Jivikeni Unyenyekevu
1 Kijana mmoja mchungaji anamtumaini Yehova na kumshinda shujaa mwenye nguvu. (1 Sam. 17:45-47) Tajiri avumilia misiba kwa subira. (Ayu. 1:20-22; 2:9, 10) Mwana wa Mungu ampa Baba yake sifa zote kwa sababu ya ufundishaji wake. (Yoh. 7:15-18; 8:28) Visa vyote hivyo vinaonyesha unyenyekevu ni muhimu. Vivyo hivyo, tunahitaji unyenyekevu ili kukabiliana na hali mbalimbali leo.—Kol. 3:12.
2 Katika Mahubiri: Tukiwa wahudumu Wakristo, tunawahubiria watu wote habari njema kwa unyenyekevu, hatuwabagui kulingana na jamii, utamaduni, au malezi yao. (1 Kor. 9:22, 23) Wengine wanapokataa ujumbe wa Ufalme kwa ujeuri au ufidhuli, hatuwajibu kwa ukali bali tunaendelea kwa unyenyekevu kuwatafuta wanaostahili. (Mt. 10:11, 14) Badala ya kujaribu kuwavutia wengine kwa ujuzi au elimu yetu, tunawaelekeza kwa Neno la Mungu, tukitambua kwamba lina nguvu kuliko maneno yetu. (1 Kor. 2:1-5; Ebr. 4:12) Kama Yesu, tunampa Yehova sifa zote.—Marko 10:17, 18.
3 Kutanikoni: Ni lazima Wakristo ‘wajifunge hali ya akili ya kujishusha chini kuelekea mtu na mwenzake.’ (1 Pet. 5:5) Tukiwaona wengine kuwa bora kuliko sisi, tutajitahidi kutafuta njia za kuwatumikia ndugu zetu badala ya kungoja watutumikie. (Yoh. 13:12-17; Flp. 2:3, 4) Hatutajiona kuwa wakubwa sana hivi kwamba hatuwezi kufanya kazi nyingine kama vile kusafisha Jumba la Ufalme.
4 Unyenyekevu hutusaidia ‘kuchukuliana mtu na mwenzake katika upendo’ na hivyo hudumisha amani na umoja kutanikoni. (Efe. 4:1-3) Hutusaidia kujitiisha kwa wale ambao wamewekwa rasmi kuongoza. (Ebr. 13:17) Hutuchochea kukubali shauri au nidhamu yoyote. (Zab. 141:5) Na unyenyekevu hutufanya tumtegemee Yehova tunaposhughulikia migawo yoyote tunayopewa kutanikoni. (1 Pet. 4:11) Kama Daudi, tunatambua kwamba mafanikio hayategemei uwezo wetu bali baraka za Mungu.—1 Sam. 17:37.
5 Mbele za Mungu Wetu: Zaidi ya yote, tunapaswa ‘kujinyenyekeza chini ya mkono wa Mungu wenye uweza.’ (1 Pet. 5:6) Tunapopata magumu, huenda tukatamani kitulizo ambacho Ufalme utaleta. Lakini kwa unyenyekevu tunaendelea kumngoja Yehova atimize ahadi zake kwa wakati wake. (Yak. 5:7-11) Kama Ayubu mwaminifu, hangaiko letu kuu ni kwamba ‘jina la BWANA libarikiwe.’—Ayu. 1:21.
6 Nabii Danieli ‘alijinyenyekeza mbele za Mungu wake’ na alikubaliwa na Yehova na akapewa mapendeleo mengi mazuri. (Dan. 10:11, 12) Vivyo hivyo, na tujivike unyenyekevu, tukijua kwamba “thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha BWANA ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.”—Mit. 22:4.