Mwige Mwalimu Mkuu Unapotumia Kitabu Biblia Inafundisha
1 Sikuzote Mwalimu Mkuu Yesu, alifafanua mambo kwa njia rahisi na inayoeleweka. Ili kuamsha fikira za wasikilizaji wake, aliwauliza maoni yao kwanza. (Mt. 17:24-27) Na alielekeza uangalifu katika Neno la Mungu. (Mt. 26:31; Marko 7:6) Alikuwa mwangalifu asiwachoshe wanafunzi wake kwa habari nyingi mno, akijua kwamba wataendelea kujifunza. (Yoh. 16:12) Yesu alipenda pia kujua ikiwa wanafunzi wake waliamini na kuelewa kile ambacho aliwafundisha. (Mt. 13:51) Kitabu Biblia Inafundisha kimeandaliwa kitusaidie kufanya vivyo hivyo pia.
2 Maswali ya Utangulizi: Unapoanza kufundisha sura mpya, ni vizuri kukazia uangalifu kwenye maswali ya utangulizi yaliyo chini ya kichwa kikuu. Uliza maswali hayo bila kutarajia majibu ili kuamsha hamu ya mwanafunzi kujifunza. Au unaweza kumwomba mwanafunzi atoe majibu mafupi kuhusu maswali hayo. Hakuna haja ya kujadili kwa muda mrefu majibu yake au kurekebisha majibu hayo. Unaweza tu kumshukuru kwa maoni yake na kuendelea na funzo. Majibu yake kwenye maswali ya utangulizi yatakusaidia kujua ni mahali gani utahitaji kukazia zaidi katika somo hilo.
3 Maandiko: Funzo linapaswa kutegemea maandiko. (Ebr. 4:12) Hata hivyo, hakuna haja ya kusoma maandiko yote yaliyoonyeshwa. Kazia yale yanayoonyesha msingi wa Kimaandiko wa imani yetu. Si lazima usome maandiko yanayoandaa habari za ziada. Kitabu Biblia Inafundisha kinaelezea kweli kwa njia rahisi. Fanya funzo liwe rahisi. Kazia hoja za msingi na uepuke kuzungumzia mambo mengi kuhusu somo hilo au kuingizia habari zisizohitajika.
4 Nyongeza: Kuna vichwa vya habari 14 ambavyo vinategemeza masomo ya msingi. Ni uamuzi wako ikiwa utataka kuzungumzia habari hizo wakati wa funzo. Ikiwa mwanafunzi wako ameelewa na anakubaliana na habari iliyo katika somo la msingi, unaweza kumtia moyo ajisomee mwenyewe maelezo ya ziada. Kwa mfano, ikiwa tayari mwanafunzi anaamini kwamba Yesu ni Masihi, hakuna haja ya kuchunguza pamoja naye nyongeza yenye kichwa “Yesu Kristo—Masihi Aliyeahidiwa” mnapozungumzia sura ya 4, “Yesu Kristo Ni Nani?” Lakini pindi nyingine, huenda ikafaa kuzungumzia habari iliyo katika nyongeza au sehemu yake wakati wa funzo.
5 Ukiamua kuchunguza habari ya nyongeza, utahitaji kutayarisha maswali mapema, na kusoma mafungu kama mfanyavyo kwenye somo la msingi. Au ikitegemea uhitaji wa mwanafunzi, huenda unaweza kutumia muda fulani wa somo kupitia habari ya nyongeza pamoja naye. Hilo litakusaidia kuhakikisha kwamba mwanafunzi wako ameelewa habari ambayo aliisoma peke yake.
6 Sanduku la Pitio: Sanduku mwishoni mwa kila sura lina maelezo ambayo kwa kawaida yanaandaa majibu ya maswali ya utangulizi. Unaweza kutumia maelezo hayo kurudia mambo makuu ya sura hiyo. Baadhi ya wahubiri wameona inafaa kusoma pamoja na mwanafunzi maelezo hayo na maandiko yanayoambatana nayo. Kisha wanawaomba wanafunzi wafafanue kwa ufupi jinsi maandiko hayo yanavyothibitisha maelezo yaliyotolewa. Hilo litamsaidia mwalimu kuona ikiwa mwanafunzi ameelewa mambo makuu ya somo na jinsi hoja hizo zinavyoungwa mkono na maandiko na ikiwa mwanafunzi anakubaliana nazo. Pia hilo linamsaidia mwanafunzi, kutumia Biblia kuthibitisha kweli kwa wengine.
7 Njia nzuri ya kutimiza huduma yetu ya kufundisha na kuwafanya watu kuwa wanafunzi, ni kwa kuiga njia zile ambazo Yesu alitumia kufundisha. (Mt. 28:19, 20) Kitabu Biblia Inafundisha kinaweza kutusaidia kufanya hivyo. Kitumie vizuri kuwafundisha wengine kweli kwa njia ya wazi, rahisi na inayopendeza.
[Maswali ya Funzo]
1. Yesu alifundishaje?
2. Tunaweza kutumiaje maswali ya utangulizi yaliyo mwanzoni mwa kila sura?
3. Tunawezaje kufanya funzo liwe rahisi?
4. Ni nini kitakachoamua ikiwa tunapaswa kusoma habari ya nyongeza wakati wa funzo?
5. Tunaweza kufanyaje ikiwa tumeamua kutumia habari ya nyongeza?
6. Sanduku la pitio mwishoni mwa kila sura linaweza kutumiwaje?
7. Tunaweza kutumiaje kitabu Biblia Inafundisha kutimiza huduma yetu?