawake Wakristo wanapaswa kutii maonyo gani?
6. Kwa nini twapaswa kudumisha viwango vya juu vya mavazi na mapambo tunaposafiri kuelekea na kutoka kusanyikoni, tunapokuwa kusanyikoni, na baada ya vipindi vya kila siku?
7. Mavazi yetu yenye mpangilio mzuri yanaweza kuwa na matokeo gani kwa wengine?
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Vaa na Kujipamba kwa Heshima
▪ Unaposafiri
▪ Unapokuwa kusanyikoni
▪ Unapostarehe