Sanduku la Swali
◼ Ni vitabu gani viwili vinavyopaswa kutumiwa tunapojifunza na watu wanaopendezwa?
Kitabu Biblia Inafundisha ndicho kifaa kikuu tunachotumia kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani. Ingawa si vibaya kutumia kichapo kingine kama vile trakti kuanzisha funzo la Biblia, tunapaswa kubadilisha na kuanza kutumia kitabu Biblia Inafundisha haraka iwezekanavyo. Kumekuwa na matokeo mazuri kitabu Biblia Inafundisha kilipotumiwa kuanzisha mafunzo.
Baada ya kumaliza kitabu Biblia Inafundisha na mwanafunzi anafanya maendeleo, kitabu Mwabudu Mungu kinapaswa kutumiwa. (Kol. 2:7) Ukurasa wa 2 unaeleza kusudi la kitabu hicho: “Biblia inawahimiza wote wanaompenda Mungu ‘wafahamu kiakili . . . upana na urefu na kimo na kina’ cha kweli zake muhimu sana. (Efe. 3:18) Kitabu hiki kimechapishwa kwa kusudi hilo. Tunatumaini kwamba kitakusaidia kukua kiroho na kukuwezesha kuendelea kutembea kwenye njia nyembamba inayoongoza kwenye uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu.”
Ikiwa mwanafunzi anastahili kubatizwa kabla ya kumaliza vitabu vyote viwili, funzo linapaswa kuendelea hadi kitabu cha pili kikamilishwe. Ingawa mwanafunzi amebatizwa, anayeongoza funzo hilo bado anaweza kuhesabu wakati anaotumia, ziara za kurudia, na funzo. Pia mhubiri anayehudhuria funzo hilo na kushiriki anaweza kuhesabu wakati huo.