Wafundishe Watoto Wako Kumsifu Yehova
1 Zaburi 148:12, 13 inawatia moyo wavulana na wasichana “walisifu jina la Yehova.” Maandiko yana mifano mingi ya watoto waliofanya hivyo. Kwa mfano, “Samweli alikuwa akihudumu mbele za Yehova, akiwa mvulana.” (1 Sam. 2:18) “Msichana mmoja mdogo” ndiye aliyemwambia mke wa Naamani kwamba nabii wa Yehova huko Israeli anaweza kumponya Naamani ukoma wake. (2 Fal. 5:1-3) Yesu alipoingia hekaluni na kufanya matendo yenye nguvu, “wavulana” ndio waliopaaza sauti na kusema: “Mwokoe Mwana wa Daudi, tunaomba!” (Mt. 21:15) Wazazi wanaweza kuwafundishaje watoto wao kumsifu Yehova?
2 Kwa Mfano: Kabla ya kukazia kweli katika mioyo ya watoto wao, akina baba Waisraeli waliagizwa kwanza wampende Yehova na waweke sheria zake katika mioyo yao wenyewe. (Kum. 6:5-9) Ikiwa utazungumza mambo yenye kujenga kuhusu huduma na kuifanya kuwa sehemu ya ratiba yako ya kila juma, watoto wako wataona huduma kuwa muhimu na yenye kuridhisha.
3 Dada mmoja anakumbuka hivi: “Nilipokuwa nikikua, familia yetu ilikuwa na zoea la kushiriki katika huduma ya shambani mwishoni mwa kila juma. Niliona kwamba wazazi wangu walifurahia sana kuhubiri. Tuliiona huduma kuwa jambo lenye kufurahisha.” Dada huyo alistahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa akiwa na umri wa miaka saba, na kufikia sasa amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 32.
4 Wazoeze Hatua kwa Hatua: Wahusishe watoto wako mnapokuwa katika huduma. Wanaweza kubisha mlango, kumpa mwenye nyumba trakti, au kusoma andiko. Hilo litawafanya wafurahie sana huduma na kuwasaidia wawe na uhakika zaidi wanapohubiri ujumbe wa Ufalme. Wanapoendelea kukua, wanapaswa kushiriki zaidi katika huduma. Kwa hiyo, wasaidie wafanye maendeleo na wafikirie miradi ya kiroho.
5 Zungumza na wazee mara unapohisi kwamba watoto wako wanastahili kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa na watoto wenyewe wakisema kwamba wanataka kufanya hivyo. Kuwa wahubiri kutawachochea wachukue kwa uzito jukumu lao la kumsifu Yehova. Kumbuka kwamba si lazima mtoto awe na ujuzi kama wa mtu mzima aliyebatizwa ili astahili. Je, mtoto wako anaelewa mafundisho ya msingi ya Biblia? Je, anafuata viwango vya Biblia vya maadili? Je, anataka kushiriki katika huduma na kutambuliwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova? Ikiwa ndivyo, wazee wanaweza kuamua kuwa anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa.—Ona kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, ukurasa wa 79-82.
6 Kuwafundisha watoto kumsifu Yehova kutoka moyoni huhitaji jitihada. Hata hivyo, kuona watoto wao wakifanya maendeleo ya kiroho ni mojawapo ya mambo machache ambayo huwaletea wazazi shangwe nyingi sana. Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba Yehova anafurahi watoto wanapowaambia wengine kuhusu kazi zake za ajabu.
[Maswali ya Funzo]
1. Je, watoto wanaweza kumsifu Yehova?
2. Kwa nini ni muhimu wazazi wawawekee watoto wao mfano mzuri?
3. Dada mmoja alinufaikaje na mfano aliowekewa na wazazi wake?
4. Kuwazoeza watoto hatua kwa hatua kunahusisha nini?
5. Ni nini kinachohitajiwa ili mtoto astahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa?
6. Kwa nini ni muhimu wazazi wawazoeze watoto wao?