Tumekabidhiwa Habari Njema
1 Tuna pendeleo kubwa sana la kukabidhiwa habari njema za Mungu! (1 The. 2:4) Huenda watu fulani wakakataa ujumbe huo wenye nguvu lakini wale walio wanyofu huvutiwa nao kama wanavyovutiwa na harufu nzuri. (2 Kor. 2:14-16) Wale wanaokubali na kutii habari njema watapata wokovu. (Rom. 1:16) Tunapaswa kufanya nini na habari njema tulizokabidhiwa?
2 Yesu na Mitume: Yesu alitanguliza kazi ya kutangaza habari njema. (Luka 4:18, 43) Aliwapenda watu na kuuthamini sana ujumbe huo hivi kwamba aliwahubiria wengine hata alipokuwa mchovu na mwenye njaa. (Marko 6:30-34) Kwa maneno yake na mfano wake, aliwaonyesha wanafunzi wake umuhimu wa kazi ya kuhubiri habari za Ufalme.—Mt. 28:18-20; Marko 13:10.
3 Mitume walimwiga Yesu kwa kuhubiri kwa bidii ujumbe wa Ufalme. Hata walipopigwa na kuagizwa wakome kuhubiri, ‘waliendelea kufundisha na kutangaza habari njema bila kuacha.’ (Mdo. 5:40-42) Mtume Paulo alifanya kazi hiyo kwa bidii bila kuacha. (1 Kor. 15:9, 10; Kol. 1:29) Aliona pendeleo la kuhubiri habari njema kama deni ambalo alidaiwa na wanadamu wenzake, na alikuwa tayari kujinyima ili alipe deni hilo.—Mdo. 20:24; Rom. 1:14-16.
4 Pendeleo Letu Leo: Kuthamini kazi takatifu tuliyokabidhiwa kutatuchochea tutafute njia za kuongeza huduma yetu. (Rom. 15:16) Edward aliyetumia kiti cha magurudumu, alikuwa akiketi karibu na lango la hoteli moja na kuwahubiria wageni waliokuja humo imani yake. Hata hivyo, alitamani kuongeza huduma yake kwa hiyo akaomba atengenezewe gari lenye chumba sehemu ya nyuma. Kwa miaka mingi, alifanya upainia akisafiri sehemu za mbali sana kwa gari hilo. Wengi leo wamefanya mabadiliko maishani mwao kama Edward ili washiriki zaidi katika kazi ya kueneza habari njema.
5 Na tumwige Yesu na mitume kwa kuendelea kutanguliza kazi ya kuhubiri maishani mwetu. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunawapenda watu na tunathamini habari njema tulizokabidhiwa.