Jinsi ya Kutumia Kitabu “Upendo wa Mungu” Kuongoza Mafunzo ya Biblia
1. Kusudi la kitabu “Upendo wa Mungu” ni nini?
1 Tulifurahi sana tulipopokea kitabu kipya “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” katika Kusanyiko la Wilaya la “Kuongozwa na Roho ya Mungu”! Kama ilivyotangazwa, kitabu hiki kimekusudiwa kutusaidia kujua na kupenda sheria za Yehova kuhusu mwenendo na si kufundisha mafundisho ya msingi ya Biblia. Hatutatumia kitabu hiki katika kazi ya nyumba kwa nyumba.
2. Kitabu hiki kitatumiwaje, na ni nani wanaopaswa kujifunza kitabu hiki?
2 Kitabu hiki ni kitabu cha pili ambacho tutajifunza pamoja na wanafunzi wa Biblia waliomaliza kujifunza kitabu Biblia Inafundisha. Kumbuka kwamba maendeleo ya watu ya kujifunza na kufuata kweli hutofautiana. Kila mwanafunzi anapaswa kufundishwa kulingana na uwezo wake. Hakikisha kwamba mwanafunzi ameelewa vizuri habari iliyozungumziwa. Kwa kawaida, kitabu hiki hakipaswi kutumiwa kuanzisha mafunzo ya Biblia na watu ambao huenda tayari wamejifunza vitabu kadhaa wakati uliopita lakini ambao hawahudhurii mikutano ya kutaniko na inaonekana wazi kwamba hawataki kuishi kupatana na kweli za Biblia walizofundishwa.
3. Tunapaswa kufanya nini ikiwa sasa tunaongoza funzo katika kitabu Mwabudu Mungu?
3 Ikiwa kwa sasa unaongoza funzo katika kitabu Mwabudu Mungu na umefikia sura za mwisho, unaweza kumaliza kujifunza kitabu hicho na kumtia moyo mwanafunzi asome kitabu “Upendo wa Mungu” peke yake. La sivyo, itakuwa vema kuanza kujifunza kitabu kipya kuanzia mwanzo. Kama ilivyo na kitabu Biblia Inafundisha, si lazima kuzungumzia habari zilizo kwenye nyongeza.
4. Tunapaswa kufanya nini mwanafunzi wetu akibatizwa kabla ya kumaliza kitabu Biblia Inafundisha au “Upendo wa Mungu”?
4 Mwanafunzi akibatizwa kabla ya kumaliza kujifunza vitabu vyote viwili, funzo linapaswa kuendelea hadi mmalize kitabu “Upendo wa Mungu.” Ingawa mwanafunzi amebatizwa, bado unaweza kuripoti muda uliotumia, ziara ya kurudia, na funzo. Mhubiri anayeandamana nawe na anayeshiriki katika funzo pia anaweza kuhesabu muda huo.
5. Kitabu “Upendo wa Mungu” kinaweza kutumiwa jinsi gani kuwasaidia wahubiri ambao hawajahubiri kwa muda fulani?
5 Ukiombwa na ndugu aliye katika Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ujifunze Biblia na mtu ambaye hajashiriki katika kazi ya kuhubiri kwa muda fulani, huenda ukaombwa kujifunza naye sura hususa katika kitabu “Upendo wa Mungu.” Hakuna haja ya kuongoza mafunzo kama hayo kwa muda mrefu. Kitabu hiki kipya ambacho kimekusudiwa kutusaidia kubaki katika “upendo wa Mungu,” ni uandalizi mzuri kama nini!—Yuda 21.