Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 8/03 kur. 3-5
  • Tudumishe Mahali Petu pa Ibada Katika Hali Nzuri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tudumishe Mahali Petu pa Ibada Katika Hali Nzuri
  • Huduma Yetu ya Ufalme—2003
  • Habari Zinazolingana
  • Mipango ya Mahali pa Ibada
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Je! Wewe Unastahi Jumba la Ufalme Lenu?
    Huduma Yetu ya Ufalme—1989
  • Hapa Ni Mahali Petu pa Ibada
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Tunaweza Kusaidiaje Kudumisha Jumba Letu la Ufalme?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
Pata Habari Zaidi
Huduma Yetu ya Ufalme—2003
km 8/03 kur. 3-5

Tudumishe Mahali Petu pa Ibada Katika Hali Nzuri

1 Ulimwenguni pote kuna zaidi ya makutaniko 94,000 ya Mashahidi wa Yehova. Makutaniko mengi hukutana ili kujifunza Biblia na kushirikiana na Wakristo wenzao katika Jumba la Ufalme, ambalo huwa kituo cha ibada safi.

2 Usafi Unaoratibiwa kwa Ukawaida: Kazi inayofanywa ili kudumisha Jumba la Ufalme ni sehemu muhimu ya utumishi wetu mtakatifu. Kitabu Huduma Yetu husema hivi katika ukurasa wa 61: “Ndugu wamepaswa walione kuwa pendeleo si kutoa tu michango ya kulipia gharama za Jumba la Ufalme, bali pia kujitolea walitunze kuwa safi, lenye kupendeza na katika hali nzuri. Jumba la Ufalme limepasa liwe mfano unaofaa wa tengenezo la Yehova, ndani na nje.” Kwa kuwa Jumba la Ufalme hutumiwa mara kadhaa kila juma, kuna uhitaji wa kulisafisha na kulidumisha kwa ukawaida. Kwa kawaida wajitoleaji kutoka katika kutaniko (au makutaniko) linalotumia Jumba la Ufalme hulitunza. Kama ilivyokuwa nyakati za Biblia, watumishi wa Yehova leo wanapaswa kuwa na bidii katika ‘kutengeneza na kufanya upya’ mahali petu pa ibada.—2 Nya. 34:10.

3 Ratiba ya usafi wa kila juma wa Jumba la Ufalme yapaswa kubandikwa kwenye ubao wa matangazo. Vikundi vyote vya mafunzo ya kitabu vyapaswa kuwa na zamu ya kusafisha jumba kila juma, vikifuata orodha ya mambo yanayopaswa kufanywa. Wote wanaoweza, wanapaswa kushiriki katika pendeleo hilo la kila juma la kulidumisha Jumba la Ufalme likiwa safi na lenye kupendeza. Watoto wanaweza kushiriki, wakiwa chini ya mwelekezo wa wazazi. Kufanya hivyo kutawafundisha watoto kuthamini pendeleo hilo. Hasa wakati ambapo Jumba la Ufalme linatumiwa na makutaniko kadhaa, ushirikiano mzuri ni wa lazima ili kazi hiyo muhimu ambayo ni sehemu ya ibada yetu, isifanywe na wachache tu.

4 Orodha ya mambo yanayopaswa kufanywa inaweza kubandikwa, labda mahali ambapo vifaa huwekwa. Orodha hiyo yapaswa kueleza mambo yanayohitaji kufanywa kila juma, kutia ndani kufagia, kusafisha madirisha, kupangusa meza, kutupa takataka, kupiga deki, na kuosha vioo. Huenda kazi nyingine zikahitaji kufanywa mara moja moja, kama vile kupiga rangi vyombo vya mbao na kusafisha kabisa viti, mapazia, na vifaa vya umeme. Kemikali zote zinazotumiwa kusafisha zapaswa kuwekwa mbali na watoto na zapaswa kuandikwa majina waziwazi. Maelezo mafupi kuhusu matumizi ya kila kemikali yapaswa kuonyeshwa.

5 Usalama katika Jumba la Ufalme ni muhimu sana. (Kum. 22:8) Kuhusiana na hilo, sanduku lililo hapa chini, linaorodhesha mambo yanayohitaji kuchunguzwa mara kwa mara ili aksidenti ziepukwe.

6 Kudumisha Jumba la Ufalme: Baraza la wazee lina daraka la kusimamia udumishaji wa Jumba la Ufalme. Kwa kawaida, mzee au mtumishi wa huduma hupewa mgawo wa kupanga kazi. Yeye hupanga shughuli za kila siku katika Jumba la Ufalme, akihakikisha kwamba linadumishwa likiwa safi na katika hali nzuri na kwamba kuna vifaa vya kutosha. Ni muhimu kuhakikisha kwamba hakuna hali zozote hatari ndani au nje ya jumba. Wakati ambapo makutaniko mawili au zaidi yanatumia jumba moja, mabaraza ya wazee huweka halmashauri ya udumishaji ili kufanya mipango ya kutunza jengo na uwanja. Halmashauri hiyo hufanya kazi chini ya mwelekezo wa mabaraza ya wazee.

7 Jumba la Ufalme hukaguliwa kikamili kila mwaka. Wazee hufanya mipango ya kutunza kikamili mambo yoyote yanayohitaji kushughulikiwa. Wahubiri wanaweza kuombwa wasaidie kufanya marekebisho yanayohitajiwa. Wote wanapaswa kuwa tayari kurekebisha hata mambo madogo-madogo na kushughulikia haraka mambo yanayohitaji uangalifu.

8 Ikiwa wazee wanahitaji shauri au msaada wa kudumisha Jumba la Ufalme, wanaweza kuwasiliana na Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa. Mashauri hayo yaweza kutia ndani mambo kama kurekebisha paa, kuta, sakafu, na kutatua matatizo ya unyevu katika jengo.

9 Kutumia Michango ya Kutaniko kwa Hekima: Kazi nyingi katika Jumba la Ufalme hufanywa na wajitoleaji. Jitihada zao za kujidhabihu huonyesha upendo na hupunguza sana gharama. Ikiwa ni lazima kutoa kandarasi ya kufanya kazi fulani, kama vile kuua wadudu wasumbufu, wazee wanapaswa kutafuta zabuni bora zaidi kwa ajili ya kazi hiyo. Wao hufanya hivyo kwanza kwa kutoa maelezo kamili kuhusu kazi inayohitaji kufanywa na vifaa vinavyohitajiwa. Wazabuni kadhaa hupewa nakala ya orodha hiyo ili wote watoe zabuni wakiwa na habari kamili. Baada ya kupokea zabuni zilizoandikwa kutoka kwa wazabuni kadhaa, wazee wanaweza kuchagua zabuni bora zaidi. Utaratibu huo unapaswa kufuatwa hata ikiwa ndugu amejitolea kufanya kazi hiyo au kuleta vifaa vinavyohitajiwa kwa bei hususa.

10 Wazee huchukua hatua zinazofaa ili kupata msamaha wa ushuru, mahali ambapo misamaha hiyo hutolewa. Maeneo ambayo kodi za uwanja na ushuru hutozwa, wazee wanapaswa kuhakikisha kwamba wanapata msamaha wa kutolipa ushuru au kodi kwa ajili ya Jumba la Ufalme. Mahali ambapo makutaniko kadhaa hutumia Jumba moja la Ufalme, halmashauri ya udumishaji huwa na akaunti yake na hujulisha kila baraza la wazee ripoti ya hesabu ya kila mwezi iliyoandikwa, na hivyo kuwataarifu wazee jinsi pesa zinavyotumiwa. Wazee wana jukumu la kuhakikisha kwamba pesa za kutaniko zinatumiwa ifaavyo.

11 Kazi Kubwa ya Udumishaji na Marekebisho: Halmashauri ya udumishaji inapoona kwamba jambo fulani kubwa lahitajiwa kuhusiana na shughuli au udumishaji wa Jumba la Ufalme, halmashauri hiyo huomba mwelekezo wa mabaraza ya wazee. Ikionekana kwamba kazi kubwa ya udumishaji au marekebisho itahitajiwa au kuna uhitaji wa msaada zaidi ya ule unaoweza kutolewa na makutaniko yanayotumia Jumba hilo la Ufalme, wazee watawasiliana na Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa. Ndugu hao wenye ujuzi na uzoefu hutoa madokezo na usimamizi mzuri katika kuongoza kazi. Ikiwa gharama kubwa yahusika, itakuwa lazima kupata makadirio sahihi ya gharama na kutayarisha azimio ili lipitishwe na kutaniko.—Ona Sanduku la Swali katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 1994.

12 Tunathamini kama nini pendeleo letu la kukutana pamoja katika Jumba la Ufalme! Hatungetaka kamwe kupuuza mikutano yetu. Wote wanaweza kuchangia mafanikio ya maandalizi hayo ya kututia moyo kwa kushiriki kikamili katika kulitunza Jumba letu la Ufalme. Kufanya hivyo hutukuza ibada safi na kufanya jina la Yehova liheshimiwe. Na tuazimie kudumisha mahali petu pa ibada katika hali nzuri.

[Maswali ya Funzo]

1. Jumba la Ufalme hutumiwa kwa kusudi gani?

2. Kwa nini ni muhimu kulidumisha Jumba la Ufalme likiwa safi na lenye kupendeza?

3. Usafi wa Jumba la Ufalme hupangwaje, na ni nani wanaoweza kushiriki pendeleo hilo?

4. Ni nini kinachopaswa kufanywa ili kutaniko lijue mambo ya kufanya wakati wa kusafisha Jumba la Ufalme?

5. Usalama ni muhimu kadiri gani, na ni mambo gani yanayohitaji kuchunguzwa mara kwa mara? (Ona sanduku lililo hapa chini.)

6. Kazi ya kudumisha Jumba la Ufalme hupangwaje?

7. (a) Ni nini hufanywa kila mwaka ili kuhakikisha kwamba Jumba la Ufalme linadumishwa katika hali nzuri? (b) Ni mambo gani yanayohitaji kuangaliwa mara kwa mara? (Ona sanduku upande wa kulia.)

8. Wazee wanaweza kuwasiliana na Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa kuhusiana na udumishaji wakati gani?

9. Ni utaratibu gani unaopaswa kufuatwa ikiwa kuna uhitaji wa kutoa kandarasi?

10. Ni nini hufanywa ili kuhakikisha kwamba pesa za kutaniko zinatumiwa ifaavyo?

11. Ni nini kinachopaswa kufanywa ikiwa kazi kubwa ya udumishaji au marekebisho inahitajiwa?

12. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini pendeleo letu la kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme?

[Sanduku katika ukurasa wa 4]

Orodha ya Usalama

◻ Vizima-moto vyapaswa kukaguliwa kila mwaka na kuwa mahali vinapoweza kufikiwa kwa urahisi.

◻ Hakikisheni kwamba kuna ufito wa kuzuia radi.

◻ Milango ya kutokea yapaswa kuwekwa alama iliyo wazi, kufikiwa kwa urahisi, na haipasi kufungwa wakati wa mikutano.

◻ Stoo na vyoo vyapaswa kuwa safi, vyenye utaratibu, na visiwe na vifaa vinavyoweza kuwaka moto haraka, vitu vya kibinafsi na takataka.

◻ Paa na michirizi zapaswa kukaguliwa na kusafishwa kwa ukawaida.

◻ Vitu vinavyoweza kusababisha kuteleza au kuanguka havipaswi kuwa katika vijia na maegesho ya magari.

◻ Mifumo ya umeme na ya kuingiza hewa yapaswa kukaguliwa na kudumishwa ifaavyo.

◻ Sehemu zozote zinazovuja zapaswa kurekebishwa haraka ili kuzuia matatizo ya unyevu.

◻ Jengo lapaswa kufungwa wakati ambapo hakuna mtu yeyote ndani ya jumba.

[Sanduku katika ukurasa wa 4]

Kutunza Jumba na Uwanja

◻ Nje: Je, paa, kuta, rangi, madirisha, na ishara ya Jumba la Ufalme ziko katika hali nzuri?

◻ Uwanja: Je, uwanja unadumishwa ifaavyo? Je, vijia, nyua, na maegesho yako katika hali nzuri?

◻ Ndani: Je, sakafu, mapazia, viti, vifaa vya umeme, rangi, kabati za vitabu, na vyumba vingine viko katika hali yenye kupendeza?

◻ Vifaa: Je, mifumo ya umeme, ya sauti, na ya kuingiza hewa inafanya kazi ifaavyo?

◻ Vyoo: Je, viko safi na vinafanya kazi ifaavyo?

◻ Hati za kutaniko: Je, nakala za hati za umiliki au hati nyingine zina habari za karibuni zaidi, ni sahihi, na zimehifadhiwa vizuri katika faili za kutaniko? Je, barua za msamaha wa kodi na ushuru zimewekwa katika faili za kutaniko?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki