Kujifunza Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?
1 Mojawapo ya mambo yenye kufurahisha katika Makusanyiko ya Wilaya ya “Utii wa Kimungu” ilikuwa kutolewa kwa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Tutatumia sana kitabu hicho katika utumishi wa shambani, hasa tunapoongoza mafunzo ya Biblia. Hivyo, tunahitaji kukifahamu vizuri. Tutaweza kukifahamu vizuri tutakapojifunza kitabu hicho katika Funzo la Kitabu la Kutaniko kuanzia juma la Aprili 17, 2006.
2 Mwangalizi wa Funzo la Kitabu la Kutaniko atakazia uangalifu maswali yaliyo mwanzoni mwa kila sura. Kisha funzo litaongozwa kwa kutumia maswali yaliyo chini kwenye kila ukurasa. Maandiko yanayokazia jambo kuu yatasomwa na kuzungumziwa. Kisha sanduku “Mambo Ambayo Biblia Inafundisha” lililo mwishoni mwa kila sura litasaidia kurudia habari hiyo kwa kuwa sanduku hilo lina majibu ya Kimaandiko kwa maswali yaliyo mwanzoni mwa kila sura. Utafurahia kutoa maelezo kwa kuwa kitabu hicho kinazungumzia mambo kwa njia ya wazi, rahisi, na yenye kupendeza.
3 Nyongeza ya kitabu hicho ina habari nyingi kuhusu mambo mbalimbali. Tutatumia habari hiyo wanafunzi wa Biblia wanapohitaji habari ya ziada kuhusu jambo fulani. Tutapitia sehemu fulani za nyongeza wakati wa Funzo la Kitabu la Kutaniko. Msomaji wa funzo la kitabu atasoma sehemu zote za nyongeza zitakazozungumziwa, ilhali sehemu ndefu zaidi zinaweza kusomwa hatua kwa hatua. Hakuna maswali ya funzo katika nyongeza. Lakini mwangalizi anaweza kuwaomba wahudhuriaji watoe maelezo kwa kuuliza maswali yanayokazia mambo makuu.
4 Katika Funzo la Kitabu la Kutaniko tutajifunza haraka kitabu Biblia Inafundisha. Hatutazamiwi kukisoma haraka hivyo tunapojifunza na wengine katika utumishi, hasa ikiwa wana ujuzi kidogo tu wa Biblia au hata hawana. (Mdo. 26:28, 29) Tunapoongoza mafunzo ya Biblia, tutahitaji kuzungumzia maandiko kwa undani zaidi, tufafanue mifano, na kadhalika. Kwa hiyo, weka mradi wa kuwapo kila juma ili unufaike kikamili tunapojifunza kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?