Msifu Yehova kwa Kutoa Ushahidi Kila Unapopata Nafasi
1 Watumishi waaminifu wa Yehova wanatafuta nafasi ya kumsifu kila siku. (Zab. 96:2, 3; Ebr. 13:15) Tunaweza kumsifu Yehova kwa kutoa ushahidi kila tunapopata nafasi. Waabudu wengi wa Yehova leo wanashukuru kwamba mtu fulani aliwatolea ushahidi kuhusu Ufalme nafasi ilipotokea.
2 Kumtolea mtu mmoja ushahidi nafasi inapotokea, mara nyingi huwawezesha wengine kusikia ujumbe wa Ufalme. Kwa mfano, mazungumzo ya Yesu pamoja na mwanamke Msamaria kwenye kisima cha Yakobo yalifanya wengi wapendezwe na habari njema. (Yoh. 4:6-30, 39-42) Paulo na Sila walipokuwa wamefungwa gerezani huko Filipi, walimtolea mlinzi wa gereza ushahidi, na watu wote wa nyumba yake wakakubali kweli.—Mdo. 16:25-34.
3 Nafasi Mbalimbali: Wewe una nafasi gani za kutoa ushahidi? Baadhi ya wahubiri wanatoa ushahidi wanapokwenda dukani au sokoni, wanaposafiri kwa magari ya umma, au wanapongoja kumwona daktari. Wengine wanapata nafasi ya kutoa ushahidi wakati wa mapumziko wakiwa kazini au shuleni. Kuweka mojawapo ya vitabu au magazeti yetu ya Biblia mahali yanapoonekana, huenda kukawafanya watu watuulize maswali kuhusu imani yetu.—1 Pet. 3:15.
4 Jinsi ya Kuanza: Msichana mmoja, mwenye umri wa miaka saba, ambaye ana haya alisikia mikutanoni kwamba ni muhimu kuwahubiria watu wote. Kwa hiyo alipojitayarisha kwenda dukani na mama yake, aliweka broshua mbili katika mkoba wake. Mama yake alipokuwa akilipa, msichana huyo alimwonyesha mwanamke fulani broshua. Mwanamke huyo aliikubali broshua kwa furaha. Alipoulizwa jinsi alivyopata ujasiri wa kuongea na mwanamke huyo, msichana huyo mwenye haya alijibu hivi: “Nilisema tu, Moja, Mbili, Tatu, na nikaenda!”
5 Tukiwa na nia kama ya huyo msichana mdogo, sote tutahubiri kila tunapopata nafasi. Ni nini kinachoweza kutusaidia? Omba Mungu upate ujasiri wa kusema. (1 The. 2:2) Tayarisha swali au maelezo kuhusu habari inayopendeza ambayo utaweza kutumia kuanzisha mazungumzo. Kisha uwe na hakika kwamba Yehova atabariki jitihada zako.—Luka 12:11, 12.
6 Kutumia kila nafasi tunayopata kuwatolea ushahidi watu tunaokutana nao kila siku, humletea Yehova sifa na hutuletea shangwe. Tunaweza kumsaidia mtu kupata tumaini la kuishi milele.