Onyesha Unawajali Watu Kikweli kwa Kuwatendea kwa Fadhili
1 Mwanamke mmoja aliyewachukia Mashahidi wa Yehova anasema hivi anapokumbuka jambo lililotukia alipokutana kwa mara ya kwanza na Shahidi mmoja: “Kwa kweli siwezi kukumbuka jambo tulilozungumzia, lakini ninalokumbuka ni jinsi alivyokuwa mwenye fadhili, na jinsi alivyokuwa mkarimu na mnyenyekevu. Kwa kweli nilihisi nimevutiwa naye.” Maneno hayo yanakazia umuhimu wa kuwajali kikweli watu tunaowahubiria.—Flp. 2:4.
2 Upendo Ni Wenye Fadhili: Njia moja ya kuonyesha kwamba tunawapenda watu ni kuwatendea kwa fadhili. (1 Kor. 13:4) Mtu mwenye fadhili huhangaikia sana hali za wengine naye hujitahidi kuwasaidia. Bila shaka, kuhubiri ni tendo la fadhili. Lakini kuwajali wengine kikweli kunahusisha mengi zaidi ya kuwahubiria tu. Mambo kama vile urafiki na adabu, mambo tunayosema na jinsi tunavyoyasema, jinsi tunavyowasikiliza na hata kuwatazama wengine, yataonyesha kwamba tunawajali kikweli.—Mt. 8:2, 3.
3 Pia, kuwahangaikia wengine kwa upendo kutatuchochea tuwasaidie kwa vitendo. Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, ndugu mmoja painia alifukuzwa na mwanamke mzee wakati mwanamke huyo alipogundua kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Alisema kwamba alikuwa amepanda ngazi jikoni ili abadilishe balbu ya taa wakati ndugu huyo alipobisha mlango. Ndugu huyo alisema: “Ni hatari kufanya hivyo ukiwa peke yako.” Mwanamke huyo alimkaribisha, kisha ndugu huyo akabadilisha ile balbu na kwenda zake. Mwana wake alipomtembelea muda mfupi baadaye ili kumjulia hali, mama yake alimweleza kilichokuwa kimetendeka. Mwana huyo alivutiwa sana na jambo hilo naye akamtafuta ndugu huyo ili amshukuru. Walikuwa na mazungumzo mazuri na mwana huyo akakubali funzo la Biblia.
4 Kwa kuwatendea watu kwa fadhili tunaiga upendo wa Yehova kwa watu, na tunapamba ujumbe wa Ufalme. Hivyo basi, nyakati zote na ‘tujipendekeze kuwa wahudumu wa Mungu, kwa kuwa wenye fadhili.’—2 Kor. 6:4, 6.